ads 728x90 B

Nguvu ya mwanamke hugeuza ngumu kuwa rahisi




Na Luqman Maloto
POKEA ukweli huu kuwa yote yanawezekana, silaha kubwa ni juhudi zako bila kusahau sala kwa Mungu wako ili akufanikishie malengo yako. Hakikisha unazo ndoto kisha uzifanye ziwe hai kwa kujituma kuzitimiza.
Ukiwa na ndoto hakikisha unakuwa na maono. Ndoto na maono (Dream and Vision) kwa pamoja huzaa msisimko wa kuyaona matarajio, hivyo kuchochea juhudi ya kufikia malengo.
Unaota kuwa nani? Jibu la swali lako ni juhudi zako. Utayari wa Mungu ni mkubwa siku zote katika kufanikisha yale mahitaji mema ya waja wake. Wewe ni mja mwema, unachokitaka ni kitu chema, basi usikate tamaa! Mbele za Mungu yote yatatimia!
Kingine ambacho unatakiwa kuzingatia ni njia za kupita. Barabara ya mtu anayeota kuwa mfanyabiashara mkubwa haifanani na ile ya mwanasiasa anayeutamani uongozi mkubwa kwa nchi.
Kama malengo yako ni kuwa mwandishi mkubwa vema sasa utaratibu wako wa kuenenda ufanane na uandishi. Haiwezekani mtu anayetaka kuwa rubani au daktari bingwa, akawa anatumia muda mwingi wa ujana wake katika harakati za kisiasa, huko ni kupoteza muda.
Somo hilohilo liendane pia wanamuziki, waigizaji, wanamichezo na fani nyingine zote. Ukitaka kufanikiwa katika eneo lako ambalo unaliota, vema kuzitambua njia zake na uzipite. Usichanganye utaratibu!
Felix Mkosamali alikuwa kijana maskini, mdogo kabisa akiwa na umri wa miaka 24 tu. Akiwa bado anasoma shahada ya kwanza ya sheria Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (Saut), Mwanza. Aliona hiyo haimzuii kutimiza ndoto zake.
Mwaka 2010, Mkosamali aligombea ubunge Jimbo la Muhambwe, Wilaya ya Kibondo, Kigoma (NCCR-Mageuzi) na kushinda. Siyo yeye wa kwanza, wapo wengi tu na umaskini wao wameweza kushika nafasi za juu za uongozi. Hata Barack Obama aliwezaje kuwa Rais wa Marekani? Sema hata kwako inawezekana!
Wewe ni mwanamke na unataka uongozi? Mtazame Wendy Russell Davis kama kioo chako. Tambua kuwa mtu kuibuka mpaka kuwa mashuhuri katika siasa za Marekani siyo kitu kidogo. Wendy ameweza!
Sifa ya Wendy kuwa kioo cha mwanamke anayesaka uongozi wa kisiasa, haitokani na kwamba amefanikiwa katika taifa kubwa la Marekani, hapana hata kidogo! Utukufu wa Wendy ni jinsi alivyoibadili sura ya Kutowezekana kuwa Inawezekana (the impossible getting done).
Wendy ni binti wa kimaskini, akiwa na umri wa miaka 19 alipewa mimba akawa mama wa watoto wawili. Hakuweza kufika chuo. Alijitahidi kujisomesha lakini maisha yalimchapa na chuo aliacha. Ila hakupoteza njia yake.
Imewatokea wengi kujikuta wakipoteza uelekeo pale mambo yanapowaendea ndivyo sivyo. Alitaka kuwa mtaalam wa sayansi ya kompyuta (computer science), baada ya kukutana na changamoto za maisha, anaamua kusaliti ndoto zake, anaamua kuwa dereva wa malori.
Usipoteze ndoto! Wendy alitaka kuwa mwanasiasa mkubwa Marekani lakini kufika kiwango alichotaka haikuwa kazi rahisi. Muhimu kushika ni kuwa dhamira inalipa. Amini kuwa chochote unachokidhamiria ndani kabisa ya maisha yako, kitawezekana kama tu hutayumba.
Ni msemo wenye kunyooka kuwa penye nia pana njia. Tambua kuwa inaanza nia kisha njia ndiyo inapatikana. Wendy aliona kila ugumu katika nyakati za ugumu wa maisha yake. Ni kweli maisha yake yalikuwa gizani, akawa hauoni mlango wa kutokea, lakini alipambana kuutafuta mlango muhimu kwa ajili ya ndoto zake.
Mlango wa kupita kuelekea kwenye mafanikio yake. Na hapa ndipo nguvu ya ndoto inapothibitika. Uwezo wa maono. Kipawa cha mwenye dhamira kinapodhihirika. Vilevile ukubwa anaoweza kuwa nao yule muota ndoto.
WENDY AMEFANIKIWA VIPI?
Ni ukweli kuwa maisha ya kisiasa ya Wendy, ndani ya chama chake cha Democrats na Marekani yote kwa jumla, yana heshima kubwa. Ila nyakati zake za utoto, aliteseka mno. Si rahisi kuamini kuwa ameweza kufika alipo sasa.
Wendy alikuwa mmoja wa watoto wanne. Wazazi wake walipotengana, mama yao alilazimika kuwalea katika hali duni aliyokuwa nayo. Mama yake alifanya vibarua vya hapa na pale ili kupata fedha za kuwahudumia watoto wake, akiwemo yeye mwenyewe Wendy.
Kutokana na ugumu wa maisha uliokuwepo nyumbani kwao, Wendy alijikuta anapoteza umakini katika masomo yake. Akiwa high school, alifeli. Alipokuwa na umri wa miaka 18, aliolewa. Alikimbilia ndoa ili kujaribu kupata nafuu ya maisha, maana nyumbani kwao palikuwa ‘pangu pakavu’ kwelikweli.
Baada ya kufunga ndoa alijifungua mtoto wake wa kwanza lakini Wendy akiwa na umri wa miaka 19, alitengana na mumewe. Hapo maisha yakawa magumu zaidi. Maana akawa mama wa mtoto, bila kazi. Afadhali mwanzoni alipokuwa bila mtoto.
Kitendo cha kurejea nyumbani, kulimfanya mama yake ayumbe kwa kiasi kikubwa. Maana Wendy alihudumiwa yeye pamoja na mtoto wake. Zingatia kuwa makazi pia hayakuwa ya uhakika. Mara leo wanaishi hapa, siku nyingine kwingine.
Wendy mwenyewe anasema: “Yalikuwa maisha yenye kuumiza sana. Sikuwa na uhakika wa kuiona kesho yenye uzuri wake. Niliumizwa sana na mtoto wangu, na nilitamani sana kuona kunakuwa na mabadiliko katika maisha yetu. Imani yangu ni kuwa kwenye kila giza, nuru hutokeza baadaye.
“Niliamini kuwa ipo nuru kwa ajili yetu, kama familia, mama yangu na ndugu zangu. Niliamini kuwa ipo nuru kwa ajili yangu, mimi binafsi na mtoto wangu. Kama kuna kitu ambacho naweza kujisifu ni kutoka tamaa. Niliamini ushindi upo.”
Wendy anasema: “Niliamini ipo siku nitakuja kuwa kiongozi, sikujua nitafikaje, maana wingu mbele yangu lilikuwa zito. Bado niliamini kuwa ipo siku, kisha nikawa nayatazama maisha yangu huku nikidhamiria siku nikipata fursa lazima nirudi kusoma.”
Elewa kuwa magumu hayakumfika Wendy mara tu alipojifungua mtoto wake au baada ya kutalikiwa na aliyekuwa mume wake wa kwanza, kwani historia yake inaonesha kuwa alipokuwa na umri wa miaka 14, alilazimika kuuza magazeti mitaani angalau apate fedha za kujikimu na familia yake.
Inaelezwa kuwa ugumu huo wa maisha ndiyo sababu ya Wendy kuanza mapenzi akiwa na umri mdogo. Kipindi yupo high school, wakati alipofikisha umri wa miaka 17, Wendy alihamia nyumbani kwa boyfriend wake, Frank Underwood ambaye alikuwa mfanyakazi wa masuala ya ujenzi.
Ni huyohuyo Underwood ambaye baadaye walifunga ndoa, wakazaa mtoto ambaye walimpa jina la Amber. Ndoa yao ilifungwa Januari 24, 1982. Baada ya kutengana, Wendy na Amber kwa pamoja wakawa mizigo ya mama yake Wendy.
“Nilijitahidi sana nisiwe mzigo kwa mama, nilipambana sana na maisha nikiwa na mwanangu Amber lakini hali ilipozidi kuwa ngumu sikuwa na jinsi zaidi ya kuhamia kwa mama, ilibidi iwe hivyo kutokana na hali halisi, sikuwa najiweza kabisa,” anasema Wendy na kuongeza:
“Kurejea nyumbani kwa mama ilikuwa muhimu zaidi kwa ajili ya ustawi wa mtoto wangu. Nisingeweza kumpa huduma bora za kimaisha, ikiwemo matibabu kama ningeng’ang’ania kusimama peke yangu. Ukweli ni kuwa sikuwa na chochote ambacho niliona naweza kufanya kumpa mtoto wangu maisha yenye afadhali.”
Zingatia kuwa alipata matokeo mabaya high school, kwa hiyo hakuwa na sifa za kudhaminiwa na Serikali ya Marekani kusoma chuo kikuu. Naye aliamini kuwa elimu ya daraja hilo ndiyo pekee inayoweza kumfanya afanikiwe kwa urahisi katika maisha yake.
Alijichangachanga kwa muda kisha akaanza masomo yake katika Chuo Kikuu cha Texas, mjini Arlington. Bahati ikawa mbaya kwake, alimudu kusoma kwa muhula mmoja tu, fedha ilikosekana ya kuendelea. Ikabidi aache.
Kipindi hicho, baba yake alikuwa amefungua duka la sandwich na piza, katikati ya Jiji la Fort Worth, Jimbo la Texas. Siku moja Wendy alimtembelea baba yake dukani kwake ndipo aliweza kukutana na Jeffry R. Davis ambaye ni mwanasheria, vilevile alipata kuwa mjumbe wa halmashauri ya Jiji la Fort Worth.
Jeffry Davis ndiye baadaye alikuja kuwa mume wa pili wa Wendy. Na Davis inayotumika kama ubini wa Wendy imetokana na Jeffry, kwani Wendy majina yake halisi ni Wendy Jean Russell.
Kuna kipindi Wendy alifanya kazi kama katibu muhtasi wa daktari katika hospitali moja binafsi kwenye Jiji la Fort Worth. Ni katika nyakati hizo ndipo mmoja wa manesi katika hospitali hiyo aliyokuwa anafanya kazi alipomuonesha kipeperushi kuhusu Chuo cha Tarrant County.
Kupitia kipeperushi hicho, alijiunga na masomo ya program ya awali ya shahada ya sheria (paralegal program) katika Chuo cha Tarrant Count. Ni kipindi hicho alianza uhusiano wa kimapenzi na Jeffry.
Mwaka 1986 baada ya kumaliza program yake, alijiunga na Chuo Kikuu cha Texas Christian, kipindi hicho aliweza kupata ufadhili wa masomo yake kutoka Serikali ya Marekani.
Mei 30, 1987, baada ya kuwa kwenye uhusiano kwa miaka miwili, Jeffry na Wendy walifunga ndoa. Maisha ya Wendy yalibadilika, waliishi kwenye nyumba yao nzuri, iliyopo Mistletoe Heights, nje kidogo ya Jiji la Fort Worth.
Pamoja na kuhamia kwenye nyumba bora, unafuu wa maisha ya Wendy ulikuwa mkubwa, kwani kipindi hicho Jeffry alikuwa anamhudumia mkewe, akimpa mahitaji yote muhumu, hususan yale yaliyohusu elimu yake.
Septemba 1988, Wendy alijifungua mtoto wake wa pili, Dru. Lakini wa kwanza kwa mume wake Jeffrey. Hata hivyo, Jeffrey baadaye alimuasili Amber, hivyo kuwa mtoto wake rasmi, kisha akawa anaitwa Amber Davis.
Mwaka 1990, alihitimu shahada yake ya kwanza ya Kiingereza. Baada ya hapo alihama na wanaye mpaka Lexington, Massachusetts, ambako alijiunga na Chuo Kikuu cha Harvard. Chuo bora kabisa duniani katika masomo ya sheria. Chuo ambacho hata Obama alisomea.
Maisha ya malezi na shule hayakuwa rahisi. Ilibidi mama yake awachukue wajukuu zake, aishi nao kipindi ambacho Wendy alikuwa anapambana kutafuta shahada yake ya sheria.
Akiwa Harvard, Wendy alianza kufanya shughuli mbalimbali za kijamii. Tayari alishaona mlango wake wa elimu umefunguka, kwa hiyo akawa anaundaa mwingine kuhusu siasa. Alijua asingeweza kupata mafanikio ya kisiasa bila elimu.
Baada ya kumaliza Harvard kisha kusoma uwakili, Wendy alianza kazi kama karani wa Jaji wa Wilaya. Jeffry baadaye alianzisha kampuni inayoitwa Safeco Title Co. ikijihusisha na masuala ya bima, Wendy akawa mmoja wa wamiliki.
ALIVYOANZA KUCHOMOZA KISIASA
Mwaka 1996, aligombea ujumbe wa Halmashauri ya Jiji la Fort Worth akashindwa kwa tofauti ya kura 90. Mwaka 1999, aligombea tena ujumbe huo na kushinda. Alikuwa mjumbe kwa miaka tisa na katika kipindi chake amekuwa mtetezi hasa katika sekta ya usafiri, maendeleo ya uchumi na ujirani mwema.
Kipindi akiwa mjumbe wa Halmashauri ya Jiji la Fort Worth, Davis alikuwa mwanachama wa Republican. Anasema alipenda Republican kwa kuvutiwa na mbunge mwanamke (Congresswoman), Kay Granger aliyekuwa akitokea Fort Worth.
Alikichagua Republican na kuchanga fedha kwa wagombea wa chama hicho. Mwaka 2006 alimchangia Granger dola 1,500. Aprili 1999, alimchangia Rais wa 43 wa Marekani, George W. Bush dola 2,500 wakati alipokuwa anawania urais kwa tiketi ya Republican.
Michango hii ina maana gani? Kwamba tayari uchumi ulishakuwa vizuri. Dola 2,500 kwa chenji ya shilingi ni zaidi ya milioni 5. Huwezi kutoa mchango wa fedha hizo kama mambo yako bado hovyo. Mambo yalishamnyookea.
Kipindi hicho hakuwa Wendy yule wa maisha ya kutangatanga, bali mwenye maisha ya uhakika. Watoto wake wakisoma shule bora. Huduma bora zilitoka kwa mama. Kila kitu kinakwenda vizuri, maana mama yupo vizuri. Hii inatosha kuonesha kuwa maisha yanaweza kubadilika. Muhimu ni kushika njia yako.
Mwaka 2008, akiwa na tiketi ya Democrats, alishinda Useneta katika Seneti ya Texas, akiwakilisha Jimbo la District 10. Mwaka 2012 aligombea na kushinda tena, hivyo kushikilia nafasi hiyo mpaka Januari 13, mwaka huu.
Sababu ya kuachana na useneta wa Texas ni mbio zake za kuwania ugavana wa Texas katika Uchaguzi Mkuu wa Texas mwaka 2014. Alishinda uteuzi ndani ya Democrats, akawa mwanamke wa kwanza kupitishwa na chama hicho tangu mwaka 1994, alipoteuliwa Ann Richards ambaye alishindwa na George Bush wa Republican.
Hata hivyo, Wendy hakuweza kushinda ugavana wa Texas, kwani alishindwa na aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Greg Abbott, aliyegombea kupitia Republican.
Pamoja na kushindwa ugavana, Wendy amebaki kuwa mwanasiasa maarufu, huku akitarajiwa kuendelea kufanya vizuri kisiasa katika nyakati zinazokuja.
Kikubwa ambacho anakumbukwa ni jinsi alivyowasilisha muswada na baadaye kuwa sheria kuhusu katazo la utoaji mimba.
Miswada na mapendekezo yake ni mingi, vilevile ipo sheria ya uvutaji bangi ambayo alipambana kuhakikisha inaanzishwa ili kudhibiti uvutaji wa mihadarati.
BADO UNAAMINI HAIWEZEKANI?
Wendy na Jeffry waliachana mwaka 2003 na baada ya talaka kutolewa rasmi mwaka 2005, ilikubaliwa Wendy awe analipa dola 1,200, yaani zaidi ya shilingi milioni 2.4 kwa mwezi kwa ajili ya matunzo ya mtoto.
Ni kipindi ambacho maisha ya Wendy yameshakuwa juu, hivyo Jeffry alitaka alipwe fedha kwa sababu mtoto alibaki kwake. Yote yaliwezekana pasipo usumbufu wowote.
Vyombo vya habari vimekuwa vikimmulika na mafanikio yake ya kisiasa yamebeba mshangao wa namna mwanamke huyu ambavyo hakuwahi kukatisha ndoto zake pamoja na ugumu uliokuwa ukimkabili.
Jeffry alimkuta Wendy anajiendeleza na masomo. Hata baada ya kufunga ndoa na kuuona urahisi wa maisha, bado Wendy alisimamia maono yake, alijitahidi mpaka kufika Harvard.
Mwaka jana wakati anawania ugavana wa Texas, aliushangaza ulimwengu alipochangisha fedha dola milioni 12 (shilingi bilioni 25.9) ndani ya usiku mmoja ambazo zilimsaidia wakati wa kampeni.
Anza na wewe leo, usigeuke nyuma. Kufanya hivyo ni mwiko, kwani utasababisha matunda yako yaliwe na wengine. Kila la heri muota ndoto!







Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment