ads 728x90 B

UKIPANDA CHUKI, UTAIVUNA, UTAIZALISHA!




MALKIA Mary I, alizaliwa Februari 18, 1516, alikufa Novemba 17, 1558. Huyu alikuwa Malkia wa England na Ireland kuanzia mwaka 1553 mpaka kifo chake.
Ni mtoto wa Mfalme Henry VIII na Catherine wa Aragon. Malkia Mary alibatizwa jina la Mary wa Damu (Bloody Mary). Alikuwa Mkatoliki na kipindi cha utawala wake, aliua viongozi wote maarufu wa madhehebu ya Protestant, hivyo kusababisha waumini wengi kukimbia nchi.
Naam! Chuki ukiipanda, utaivuna na kuizalisha! Mary alitenda ukatili huo kama sehemu ya kulipiza yale ambayo mama yake mzazi, Catherine wa Aragon alitendewa.
Ukatoliki na madhehebu yenye kuupinga Ukatoloki (Uprotestant), kwa pamoja uliyagharamu maisha ya Catherine wa Aragon (mama wa Malkia Mary I), na sababu kuu ni baba yake mzazi, yaani Mfalme Henry VIII.
Pokea simulizi hii uone jinsi ambavyo chuki inapopandwa, huvunwa na kuzaa.
Ni kwamba Henry asingekuwa Mfalme wa Uingereza kama asingemuua kaka yake, Arthur Tudor, ambaye alikuwa anangoja tu baba yake Mfalme Henry VII afariki dunia kisha yeye atawazwe ufalme.
Arthur alikuwa Prince wa Wales na mkewe, Catherine wa Aragon ndiye alikuwa Princess wa Wales.
Henry VIII alimuua Arthur, na ili atawazwe kuwa Mfalme wa Uingereza, ilibidi atimize sharti la kumuoa Catherine wa Aragon ambaye alikuwa anasubiri wakati ufike awe malkia (The Waiting Queen).
Baada ya kufunga ndoa na Catherine, alitawazwa kuwa mfalme, kisha Catherine akawa malkia wa Uingereza.
Tambua kuwa Henry VIII alimuoa Catherine kwa sababu tu ya ufalme, hivyo hakuwa na mapenzi naye ya dhati.
Basi baadaye akatokea mtumishi wa Catherine, anayeitwa Anne Boleyn. Mfalme Henry akampenda Anne, akamfanya kimada wake, na aliponogewa na penzi akataka kumtaliki Catherine ili amuoe Anne.
Mfalme Henry VIII kwa kutumia ufalme wake, akadhani inawezekana kupindisha sheria za Kikatoliki, kwamba ndoa ni moja. Hivyo basi, alimuomba Kiongozi wa Kanisa Katoliki wakati huo, Papa Clement VII, amruhusu amtaliki Catherine kisha amuoe Anne.
Papa Clement VII alikataa ombi hilo, akamsisitizia kuwa ndoa ni moja kisheria na kwamba talaka haikubaliki.
Kwa hasira, Mfalme Henry VIII alimkashifu Papa Clement VII, kwamba siyo kiongozi wa Kanisa duniani, bali ni askofu tu wa Roma.
Baada ya hapo Mfalme Henry VIII alianzisha madhehebu ya Anglikana. Ukatoliki ukapigwa marufuku Uingereza. Kisha Mfalme Henry VIII alimtaliki Catherine na kumuoa Anne chini ya Uanglikana.
Maisha ya Catherine yakawa magumu mno, aliteswa mno na Mfalme Henry VIII na Anne. Mfalme Henry VIII hakutunza heshima ya Catherine kama mwanamke aliyemfanya awe mfalme, vilevile mama wa watoto wake.
Mateso yote ambayo Catherine alitendewa, Mary aliyaona. Akamuona baba yake adui, kwani hakumpenda mama yake na alishuhudia. Aliwachukia wapinga Ukatoliki kwa sababu aliwaona kama maadui wa mama yake.
Baadaye Catherine alifariki dunia. Kifo kilijaa utata mkubwa. Anne alidaiwa kumuua Catherine kwa jeuri aliyokuwa anapewa na Mfalme Henry VIII. Yote hayo Mary aliyaona!
Chuki ukishaipanda lazima uivune; Unafiki wa Anne na ubaya wote aliomtendea Catherine, ulimrudia baada ya kila kitu kujidhihirisha kwa Mfalme Henry VIII. Anne Boleyn akahukumiwa kuuawa, hivyo kuvuna ile chuki yake kwa Catherine.
Mfalme Henry VIII kwa shingo upande alilazimika kukubali mke wake kipenzi auawe. Alivuna chuki ambayo aliipanda kwa kumuua kaka yake, kisha kumtesa Catherine.
Mfalme Henry VIII alizalisha chuki; Kwani mwanaye Mary baada ya kutawazwa kuwa malkia wa Uingereza, kumbukumbu za mateso ya mama yake zilimjia na kuanza kumwaga damu ovyo kwa Waprotestanti.
Alitaka watu wote wawe Wakatoliki. Na hiyo ndiyo ikawa sababu ya ukatili wote alioufanya. Na hayo ndiyo matunda ya chuki, iliyoanzia kwa baba yake.
Chuki ni kama tindikali, ukiimwaga juu ya kabati, baada ya muda utakuta imefika sakafuni, yaani kabati lenyewe na nguo, vitakuwa vimetafunwa na makali yake.
Daud alianza chuki kwa kumtwaa Bathsheba ambaye ni mke wa askari wake, Uriah. Chuki ya Daud haikuishia hapo, akaagiza Uriah auawe, na kweli, kijana asiye na hatia akauawa. Kisa mke wake ni mzuri, amependwa na Mfalme Daud.
Ona jinsi Daud alivyovuna na kuizalisha chuki kwenye familia yake; Kwanza kabisa Amnon ambaye ni mtoto wa kiume wa Daud, alimbaka dada yake Tamar. Watoto wa mfalme, yaani mtu na dada yake, kutenda dhambi ya ngono, tena katika njia ya ubakaji.
Haikuishia hapo; Absalom, mtoto wa kiume wa Mfalme Daud, alifanya mapenzi na wake wa baba yake. Zaidi, akamuwinda baba yake amuue.
Absalom alitengeneza jeshi lake la kumkabili baba yake. Ukisoma Biblia 2 Samuel, utaona Daud akiumizwa na jinsi mwanaye alivyogeuka adui yake, hadi kuutaka uhai wake.
Mwisho, ilibidi askari waaminifu wa Daud wamuue Absalom. Japo Daud aliumia sana mwanaye kuuawa kiasi cha kutamani bora angekufa yeye Absalom abaki, lakini matokeo yalikuwa hivyo. Chuki ina tabia kustawi na kumlazimisha aliyeipanda aivune na kuizalisha.
Mary Ann Cotton, alizaliwa Oktoba 1832, alikufa Machi 24, 1873. Wakati akiwa mdogo, alijifunza kuwachukia wanaume kutokana na jinsi mama yake alivyopata mateso.
Matokeo yake, mwanamke huyo raia wa Uingereza, aliwaua watoto wake nane kwa nyakati tofauti, wote kwa kuwawekea sumu. Aliolewa mara mbili na waume zake wote aliwaua kwa sumu. Vifo vya watoto na waume zake, vinafanana. Alinyongwa baada ya kukutwa na hatia ya kutenda unyama huo.
Usizalishe chuki ndugu yangu, gharama yake ni kubwa. Inaweza kukukuta wewe mwenyewe au hata kizazi chako.
Chuki ina tabia ya kusafiri. Ukimchukia mtu fulani na kizazi chake kinapokea. Unaweza kujikuta unazalisha watoto maadui, baada ya wazazi kupanda chuki na kuondoka duniani kabla ya kupata suluhu.
Ni chuki za kurithi ndizo zilizosababisha Isabella wa Castile aingie kwenye orodha ya wanawake katili kuwahi kutokea duniani.
Isabela ambaye alizaliwa Aprili 22, 1451 na kufariki dunia Novemba 26, 1504, alikuwa Malkia wa Hispania.
Utawala wake ulikuwa wa kiimla hasa. Pamoja na udikteta wake, Machi 31, 1492, alianzisha mpango wa kudhibiti uasi Kanisa Katoliki (Inquisition).
Alimteua Tomas de Torquemada kuwa kamanda wa kusafisha watu ambao siyo Wakatoliki nchini humo. Kipindi hicho, watu wengi wasio Wakatoliki walipoteza maisha, huku Waislam na Wayahudi wapatao 200,000 wakiikimbia nchi hiyo.
Chuki ni ugonjwa mbaya mno na unaambukiza (communicable disease), tena huwezi kuuweka katika kundi moja na magonjwa yasiyoambukiza (non communicable diseases) kama ilivyo presha au kisukari.
Wapo wafanyabiashara walikuwa na uhasimu mkubwa, na matokeo yake watoto wao wakarithi chuki na hata kuuana.
Walioanzisha uhasama kati ya Wahutu na Watutsi walifariki dunia miaka mingi kabla ya vita ya kimbari, iliyogharimu maisha ya watu zaidi ya watu milioni 1.2 nchini Rwanda mwaka 1994. Hii ina maana kuwa wanaorithi chuki, huivalia njuga kuliko walioianzisha.
Chuki kati ya Palestina na Israel, walioianzisha walishatangulia mbele ya haki miaka dahari na dahari iliyopita, lakini mpaka leo watu wanauana. Chuki ina kawaida ya kuishi na kuhama kutoka kizazi kimoja hadi kingine.
Walioanzisha chuki ya wakulima na wafugaji wala wao hawakuuana, walinuniana na kutishana tu lakini waliorithi wanauana na kuchomeana nyumba. Chuki ina hulka kama risasi, inapoingilia kuna tundu padogo, ila inapotokea tundu lake ni kubwa.
Acha kutengeneza chuki na mtu leo, maana huwezi kujua mbeleni athari zake ni kubwa kiasi gani.
Usipende kutangaza chuki na watu wengine, pengine wanaokupenda wakaichukulia kwa uzito kuliko wewe mwenyewe.
Labda nikufahamishe kitu, kwamba hata upendo na undugu huambukiza. Ukiwapenda watu, na kizazi chako kitakuja kuwapenda. Ruhusu upendo usambae.
Huwezi kujua kuwa chuki zako zinaweza kuwapa wakati mgumu watoto au ndugu zako kwa kiasi gani.
Hujawahi kuona mtu anagombana na hasimu wake, lakini anakwenda kulipiza kwa mtoto wa adui yake? Au mkewe? Au hata wazazi?
Inawezekana kuwa na maisha bila chuki. Yafanye maisha yako yawe rahisi, vilevile warahisishie watoto au ndugu zako maisha yao, kwa kutowaachia urithi wa chuki. Chuki ni mzigo haramu, usiwabebeshe.
Ishi na watu vizuri kisha hata baada ya kuondoka kwako, kizazi chako kitafaidi matunda mema. Maisha yenye kujengwa na upendo ni ulinzi kwako binafsi na familia yako. Ni msaada kwa kizazi chako utakapokuwa umeondoka.
Wapo watu watalazimisha chuki, wewe tabasamu mbele yao. Usiwape nafasi ya kustawisha chuki zao. Wewe siyo shamba lenye rutuba ya kustawisha chuki.
Ndiyo, kama mtu anakuchukia kisha akafanikiwa kuifanya chuki yake istawi juu yako, maana yake wewe ni shamba bora lenye kustawisha chuki. Usikubali. Ladha ya maisha bila chuki ni tamu asikwambie mtu.
Akijitahidi kupandikiza chuki kwako, wewe pandikiza upendo kwake, ongeza zaidi na kwa wengine. Ifanye chuki yake ikose nguzo kwenye maisha yako. Ni kawaida kwamba chuki ikikosa nguvu kwa mkusudiwa, humrudia mwenye nayo.
Asante.
Ndimi Luqman Maloto

Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment