NA LUQMAN MALOTO
JANA (Machi 9), nilipigiwa simu na
mtangazaji wa Clouds Media Group, Soud Brown ambaye ni mtayarishaji mkuu
wa kipindi cha XXL, akitaka maoni yangu kama mwandishi wa habari,
vilevile mchambuzi wa masuala ya sanaa.
Mada aliyotaka nichambue
ni namna ambavyo familia za wasanii zinaweza kuendelea kunufaika kupitia
sanaa ya ndugu yao hata baada ya msanii mwenyewe kuwa ameshafariki
dunia.
Nikiri kuwa ni mada nzuri na ya kikubwa. Kupitia kwenye
simu sikuweza kumpongeza Soud kwa mawazo mazuri, vilevile sikumshukuru
kwa kunishirikisha, maana wachambuzi wapo wengi na wenye viwango vikubwa
kabisa. Ila hapa naomba nimpongeze na kumshukuru.
Nilichokizungumza na Soud, nimeona bora pia nikiweke kwenye maandishi ili kusambaza ujumbe na maarifa kiduchu kwa wengine.
Kwanza msanii huwa hafi ila huipisha dunia baada ya wito wa Mungu.
Duniani kote huwa hivyo, ni Tanzania na nchi chache ambazo hazithamini
umuhimu wa sanaa na kuwekeza kwenye sanaa ndiyo wasanii hufa.
Mathalan, Steven Charles Kanumba ‘The Great’ amekufa. Ndiyo amekufa
jumla. Sasa hivi wanasimuliana “Kanumba alikuwa fundi Bongo Movie”,
tunasimuliana tu!
Kizazi cha sasa kitapotea na Kanumba
atasahaulika jumla. Msanii kusahaulika ni kosa la jinai. Msanii huwa
hafi, kwa hiyo haiwezekani asahaulike. Msanii hupokea wito wa kuagana na
dunia kwa sababu ni agizo la Mungu kuwa binadamu lazima arejee
mavumbini!
Msanii kwa kazi zake huendelea kuishi kila siku.
Msanii huwa hafi jumla. Hapa Tanzania kwetu akina Marijan Rajab pamoja
na ujabali wake wa muziki lakini ameondoka jumla. Tatizo siyo yeye, ni
Tanzania yetu na mwamko mdogo wa sanaa.
Mbaraka Mwishehe, mpaka
leo watu wanaimba Mtaa wa Saba. Matunda hayapo, kama nchi tuliamua
aondoke na sanaa yake. Mara moja moja ndiyo nyimbo zake zinachezwa baa,
“Shida haikosekani hata siku ya harusi”, kisha walevi wanagonga glasi na
kusema: “Mzee alikuwa fundi.”
Mzee Kassim Mapili emeondoka hivi
karibuni, hata akiwa hai thamani yake haikuonekana pamoja na Rangi Yake
ya Chungwa! Na hivi kaondoka, basi ndiyo kabisa. Unamuuaje jumla Mzee
Mapili?
TX Moshi William na uhodari wake wa kutunga pamoja na
sauti yake nzuri, wapi alipo leo. Kifo kilipomchukua na bendi yake ya
Msondo nayo ikapoteza hadhi.
Msondo ilimbakiza Kamanda Maalim
Muhidin Gurumo ambaye TX Moshi alipofikwa na mauti yeye alibaki mgonjwa.
Siku ikawadia Maalim Gurumo akaipa kisogo dunia. Wito wa Mungu
haukwepeki!
Unawezaje kuwasahau Gurumo na TX Moshi? Tanzania
tumekuwa na uthubutu wa ajabu mno. Eti hatuna mbinu bora za kuwafanya
watu hawa adhimu waendelee kuishi hata baada ya kuingia kaburini.
Juma Kilowoko ‘Sajuki’ amesahaulika mapema pamoja na kuwepo kwa simulizi ya kuumiza kuhusu maradhi yake mpaka kifo.
Adam Kuambiana hata wasanii wenzake wanamtaja kwa kuvizia, tena pale
wanapokuwa wamekwama maeneo fulani ya kikazi ndiyo wanasema: “Angekuwepo
Kuambiana hapa hili lisingekuwa tatizo!”
Hakika inauma mno
kumkumbuka Sharo Millionea na ubitozi wake. Aliitenda sanaa yake ya
comedy vizuri kwa kuigiza usharobaro. Alitokea kuwa mashuhuri. Alizikwa
kwa kishindo na kweli alizikwa jumla. Hakumbukwi tena!
Acha
nishike tama! Eti hata Albert Mangweha ‘Ngwair’, naye ameondoka kimoja.
Inakuwaje tena Mfalme wa Freestyle katika Bongo Rap?
Maskini
Ngwair mwenye kichwa kama mgodi wa Tanzanite, kutokana na ufundi mkubwa
aliokuwa nao wa kutunga na kurap, kweli imekosekana njia ya kumfanya
aendelee kuishi?
Ifike mahali tuwe na aibu, yaani Ramadhan
Masanja ‘Banza Stone’, yuleyule Mwalimu wa Walimu apotee jumla na
tusimkumbuke kabisa? Vizazi vijavyo visiwe na taarifa kuwa ardhi ya
Tanzania ilipatwa kukanyagwa na mwanafasihi huyu?
NGOJA TUSEMEZANE
Familia zina wajibu wa kuwafanya ndugu zao wasanii waliofikwa na mauti kuendelea kuishi.
Ni kwa vipi Tupac Shakur ‘Makaveli’, Christopher Wallace ‘Notorious
BIG’, Elvis Presley ‘King of Rock’, Michael Jackson ‘King of Pop’,
Marvin Gaye, Whitney Houston, Big Punisher, Ella Fitzgerald ‘Queen of
Jazzy’ na wengineo wanaendelea kuishi?
Inakuwaje Kanumba, Ngwair,
Gurumo, TX Moshi William, Sajuki, Kuambiana, Banza, Marijan Rajab,
Mbaraka Mwishehe, Suleiman Mbwembwe, Hemedi Maneti na wengine wamekufa
jumla?
Na hapa nifafanue kuwa kuishi kwa msanii haina maana ya
nyimbo zake kusikika mara mojamoja redioni, kutazamwa kwenye video,
kuwarusha watu klabu na maeneo mengine ya starehe, la hasha!
Kuishi kwa msanii ni kule kuondoka kwake lakini nyuma yake anawaacha
watu wakiendelea kuwa ‘bize’, yaani jina lake linaendelea kutengeneza
shughuli na matukio ya kila siku yenye kuingiza fedha.
Hapa sina
maana ya maonesho ya kumbukumbu ambayo huandaliwa na wajanja kumkumbuka
msanii fulani. Zipo namna kadhaa za kuwaenzi wasanii na kuwafanya
waendelee kuishi.
VITUO VYA KUMBUKUMBU
Unaweza kujiuliza
ni kwa nini mpaka leo, Flora Mtegoa ambaye ni mama yake Kanumba,
hajaweza kufungua kituo cha kumbukumbu za mwanaye.
Je, hata
wasanii wenzake wameshindwa kumsaidia mawazo Flora kutambua kiasi cha
fedha ambazo anaweza kutengeneza kupitia kituo cha kumbukumbu za
Kanumba?
Hapa Tanzania hakuna kituo cha Marijan Rajab wala Mbaraka Mwishehe, hakipo cha Gurumo wala hakijafikiriwa cha TX Moshi William.
Wasanii kwa kawaida wanakuwa na vitu vingi vya kuenziwa. Jamii
inanyimwa kuvijua kwa undani wake, hivyo kusababisha wasahaulike na
wakati huohuo, familia zinakosa fedha ambazo ingepata.
Hapa haina
maana ya kufa kufaana, hapana! Ila ni ukweli kuwa wasanii wengi
wanapoondoka huacha fedha nyingi nyuma yao lakini hazikamatiki kwa
sababu ya familia zao kukosa ubunifu.
Lazima kuwafanya watu watoke kona mbalimbali za ndani na nje ya nchi kisha kutembelea vituo vya wasanii wao.
Mathalan, siku ya kuzaliwa na ile aliyokufa msanii, katika kituo cha
kumbukumbu za msanii husika, kunakuwa na shughuli nyingi. Watu wanalipa
fedha!
Muhimu ni jinsi ya kukifanya kituo kuwa na hadhi kwa
kukitangaza na kuhakikisha mtu akifika hachushwi. Yaani huduma zisiwe za
kuboa.
Afeni Shakur ambaye ni mama yake Tupac, yeye aliona fursa
baada ya mwanaye kufariki dunia, ndiyo maana ‘ukimgugo’ utakuta utajiri
wake unasoma zaidi ya dola milioni 50, yaani Kibongo-Bongo ni zaidi ya
shilingi bilioni 100.
Mama yake Tupac pamoja na wingi wa nyimbo
ambazo mwanaye aliziacha zinazoendelea kumpa fedha nyingi, mapema kabisa
alifungua kituo cha sanaa (gallery) chenye picha na maelezo mbalimbali
kuhusu maisha ya Tupac. Ni kuchangamkia fursa.
DOCUMENTARIES
Mathalan, maisha ya Maalim Gurumo yakipata simulizi nzuri na yenye
ufasaha, ikatengenezwa documentary, nani ambaye asingependa kuitazama au
kuisikiliza?
Waza pia kuhusu TX Moshi, maisha yake, ubishoo
wake, ukuu wake kimuziki, ustaa wake, alivyokuwa mtu pendwa kwenye jamii
kisha afya yake ilipoanza kutetereka baada ya ajali na hatimaye kifo!
Nyimbo zake zinasikika zikisindikiza simulizi nzuri yenye mengi ambayo
jamii haijapata kuambiwa na mengine yaleyale yaliyofahamika lakini
yanawekwa pamoja. Je, familia haioni kama hizo ni fedha na zipo nje-nje?
Watoto wa Marijan Rajab na Mbaraka Mwishehe mnashindwa vipi kuwafanya wazazi wenu waendelee kuwa hai kimaisha na kibiashara?
Na ieleweke kuwa kadiri mipango ya kutengeneza fedha inapokuwa kwenye
mstari wake, ndivyo na jamii inapata fursa ya kutambua mengi.
Kutahamaki, kizazi na kizazi Banza Stone hatasahaulika.
Leo hii
James Dandu ‘Mtot wa Dandu’ au ‘Cool James’ hata hakumbukwi. Ni wachache
wenye kutambua kuwa alikuwa mwanamuziki mkubwa nchini na ndiye
mwanzilishi wa Tuzo za Muziki Tanzania, siku hizi zikijulikana kama Kili
Music Awards. Familia ziamke!
Tatizo ndugu wengi wa wasanii
waliofariki dunia wakiulizwa, utasikia wanalalamika kuwa serikali
haiwasaidii. Dah, kudadadeki! Yaani hata kubuni njia ya kutengeneza
fedha kupitia jina la ndugu yako unataka usaidiwe na serikali?
Wewe andaa mpango mzuri, kisha utaona mwenyewe jinsi serikali inavyoweza
kuwa karibu na wewe. Itajileta tu, si itataka kodi yake?
Voleta
Wallace ni mama wa BIG, ukimfuatilia utagundua ana utajiri unaokadiriwa
kuwa dola milioni 40, zaidi ya shilingi bilioni 80.
Moja ya vitu ambavyo vimempa fedha nyingi Voleta ni documentary kuelezea maisha ya BIG.
Ni suala la kuiandaa vizuri na kuitengenezea njia bora za masoko. Mtaji
mmoja mkubwa ni lile jina ambalo msanii husika anakuwa ameliacha.
MAANDISHI
Maisha ya msanii yakiwekwa vizuri katika kitabu kizuri, watu watapenda
kusoma. Itasaidia kumfanya msanii aendelee kuishi na familia kutengeneza
fedha.
Wasanii wengi huwa na vitu ambavyo havijulikani, na watu
wenye uwezo wa kuvisimulia kwa ufasaha ni ndugu zake. Mathalan, mama
yake Ngwair, anayo mengi ya kusimulia kuhusu mwanaye, na watu
wangeyapenda.
Yapi hasa maisha ya Ngwair tangu akiwa mtoto?
Vitabia vyake vya utotoni, alipoanza kuisumbua familia wakati akiwa na
kiu kubwa ya kufanikiwa kimuziki. Kunakuwa na simulizi kutoka kwa
marafiki zake kuhusu maisha yao ya ghetto.
Nakala za vitabu
zinapelekwa Maktaba ya Taifa ili vizazi na vizazi, wakienda kujisomea,
wanapata pia fursa ya kusoma maisha ya wasanii ambao kwa hakika
wanastahili kuitwa mashujaa wa sanaa.
Vitabu vina maana kubwa.
Pattie Mallete ni mama yake Justin Bieber, yeye alipoona mwanaye ana
jina kubwa, aliandika kitabu kuhusu maisha yake ya kumlea Bieber
kinachoitwa Nowhere but Up (The Story of Justin Bieber’s Mom).
Pattie aliweza kuuza kitabu hicho nakala nyingi na kumpatia fedha zaidi
ya dola milioni 10 ambazo ni zaidi ya shilingi bilioni 20.
Hata
mama yake Diamond Platnumz, anaweza kuandika kitabu cha jinsi alivyomlea
kwa tabu mwanaye na kutengeneza fedha nyingi kipindi hiki ambacho
mwanaye anang’ara kila kona. Ni fursa!
Mimi mwenyewe ningependa
sana kusoma kitabu kinachoeleza kwa ufasaha maisha ya Shem Kalenga
lakini hakipo. Nahitaji mno kumsoma Dk. Remmy Ongala, sina pa kupata
undani wa maisha yake. Fursa zinachezewa.
TUKUBALIANE
Kama
wewe ni mwanafamilia wa msanii maarufu aliyefariki dunia na mnakaa
pembeni kulalamika kuwa maisha magumu, basi tatizo lipo kwenu wenyewe.
Wazazi na watoto wa wasanii ndiyo wenye haki zaidi. Ni muda wa
kufikiria mara mbili, kipi ambacho watu wangependa kukipata kuhusiana na
msanii wao kisha wapewe. Watakuwa wanaihudumia jamii na wakati huohuo
wanatengeneza fedha.
Wanaweza pia kutengeneza mfuko wa
kuhudumia jamii kwa jina la msanii husika. Jinsi kazi zinavyofanyika
ndivyo jina la msanii linaendelea kuwa hai na wakati huohuo fedha
zinaingia.
Ni rahisi mtu kuchangia fedha kwenye mfuko wa elimu, afya na kadhalika, wenye jina la Sajuki kwa sababu anajulikana.
Muhimu kuzingatia ni kuwa leo hii tunao akina Lady Jaydee, Sugu, Prof
Jay, Afande Sele, Juma Nature na wengine wengi, nao wataondoka, ila
watakuwa wameipa kisogo dunia kama wataendelea kuishi, ikiwa wataondoka
jumla kweli watakuwa wamekufa na hawatakumbukwa!
Ndimi Luqman Maloto
-
Blogger Comment
-
Facebook Comment
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)
0 comments :
Post a Comment