ads 728x90 B

Kifo cha wakili tajiri mwanamke, chanzo mapenzi!




Mwandishi Wetu

DAIMA tuendelee kukumbushana kuhusu umuhimu wa uaminifu. Tuzingatie na kukiri kuwa usaliti siyo kosa la bahati mbaya ni uamuzi wa makusudi. Hajapata kutokea msaliti akatenda dhambi hiyo pasipo kujua, eti baada ya tendo ndiyo akagundua, hiyo haipo!
Ongeza kitu kichwani kwa stori ya Sarah Johnson. Baada ya kutenda dhambi ya usaliti na mumewe kujua, alianza kuteseka ndani kwa ndani, akijilaumu na kujilaumu.
Pokea ukweli huu; Mtu anapotenda usaliti hujidanganya kuwa itabaki kuwa siri. Mbaya zaidi hujiaminisha kuwa ‘usaliti’ wake hautajulikana.
Hakuna maandalizi ya kisaikolojia ambayo unaweza kuyafanya na yakakusaidia pindi tendo lako la usaliti litakapogundulika. Kila aliyegundulika, aibu ilimshika na akaishia kujuta.
Sarah, mwanamke msomi mtaalam wa sheria, yeye baada ya tendo lake la usaliti kugundulika, aliona mambo ni mazito, akaishi kwa mateso kwa takriban miezi minne, mwisho akaona afadhali kukatisha maisha yake.
Hakuna anayeweza kufurahia kifo cha mwingine, ila haipingiki kuwa Sarah alijipeleka mwenyewe kwa Mungu baada ya kuona dunia imegeuka mzigo mzito kichwani kwake, kisha Mfalme wa Mbingu na Ardhi naye akampokea.
Sarah, wakili tajiri, aliyekuwa akiishi kwenye nyumba yenye thamani ya shilingi bilioni 30 (pauni milioni 12), unaweza kuwaza alikuwa kwenye wakati mzuri kiasi gani wa kufurahia maisha. Halafu katika tafakuri yako ongezea kuwa amejiua mwenyewe.
Alikuwa mwanamke tajiri, aliyepata kila alichotaka. Jumba lake lililopo Chester Square, ndani ya Wilaya ya Belgravia, Jiji la London, Uingereza, lilikuwa na kila aina ya burudani. Aliendesha magari ya kifahari jinsi alivyotaka.
Mume wa Sarah, David Johnson, ni mtu mwenye uwezo pia. Na David hakuwa akimbughudhi wakili huyo ila tu mwenyewe alishindwa kupata utulivu tangu kitendo chake cha usaliti kilipogundulika.
Baba yake Sarah, Graham Parr, ni mfanyabiashara mkubwa. Alikuwa karibu na binti yake kumpa chochote kile ambacho angekihitaji yeye binafsi na familia yake lakini Sarah hakuona kama kuna kingine kinachoweza kubeba thamani ya heshima yake baada ya mumewe kuubaini usaliti wake.
Sarah, alimweleza mara kwa mara daktari wake wa saikolojia, aliyejitahidi kumtibu kwa miezi minne: “Mimi siyo mama bora, siyo mke bora.”
Dk Shirley Radcliffe, mtaalamu wa saikolojia aliyekuwa akimtibu Sarah, alisema: “Ugonjwa wa Sarah ulitokana na kujiona mwenye hatia ndani yake. Baada ya yote kutokea, alikuwa akisema kwa msisitizo kuwa yeye siyo mama bora. Aliona heshima yake yote imetoweka. Na ukiniuliza maoni yangu, nitakujibu kuwa hiyo inaweza kuwa sababu ya yeye kujiua.”
Sarah ambaye mpaka anajiua alikuwa na umri wa miaka 36, inaelezwa kuwa tangu mumewe alipojua kuhusu usaliti wake, alijiingiza kwenye vitendo vya ulevi na zipo nyakati alilewa mpaka kuzimika. Rekodi zinaonesha kuwa alianza ulevi Januari mwaka huu.
Daktari wake alimtibu mpaka akaonekana kama anaelekea kupata nafuu, lakini Aprili 27, mwaka huu, alijirusha mbele ya treni , ilipokuwa kwenye mwendo, Stesheni ya Victoria, London.
Zaidi, Sarah aliwahi kulazwa kwenye hospitali ya matatizo ya akili, The Priory, ambayo huhudumia watu mashuhuri na matajiri kutokana na gharama zake kuwa kubwa. Pamoja na hivyo, hakuweza kupona.
Mataabikiko ya usaliti ni mbaya mno; Madaktari bingwa Uingereza hawakumsaidia, pombe zikazidi kumvuruga akili. Kila alipokumbuka dhambi aliyotenda ya kusaliti ndoa alijiona mwenye hatia, mwisho akaona bora kuutanguliza mwili wake kaburini.
Kwa mujibu wa taarifa za ndani ya familia, Sarah alianza kunywa pombe saa 5 asubuhi, alitumia vodka na kila jioni aligeukia bia.
Sarah, aliamini pombe ndizo zinaweza kumsaidia kwa maelezo kuwa kugundulika kwake kwa mambo aliyokuwa anayafanya kwa siri, kulisababisha furaha yake yote ya maisha kutoweka.
Ukiachana na Dk Radcliffe, ndani ya Hospitali ya The Priory alilazwa mara mbili, Februari na Aprili 2015. Na alijiua akiwa hajamaliza siku nyingi tangu alipotibiwa.
Daktari wa saikolojia ya akili katika Hospitali ya The Priory, Dk Neil Brener ambaye ndiye alikuwa anamhudumia Sarah, alisema: “Tatizo lake kubwa lilihusu masuala binafsi ndani ya familia, na alikuwa akitumia pombe kwa wingi ili kutuliza mawazo.
“Hakuwahi kuwa na matatizo ya kisaikolojia huko nyuma. Mawazo pekee yaliyomsumbua ni kwamba alimwangusha kila mmoja ndani ya familia yake, mume wake na watoto wake. Kwa maana hiyo sababu ya kujiua itakuwa hiyo.”
Dk Brener alisema kuwa siku ambayo Sarah aliruhusiwa kutoka Hospitali ya The Priory, alifurahi kwa sababu alimuona mgonjwa wake akiwa kwenye maendeleo mazuri ya kiafya.
Daktari huyo aliongeza: “Siku tunamruhusu hakuwa na mawazo ya kujiua, alikuwa na maendeleo mazuri kabisa kiakili, na alikuwa mzungumzaji sana.”
Inaelezwa kuwa Aprili 26, 2015, Sarah alikuwa na ahadi ya kumuona Dk Brener lakini hakwenda, wala hakutoa sababu yoyote.
Asabuhu ya siku iliyofuata (Aprili 27), mume wa Sarah, David, aliamka na kukuta mkewe hayupo na aliona karatasi aliyoacha ujumbe kwamba anakwenda kujiua kwa sababu ya kuzidiwa na mzigo mzito wa mawazo ya kujiona mwenye hatia.
Kwa karatasi hiyo, David, 37, aliwahi polisi kutoa taarifa ya kutoweka kwa mkewe na kuhusu uwezekano wa kufanya jambo baya, lakini hakuna kilichosaidia kuokoa maisha ya Sarah, kwani muda huo tayari roho ilikuwa imeshatengana na mwili.
Ilibainika kuwa Sarah aliwasili Stesheni ya Victoria saa 11:30 asubuhi, na alishangaashangaa kwa takriban dakika 50 kabla ya kujirusha saa 12:20 asubuhi mbele ya treni ya ardhini inayotumia umeme, iliyokuwa inatembea.
Mpelelezi Steve Tucker alisema, kabla Sarah hajafariki dunia, alionekana akijiandaa kujirusha, kwa hiyo hivyo ni wazi dhamira yake alitembea nayo kwa muda mrefu.
Tucker alisema: “Picha ya kwanza inayomuonesha Sarah kupitia kamera za usalama (CCTV), ilikuwa saa 11:37 asubuhi. Alikuwa akizunguka zunguka kutoka upande mmoja kwenda mwingine.
“Saa 12:00 asubuhi alionekana kwenye kamera katika sehemu ya kupandia abiria ya kaskazini. Kwa kufuatilia hatua zake, niliingiwa na wasiwasi kuwa kuna kitu anataka kufanya. Nilipata hisia hizo kwa sababu alikuwa anakwenda mbele kisha kurudi nyuma kwa mtindo wa kushangaza.
“Saa 12:20 asubuhi, kamera zinamuonesha anatazama upande ambao treni inapita.”
Taarifa za Kitengo cha Ambulance zinasema kuwa Sarah alichukuliwa stesheni akiwa na majeraha makali na ilionekana wazi kuwa asingeweza kupona.
Kwa upande mwingine, taarifa za simu yake aina ya iPhone, ilikutwa na historia ya intaneti, zilizoonesha kuwa Sarah kupitia mtandao wa Google, kwa mara ya mwisho alitafuta ‘idadi ya vidonge vya paracetamol ambayo mtu mzima akimeza anaweza kufariki dunia.’
Uchunguzi wa mwili wa marehemu ulionesha kuwa Sarah hakuwa na kiwango chochote cha pombe, kuonesha kuwa kujiua kwake hakukutokana na aina yoyote ya kilevi.
UNACHOPASWA KUCHUKUA
Kifo cha Sarah kiwe na mambo mawili yenye kufundisha. Kwanza ni usaliti, athari yake ni kubwa mno baada ya kugundulika.
Usiseme itakuwa siri, amini usiamini kuwa ipo siku itajulikana na wewe utakosa mahali pa kuiweka sura yako kwa aibu.
Usisubiri majuto ya baadaye na hata kufikia uamuzi mgumu na uliojaa maumivu makali kama wa Sarah, jenga utaratibu wa kujikosoa kila Shetani anapokuvuta kwenye njia yake.
Mfumo wa kuukataa usaliti ni kuzishtukia dalili zote zinazoletwa na Shetani. Usingoje kusema “Shetani alinipitia.” Fanya kumzuia asiingie kabisa kwenye anga zako.
SAMEHE ANAYEJUTA
Kama mwenzio amekusaliti na unajiridhisha kuwa anajuta kwa alichokifanya, jaribu kuyatibu maumivu uliyonayo kisha umsamehe.
Usisamehe kama hujapona. Matokeo yake leo utamwambia umemsamehe kesho unalianzisha tena. Pona majeraha kwanza na baada ya hapo toa msamaha wa kweli.
Kikubwa ni kwamba ni heri kumsamehe anayejuta kwa kosa alilofanya, maana atakuwa mwangalifu siku zijazo, kuliko kwenda kumvamia mwingine ambaye anaweza kukuibulia maumivu mapya.
MASKINI SARAH KAACHA MTOTO MDOGO KABISA
Sarah amekwenda, amemwacha mumewe na watoto wake wakiwa kwenye ukiwa mkubwa. Maumivu makubwa ni kwamba mwanaye wa mwisho ndiyo kwanza alimwacha akiwa ametimiza umri wa miaka mitatu.
David (mume wa Sarah), hajatoa tamko lolote au kuelezea kile hasa ambacho marehemu mke wake alikosea, yupo kimya, anasitiri aibu ya mwandani wake lakini ndani yake kuna donda kubwa, kusalitiwa na kumpoteza mke. Labda alimsamehe lakini Sarah hakujisaheme kabisa. Tuwe waaminifu siku zote!


Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment