Na Luqman
Maloto
MUNGU pekee
anajua kilichokuwepo kwenye kichwa cha Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, kupendekeza jina la Dk. Vincent Mashingi
kisha kuthibitishwa kuwa katibu mkuu mpya wa chama hicho.
Wapo watu
kwa upeo wao waliamini uteuzi wa katibu mkuu Chadema ni jambo rahisi. Hali ya
kisiasa kwa sasa na sura ya kuendelea kukibakisha chama kuwa taasisi imara,
ilikuwa mtihani kwa Mbowe kuteua.
Ndani ya
Chadema kuna viongozi maarufu vijana ambao mtaani wanaitwa masupastaa wa chama.
Umpe Salum Mwalimu (Naibu Katibu Mkuu Zanzibar), John Mnyika (Naibu Katibu Mkuu
Tanzania Bara) anune?
Wapo akina
Tundu Lissu, Halima Mdee, Ezekia Wenje, Peter Msigwa na wengine. Wote hao ni
maarufu, na kila mmoja kwa nafasi yake anajiona ni roho ya chama na anatosha
viwango vya kuwa katibu mkuu. Ampe nani, amnyime nani?
Ifahamike
kuwa katibu mkuu ndiye mtendaji mkuu wa shughuli za chama. Anatakiwa mtu mwenye
weledi, afya, busara na mvumilivu. Nani kati yao? Naweza kuhisi maumivu ya
kichwa aliyokuwa nayo Mbowe!
Hapohapo
lazima kutambua kuwa anayerithiwa ni Dk. Willibroad Slaa. Mwanasiasa mkongwe
nchini, aliyejitengenezea haiba ya kupendwa na watu wengi katika kada
mbalimbali.
Misimamo ya
Slaa na kazi kubwa aliyopata kuifanya akiwa mbunge na kiongozi wa Chadema, ni
thamani ambayo si rahisi kuilinganisha na mtu. Hivyo ilikuwa lazima kuwa na
uhakika hasa wa anayeziba nafasi yake.
Jinsi Dk.
Slaa alivyoondoka, alichafua hali ya hewa kuwa Chadema iliingia ubia na Waziri
Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, na kumfanya kuwa mgombea urais wa chama hicho kwa
ushirikiano na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Slaa
alipakaza kuwa Lowassa aliingia Chadema kwa matumizi makubwa ya fedha. Maneno
hayo kwa tafsiri ya karibu ni kwamba chama kilinunuliwa. Na CCM walitumia
maneno hayo kwenye kampeni zao.
Kwa mantiki
hiyo, siyo uongo kuwa chama kimesemwa vibaya, na kimekuwa kikishambuliwa kwa
kupoteza ajenda ya ufisadi katika harakati zake za kuiondondoa CCM madarakani.
Nani wa
kufaa kukipaka chama sabuni na kukiondolea uvundo wa mashambulizi yote ya
nyuma? Mbowe alihitaji mtu mithili ya pafyumu nzuri, ambaye atakuwa manukato
yenye kukifanya chama kinukie.
Kuelekea
Mwanza kwenye uteuzi, yapo majina ambayo yalikuwa yakifikiriwa kuwa pengine
yangepewa nafasi. Hata Profesa Mwesiga Baregu alitajwa, lakini haikuwa hivyo.
Hatimaye Dk. Mashingi akawa moshi mweupe kwenye Mkutano wa Baraza Kuu.
Zikapigwa kura za wazi!
Kwa hili
suala la kura za wazi ni lazima tuliseme na liishe. Linaua demokrasia ndani ya
vyama. Wakuu wameibuka na utaratibu wao wa kutotaka uamuzi wao usipingwe, kwa
hiyo wanataka uchaguzi wa machoni. Kwamba “tukuone ukisema hapana.”
Mwanachama
unawezaje kusema hapana mbele ya mwenyekiti na viongozi wote wakuu? Hii ndiyo
sababu kura zote za wazi huwa na matokeo ya asilimia 100. Nani hajipendi? Hii
ikome ili kukomaza demokrasia kwenye vyama!
Tukirejea
kwenye muktadha wetu, ni kuwa uteuzi umeshafanyika na Dk. Mashingi ndiye katibu
mkuu lakini ni vizuri kwa wakati huu kumkumbusha madeni yake.
Madeni hayo
yanahusu nafasi aliyoteuliwa ili kukidhi viwango vya cheo chake, vilevile kutii
kiu na matarajio ya wanachama wa Chadema.
DENI LA
UMAARUFU
Dk. Mashingi
ni mwanasiasa mpya. Siasa za nchi ndiyo kwanza zimepokea jina lake. Hajawahi
kutajwa popote kabla, kwa hiyo watu ndiyo kwanza wanamtazama na kumchimba
wapate kumfahamu kwa undani.
Siasa siku zote
hutegemea mtaji wa umaarufu, na pointi hii siyo rafiki wa Dk. Mashingi kwa
sababu hajulikani.
Ni ukweli
kuwa chama chake ni maarufu, kwa hiyo atajulikana tu lakini umaarufu ambao
unaohitajika ni ule wa ushawishi (influence). Awe na viwango vya kutengeneza
maneno yenye nguvu kisiasa, kijamii na kihabari. Hili ni deni!
Ni deni
kubwa kwa sababu anazungukwa na timu ya watu maarufu na yeye anatakiwa kuchanua
katikati yao.
Zaidi,
anatakiwa kufanya kazi ili kuupiku umarufu wa akina Lissu, Mnyika, Mwalimu na
wengineo kwa sababu yeye ndiye anakuwa bosi na mtendaji mkuu wa chama.
Hatakiwi
kabisa kutenda au kung’ara chini ya kiwango. Akifanya hivyo litakuwa kosa kubwa
mno.
DENI LA
VIATU VYA DK. SLAA
Nimeshaeleza
kuwa Dk. Mashingi amepata nafasi hiyo baada ya Slaa kujiuzulu nafasi hiyo kisha
kuachana na siasa, kutokana na kutokubaliana na uamuzi wa chama hicho kumpokea Lowassa
na kumfanya kuwa mgombea urais.
Slaa ni
mwanasiasa mwenye jina kubwa. Amefanya mengi kwenye siasa za upinzani. Chadema
hakikuwahi kukua na kupata ukubwa wa kiwango cha sasa kabla ya Slaa kuwa katibu
mkuu.
Kabla ya
Lowassa kuondoka CCM na kujiunga Chadema, Slaa ndiye alikuwa nembo ya upinzani
na kiongozi mwenye ushawishi mkubwa kuliko mwingine yeyote. Takwimu mbalimbali
za kitaalamu zilimtaja hivyo.
Yapo maeneo
Chadema imejulikana kwa sababu ya Slaa. Hili ni dhambi kulipinga. Kwa mantiki
hiyo, Mashingi anatakiwa kucheza karata zake vema ili asiache pengo katika
kiatu alichovua Slaa. Udhaifu wowote atakaouonesha, utaibua kelele nyingi za
wanachama kwamba ameondoka mtu imara, amefuata dhaifu.
DENI LA
SIASA ZA SASA
Mashingi
ameingia kuwa mtendaji mkuu wa chama ambacho kina kiu kubwa ya kuchukua usukani
wa nchi ifikapo mwaka 2020.
Ni kipindi
ambacho siasa za upinzani zimepewa mazingira magumu ya kung’ara kutokana na
mfumo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli.
Tangu Dk.
Magufuli alipoapishwa Novemba 5, mwaka jana, amekuwa akipita kulekule ambako
wapinzani siku zote walipigia kelele, hivyo kuwafanya wapinzani kukosa ajenda yenye
nguvu ya kusimamia.
Mtindo wa
kutumbua majipu, udhibiti wa matumizi ya serikali na mambo mengine, vimekuwa
vitu vinavyomfanya Dk. Magufuli ang’are, na kutazamwa zaidi kuliko harakati za
upinzani.
Mfano mdogo
ni kuwa baada ya jina la Mashingi kutangazwa usiku wa kuamkia Jumapili (Machi
13), tangu asubuhi yake, vijana wa Chadema wanaofahamika walikuwa ‘bize’ sana
kusambaza wasifu wake ili kuonesha kuwa Mbowe amefanya kazi nzuri.
Sifa kubwa
ambayo Mashingi alipewa ni kuwa ndiye katibu mkuu msomi kuliko makatibu wakuu
wote duniani! Sijui kwa takwimu za wapi!
Walieleza
kuwa Mashingi ana shahada ya Udaktari (MD), aliyosomea Chuo Kikuu cha Makerere,
Uganda kati ya mwaka 1995 mpaka 2001.
Wakasema
anayo shahada ya pili ya Udaktari Bingwa (MMED Anesthesiology) aliyosomea Chuo
Kikuu cha Muhimbili, Dar es Salaam kati ya mwaka 2003 mpaka 2005.
Walimchambua kuwa mwaka 2004 alitunukiwa cheti
(astashahada) katika Utafiti, Chuo Kikuu cha Muhimbili.
Wasifu wa
Mashingi uliendelea kusambazwa kuwa kati ya mwaka 2008 na 2010, alisoma na
kutukiwa shashada ya uzamili ya Uhusiano wa Umma (Public Relations) katika Chuo
cha Evin School of Management, Dar es Salaam.
Sifa
nyingine ya kielimu ni kuwa Mashingi kati ya mwaka 2007 na 2010, alisoma
shahada ya uzamili ya Usimamizi wa Biashara katika Taasisi ya Teknolojia ya Blekinge,
Sweden.
Mwaka 2010,
Mashingi alisoma Chuo Kikuu cha California, katika Shule ya Anderson, hapo
alisomea stashahada ya Usimamizi wa Maendeleo.
Mwaka 2008
alisoma Chuo Kikuu cha Maryland, Marekani, Shule ya Dawa, akatunukiwa cheti cha
Mfumo wa Wadudu Maradhi kwa Binadamu (Human Virology).
Kwamba kati
ya mwaka 2010 mpaka 2016, alisoma na kutunukiwa shahada ya uzamivu (PhD) ya
Uongozi katika Chuo Kikuu Huria Tanzania.
Uzoefu wa
kazi ni kwamba amewahi kuwa daktari Hospitali ya Muhimbili, mtafiti wa
kujitegemea, daktari bingwa Hospitali ya Regency, msimamizi wa miradi Shirika
la Kimataifa la Afya (IMA World Health), vilevile mshauri wa tiba za kifua
kikuu na Ukimwi wa Shirika la IMA.
Pamoja na
sifa zote hizo, habari za katibu mkuu huyo kwenye mitandao ya kijamii,
zilimezwa mara tu taarifa ya Ikulu kuhusu uteuzi wa wakuu wa mikoa ilipotoka mchana
wake.
Baada ya
wakuu wa mikoa kutangazwa, kila upande habari zinazotamba ni majina ya wakuu wa
mikoa, huyu kamzungumzia Paul Makonda kuwa mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam,
mwingine anajadili wanajeshi kupewa vyeo na kadhalika.
Hapa kwa
hakika, Mashingi anayo kazi ya kufanya kipindi hiki ambacho upinzani unabanwa
mbavu na serikali. Anatakiwa kuwa na ajenda zenye nguvu ili chama chake kipewe
nafasi ya kutamba kwenye mzunguko wa habari na mitandao ya kijamii.
www.luqmanmaloto.com
0 comments :
Post a Comment