ads 728x90 B

SHULE ZETU KAMA MASHINDANO YA BIG BROTHER!




NA LUQMAN MALOTO
TUNALALAMIKA matokeo, eti wanafunzi wengi wameanguka! Hatujui tatizo. Tuache kudanganyana!
Shida za walimu zinajulikana? Mwalimu na mwanafunzi wanacheza kamari ya kutabiri matokeo ya soka. Asubuhi wakikutana, mwanafunzi anamuuliza mwalimu wake: “Ticha vipi, mkeka wako jana ulisoma?”
Tunataka elimu ipande kweli? Shida za walimu zimetatuliwa? Walimu wamejaa dhiki mpaka Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda anawaombea wapande daladala bure. Eti tunataka ufaulu ufande!
Mwalimu na mwanafunzi wanakutana kwenye kibanda cha kuangalia mpira, tena mwanafunzi anamlipia kiingilio mwalimu. Kesho tunataka mwanafunzi awe na nidhamu kisha afaulu. Hii tabia ya kuitania elimu yetu tutaacha lini?
Mwalimu na mwanafunzi wana uhusiano wa kimapenzi. Mwalimu na mwanafunzi wana vita ya kugombea mpenzi. Jamani jamani jamani!
Mwalimu na mwanafunzi wamegawanywa na Team Diamond na Team Kiba. Wakikutana wanaanza kubishana, mwanafunzi: “Diamond Platnumz wa kimataifa, yule ndiye Dangote.”
Mwalimu anajibu: “Anaitwa King Kiba, jamaa fundi sana. Mwite Ali K For Real.”
Katikati ya masomo, inaingia michapo ya Wema Sepetu na Zari The Boss Lady. Mwanafunzi anamuuliza mwalimu wake: “Eti mwalimu kati ya Zari na Wema nani mzuri?”
Mwalimu kabla ya kujibu anamuuliza mwanafunzi wake: “Anza kujibu kwanza wewe, nani mkali kati yao?”
Mwanafunzi: “Zari noma, ana watoto wanne lakini kama vile hajazaa. Mweupe, ana mguu umejaa, umenona kama chupa ya Dompo. Yote tisa, 10 ana pesa, mwite Zari The Boss Lady. Yule Wema anapumua kwa nguvu ya wanaume tu!”
Mwalimu naye anajibu: “Acha kujishaua, Madam Sepetu ndiye homa ya nchi. Anaitwa Beautiful Onyinye. Kale kasauti kake huwa kanamliza Diamond, halafu ana mwanya fulani hivi mwembamba, sura yake haizeeki.”
Mtihani wa mwisho kitaifa ukiwadia, hakuna swali la kuhusu Diamond, Ali Kiba, Wema wala Zari, unadhani nani atafaulu? Siku tukiweka utani pembeni elimu itapanda na viwango vya ufaulu tutaviona.
Tatizo siyo wanafunzi kuwa hawana akili, ni kizazi cha sasa na aina ya walimu wanaoshika chaki kuingia darasani, hali zao za kimaisha, nidhamu yao ya ufundishaji, wito wao kwenye kazi na maadili ya ualimu kwa jumla.
Mwalimu kamtaka mwanafunzi, wakishakubaliana kimapenzi basi anahakikisha kila mtihani anapata A. Mwanafunzi anabweteka, anasahau kuwa mtihani wa mwisho mwalimu wake hatakuwepo kwenye chumba cha usahihishaji wala cha utungaji wa mitihani. Mwenye A nyingi shuleni, anapata Sifuri kitaifa.
Mwalimu anawakuta wanafunzi wawili wanajisomea, wakiwa mvulana na msichana, anawaambia: “Inaonekana mnapendana sana, wewe Mage mwangalie huyo Mudi atakuja kukupa mimba.” Wanafunzi wanacheka, kisha Mudi anasema: “Mwalimu bwana kwa madongo!”
Mwalimu akiwakuta wanafunzi wawili wa kike wanajisomea au wanaongea peke yao, anawaambia: “Nina wasiwasi nyie mnasagana, huu ukaribu wenu siyo wa kawaida.”
Mwanafunzi mmoja anauliza: “Mwalimu kusagana ndiyo nini.”
Mwalimu anasema: “Mnajifanya hamjui eeeh!”
Mwanafunzi: “Kweli tena mwalimu, hatujui.”
Mwalimu: “Kama kweli hamjui basi nyie ni washamba. Fuatilieni mtagundua.”
Halafu wakubwa wanapokutana, baada ya kuanza kutafuta kiini, eti wanajikita kwenye vitu vidogo-vidogo. Mara GPA, mara Division! Ndiyo maana kwenye suala la elimu yetu, nimekataa kabisa utani na Profesa Joyce Ndalichako.
Walimu wakiwa ofisini, wanateta, anaanza Mwalimu Kimpomo: “Mimi Mwaija, Sikudhani, Sikitu, Chausiku na Kaundime wote tayari.”
Mwalimu Mong’o anadakia: “Kuanzia form IV na III, nimewazunguka kama sina akili nzuri. Maslahi yenyewe ya ualimu ubabaishaji mtupu, tutafanyaje zaidi ya kujilipa mapenzi ya wanafunzi wazuri?”
Mwalimu Chongo anaunga mkono: “Kweli bwana, inabidi tufidie machungu ya ukapa wa ualimu kwa watoto wazuri. Ila washkaji tuwe tunapeana signal, isije tukagonganishwa magari bure!”
Mwalimu Mkweche anashusha nyepesi: “Hivi mnajua kuwa sasa hivi mwalimu Pili na mwalimu Maria wana ‘bifu’? Kimenuka nawaambia!”
Mwalimu Mkangafu anauliza: “Bifu la nini tena, wanagombea bwana?”
Mwalimu Mbinuko anachangia: “Wewe upo wapi? Shule nzima watu wanajua. Wale wanamgombea James, yule dogo bishoo wa Form IV anayeimba Bongo Fleva, dogo katembea nao wote, wamejuana, sasa ni vita, kila mmoja anataka yeye ndiye awe mmiliki wa penzi la James.”
Usiku mwalimu Jessica anazungumza kwa simu na mwalimu Sudi, anamwambia: “Ndiyo nini ulichonifanyia kunichanganya na Salome? Kile kisichana chako cha Fom III? Kwa taarifa yako nimeshajua kila kitu.”
Asubuhi mwalimu Jessica akiingia darasani anaamrisha: “Salome toka nje, na kuanzia leo nisikuone darasani kwenye vipindi vyangu.”
Jioni Salome anamwandikia SMS mwalimu Jessica: “Najua unanichukia kwa sababu nimekuzidi ujanja kwa mwalimu Sudi. Tena nikwambie, Sudi hapa kwangu ndiyo kafika, wewe utaishia kulia, humpati tena.”
Mwalimu Jessica akiwa anatafakari, mara anapokea SMS nyingine ya Salome: “Utavimba mpaka upasuke. Sudi hawezi kuwa na wewe tena, mwanamke huna vionjo wala manjonjo!”
Kisha mwalimu Jessica naye anajibu: “Sibishani na watoto wasiojua hata kuoga. Sudi kwako anafanya utafiti tu, mimi ndiye malkia wake.”
Mwalimu anakatiza mitaani, anakutana na kundi la watoto wakiwa wamevaa kinyumbaninyumbani, Jose anampa ‘shua’ mwalimu wake: “Leo utakoma kuringa, si huwa unajifanya mjanja kuniletea unoko shuleni!” Mwalimu anapigwa halafu anaambiwa: “Usirudie tena kucheza na wahuni wa kitaa!”
Mwalimu mkuu anafanya mapenzi ofisini kwake, wanafunzi wakiwa nje wanachungulia dirishani na kuona kila kitu.     
Wanafunzi wakikaa wanasimuliana. Vicheko na simulizi zinakuwa nyingi, kuhusu tukio na vitendo hatua kwa hatua. Jamani elimu yetu inapokwenda!
Mwalimu Consolata anamwita Abbas ofisini kwake amwadhibu, Abbas anamchimba mkwara mwalimu wake: “Thubutu, ukinikomalia kuniadhibu nitasema siri zako zote.”
Mara Abbas anamwonesha mwalimu Consolata picha yake ya aibu. Mwalimu badala ya kuwa mkali anambembeleza Abbas kwa zawadi na ahadi. Matokeo ya baadaye ni Abbas kuwa mpenzi wa mwalimu Consolata. Ni mengi ya aibu kwenye shule zetu.
Mwalimu na mwanafunzi usiku ‘wanachati’, maswali wanayoulizana: “Umelalaje? Eehhee, umevaa nini? Hebu jipige selfie hapo kitandani unitumie picha kwa WhatsApp.” Eti mwanafunzi na mwalimu, hapana jamani, hatukutakiwa kabisa kufika huku!
Wakati mwingine mwalimu anawafanya wanafunzi wake makuwadi wa kumuunganishia wanafunzi wa kike. Haya yanatokea jamani!
Mwalimu wa kike anakuwa na mabwana zake hata watano. Anamtuma mwanafunzi amfuatie pesa kwa wanaume wake, leo kaenda kwa Paul, kesho Seba, keshokutwa Mathew, mtondogoo Sam, halafu jana alimtuma kwa Faridi.
Baadaye mwalimu anakuwa anamuogopa mwanafunzi kuliko hata mwalimu mkuu. Na mwanafunzi naye akikaa na wenzake anawaambia: “Mwalimu hawezi kufunua mdomo mbele yangu, najua siri zake kibao na yeye anajua, ndiyo maana ananiogopa.”
Baba kaenda shule kufuatilia maendeleo ya mwanaye, baadaye mwalimu anamwambia mwanafunzi: “Baba yako handsome kweli.”
Mtoto naye anafika nyumbani, anamwambia baba yake: “Daddy eeh, ticha Nuru amekufagilia sana leo, anasema wewe ni bonge la handsome.”
Baba na mwana wanaishi kisasa, Uzungu mwingi! Ndivyo walivyoamua iwe mtindo wao wa maisha. Baada ya muda mtoto anakuwa anatumwa na baba yake kumpelekea zawadi na fedha mwalimu Nuru. Tayari baba na mwalimu wameshakuwa wapenzi.
Mama naye kwenda mara moja tu shuleni, tayari kawa mpenzi wa mwalimu. Uhusiano unakwenda mpaka mtoto anajua. Tena mara kwa mara mama anakwenda shuleni.
Mengine yanafanyika ofisni. Matokeo yake mtoto ananyimwa raha, wenzake wanamtania: “Mama yako ni demu wa ticha.”
Wanafunzi wanasasambua darasani, Mduara unachezeka, mwalimua anamwambia Jamila: “Nakukubali sana kwa kusasambua, nilikuona darasani, itabidi tufanye kweli.”
Wazazi wanawaruhusu watoto wao kwenda kwenye Vigodoro usiku, asubuhi darasani ni mashindano, nani mkali wa kuyakata mauno. Tobaaaa!
Hatuwezi kukimbilia matokeo bila maandalizi. Na jambo la kwanza na muhimu ni nidhamu, bila hilo ni utani. Na kama tunataka kuendelea kutaniana sawa, ila ikiwa tunahitaji mabadiliko, basi yaonekane.
Walimu waache kuzifanya shule ni eneo la ‘nikamate nichinje’ kama mashindano ya Big Brother Africa. Heshima ya kweli inahitajika kati ya walimu na wanafunzi ili dhana ya ufundishaji ipate hadhi yake.
Wazazi wajiheshimu. Watambue kuwa kuhusika kimapenzi na walimu kwa namna moja au nyingine kunaifanya saikolojia ya mtoto iwe tenge.
Tukitaka elimu ipae, lazima kwanza tupigie kelele kwa zingatio “Nidhamu… Nidhamu… Nidhamu.”  
Ndimi Luqman Maloto




Kwanza mfumo wenyewe ubabaishaji mtupu! Anza darasa la saba, njoo kidato cha nne, ni kwa nini mwanafunzi aliyekuwa anafanya vizuri darasani siku zote ndoto zake za kielimu zinaweza kukatika kwa mchujo tu wa mtihani wa mwisho? Nasisitiza mfumo ubadilike.
Sipingani na mitihani ya mwisho, lakini lazima kuwepo na utaratibu wa alama za awali. Mathalani, inakuwepo mitihani ya kidato cha kwanza mpaka cha nne yenye hadhi ya kitaifa kila mwaka, lengo likiwa kupima maendeleo ya mwanafunzi hatua kwa hatua.
Mathalan, katika alama 100, 70 zinakuwa zimekusanywa kuanzia kidato cha kwanza mpaka cha nne na 30 ndiyo ambayo inapatikana katika mtihani wa mwisho. Yule ambaye alikuwa na kawaida ya kufanya vizuri kila mwaka, anaweza kuokoka hata kama mwishoni aliteleza.
Inawezekana katika katika mitihani ya nyuma alikuwa na pointi 60, anapopata pointi 15 katika mtihani wa mwisho, anakuwa na jumla ya alama 75. Hata viwango vya ufaulu vipimwe kwa pointi ambazo mwanafunzi anakuwa amekusanya kuanzia mwaka wa kwanza mpaka wa mwisho.
Huko nyuma mwanafunzi wa shule ya msingi alipimwa kwa mtihani wa siku moja tu. Yaani miaka saba anatoka kwa kwanza darasani mpaka Juni kwenye mitihani ya Moko na nusu muhula, anaongoza lakini Oktoba anaingia kwenye mitihani ya mwisho, siku inamkataa. Anafeli. Ndoto zake kielimu zinapotea, anakwenda kukata mkaa!
Kuna watu wengi ambao walimaanishwa kuwa wakombozi wa nchi hii, waliokuwa tishio darasani hawakufika hata sekondari kwa sababu ya matokeo ya mwisho darasa la saba. Kama aliingia kwenye chumba cha mtihani na kupaniki, basi ni tatizo.
Yapo pia makosa ya usahihishaji. Hili tatizo la uwezo wa wasahihishaji lilishazungumzwa sana. Wengi walisoma kwa kukariri, alishakariri jawabu kuwa Mnara wa Bismini upo Mtaa wa Azikiwe, akikutana na jibu la mwanafunzi mwelewa zaidi, anayefafanua kuwa Bismini ipo kwenye makutano ya Samora na Azikiwe, anamwandikia kosa.
Ni rahisi mwananchi wa kawaida kuwaza kuwa pengine kwa sababu watoto wa wakubwa wamekuwa hawapati wakati mgumu kwenye maisha yao ya kutafuta elimu ndiyo maana matatizo kama hayo yamekuwa hayazingatiwi.
Kweli watu hawajiulizi tiba, yaani mitihani ya mwisho haifanywi kama chujio la mwisho, inakuwa kama sadakalawe, anayepata apate, anayekosa akose. Ikawa sababu ya wengi hawasomi, wanasibiri mitihani ya mwisho waibe na kukariri majibu ya kuingia nayo kwenye chumba cha mtihani.
Matokeo yake tumeshuhudia baadhi  ya wanafunzi wanaofaulu lakini hawajui kusoma wala kuandika. Katika nyakati ambazo hakujawa na jawabu la kimsingi la wanaofaulu lakini hata majina yao hawawezi kuandika vizuri, serikali ikashusha viwango vya ufaulu.
Ni janga kubwa kuongezeka kwa idadi ya watu wasiojua kusoma na kuandika katika zama hizi zinazoitwa za sayansi na teknolojia. Ni lazima kuutazama vizuri mfumo mzima wa elimu inayotolewa nchini, ubomolewe na kusukwa upya. Ni ngumu kwa kuwaza na kujawa na nyoyo zenye kusitasita, ila ni rahisi kama dhamira ya dhati ipo.
Ukosefu wa hali bora za kimaisha za walimu, maslahi duni, posho za kukijikimu na huduma nyingine stahiki kama vile afya ya uhakika, ikiwemo suala zima la  mishahara, ni mojawapo ya mchango mkubwa wa elimu ya msingi na ya sekondari kuporomoka. Tunapokataa ukweli tunaichimbia kaburini elimu yetu.
Kiwango duni cha kimaisha walichonacho walimu, kinawafanya wafundishe mwanafunzi wakiwa hawana molari ya kazi na kufanya  bora liende na matokeo yake ni kuwa na kizazi mbumbumbu kutokana na kufundisha bora elimu kuliko elimu bora.
Lazima serikali iwekeze kwa walimu kwanza kama tiba kuu ya kupanda kwa elimu, vinginevyo wanafunzi wataendelea kufeli, kisha maskini watazidi kuangamia, maana wao ndiyo hawana uwezo wa kupeleka watoto wao kwenye shule za kulipia.


Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment