ads 728x90 B

Celine Dion Analia kumpoteza mume na shujaa wake





Luqman Maloto
HAYAMITHILIKI maumivu ya kuondokewa na mtu uliyempenda. Kuna watu wamewahi kuanguka katika maisha yao kwa sababu ya kushindwa kuzoea machungu na upungufu wa kufiwa na watu wao muhimu.
Celine Dion, mwanamuziki mkubwa duniani na mwanamke imara nyakati zote kutokana na jinsi alivyobadili upepo wa maisha yake, kutoka ufukara mpaka utajiri mkubwa, yupo kwenye majonzi makubwa.
Celine amefiwa mume wake, Rene Angelil, aliyefikwa na mauti Januari 14, mwaka huu. Ni machungu kwa sababu siyo tu kwamba amempoteza mume, bali pia baba wa wanaye na mshirika mkuu wa kazi zake.
Yatazame mafanikio ya Celine kwa upana kabisa, kisha tambua kuwa Rene amekuwa na mchango mkubwa mno.
Rene amekuwa meneja wa Celina na msimamizi mkuu wa kazi za mwanamuziki huyo, hususan kile kipindi chake cha dhahabu, alipouza mamilioni ya nakala ulimwenguni kote.
RENE NI NANI?
Alizaliwa Januari 16, 1942 nchini Canada. Alianza kama mwanamuziki kabla ya kugeuka meneja wa wanamuziki.
Rene na Celine walianza kufanya kazi pamoja lakini mapenzi yaliwateka, na mwaka 1994 walifunga ndoa.
Mji aliozaliwa ni Montreal, Quebec, Canada. Asili yake ni Mashariki ya Kati, kwani kiasili baba yake ni mtu wa Syria na mama yake alitokea Lebanon. Walihamia Canada na kuchukua uraia wa taifa hilo la Amerika Kaskazini.
Miaka ya 1960 Rene alifanya muziki wa Pop na aliwahi kuunda kundi lililoitwa Les Baronets ambalo lilijihusisha na muziki wa pop rock.
Baada ya hapo, kuanzia mwaka 1981, Rene alianza kujishuhughulisha na usimamizi wa kazi za wanamuziki mbalimbali (umeneja).
Mwishoni mwa mwaka 1980, Rene aligundua kipaji cha Celine na uwezo mkubwa alionao baada ya kusikiliza demo yake.
Kipindi hicho, Celine alikuwa akitafuta watu ambao angeweza kuingia nao mkataba wa muziki, ndipo alipopeleka demo kwa Rene.
Sauti ya Celine ilimtoa machozi Rene na ndipo aliamua kuwekeza nguvu zake zote kuhakikisha mwanamuziki huyo anakuwa staa wa dunia. Na hakika amefanikiwa.
Na ndiyo maana leo hii Celine anapoumia kuondokewa na mume wake, maumivu yanaongezeka zaidi kwa sababu Rene ndiye shujaa wa mafanikio yake.
Mwaka 1981, Rene aliweka rehani nyumba yake na kupata fedha ambazo alizitumia kuwekeza kwenye kurekodi albamu ya kwanza inayoitwa kwa Lugha ya Kifaransa, La voix du bon Dieu, ikiwa na maana Sauti ya Mungu Mzuri.
Baada ya kutoa albamu hiyo, Celine alivuma vilivyo Canada na kufanya biashara kubwa. Vilevile muziki mzuri wa Celine kutoka kwenye albamu hiyo, ulivuma mpaka Marekani na maeneo mengine duniani.
Mwaka 1982, alishinda tuzo Tokyo, Japan, mwaka 1983, alikuwa mwanamuziki wa kwanza mwenye asili ya Canada kufikisha mauzo ya kiwango cha dhahabu (nakala zaidi ya 500,000), kupitia wimbo wake D'amour ou d'amitiƩ ukiwa na maana ya Kwa Mapenzi au Kwa Urafiki (Of Love or of Friendship).
Kupitia mafanikio ya Celine, Rene aliweza kushinda tuzo mbalimbali kama meneja bora wa muziki.
Hivyo, kwa sasa Celina anapotajwa kuwa na utajiri unaofikia dola milioni 630, ambazo ni zaidi ya shilingi trilioni 1.37, nguvu kubwa ya kufikia hapo, imetoka kwa Rene.
Ni Rene aliyemtoa Celine Canada mpaka Marekani na kumbadilisha kutoka kuimba nyimbo za Kifaransa mpaka za Kiingereza, hivyo kumuwezesha kufanya biashara kubwa zaidi.
Rene ameacha utajiri unaokaribia kuzidi dola milioni 400 ambazo kwa sarafu ya Tanzania ni shilingi bilioni 875.
Hii ina maana kuwa kwa kuunganisha utajiri wa Rene na Celine, unaipata familia inayomiliki dola bilioni 1.03 ambazo ni sawa na shilingi trilioni 2.25.
Celine na Rene wana watoto watatu lakini Rene anao watoto wengine watatu ambao aliwapata kwa wake zake wengine wawili aliokuwa nao kwa vipindi tofauti kabla hajafunga ndoa na Celine,
CELINE ALIVYOPAMBANA KWA AJILI YA AFYA YA RENE
Rekodi za afya ya Rene zinaonesha kuwa alipata shambulio la moyo mwaka 1992, kipindi hicho alikuwa na umri wa miaka 51.
Mwaka 1998 Rene aligundulika kuwa na kansa ya koo kisha ikaripotiwa amepona kabisa. Kipindi hicho, Celine alikuwa bega kwa bega na mumewe kuhakikisha anapata matibabu ya kimsingi, na kwa hakika walifanikiwa.
Mwaka 2009, aligundulika kuwa na matatizo ya moyo lakini tatizo la kansa ya koo lilijidhihirisha tena na mwaka 2013 alifanyiwa upasuaji.
Mwaka 2014, Rene alijiuzulu umeneja wa Celine ili ashughulikie zaidi afya yake. Hata hivyo, alibaki kuwa sehemu ya washauri wa kazi za kile siku za Celine.
Bwana alitoa, Bwana ametwaa, jina lake lihimidiwe.

Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment