Luqman
Maloto
ISHI kwa
tabasamu kila siku. Hata uwe ndani ya nyakati ngumu kiasi gani, elewa tu kuwa
utavuka. Mungu aliyekuumba anakuona, analo fungu lako bora kabisa.
Jambo la
kutambua na kuheshimu ni kuwa Mungu anajua namna ya kukupa mafanikio. Anaweza
kukufanikishia ukiwa kijana, wakati wa makamo au hata uzeeni.
Mafanikio
yanaweza kuja kwako moja kwa moja (direct) au kupitia mlango wa nyuma
(indirect). Ila yote ni mafanikio yako.
Mafanikio
mlango wa nyuma; Yale ya kuja moja kwa moja hayahitaji ufafanuzi, kwa upande wa
yenye kuja kupitia mlango wa nyuma ni kama vile mzazi kuvuna kupitia kwa
mwanaye aliyemzaa na kumlea kwa tabu au hata mtoto aliyemuasili na kumlea.
Mungu
amekuwa na utaratibu usiokoma, wa kupandikiza uzao wa matajiri na wafalme
katikati ya familia zinazoishi kwenye lindi la umaskini.
Zingatio kwa
mama; Usitoe mimba, usinyonge kichanga wala usitelekeze mtoto. Huyo anaweza
kuwa ndiye ameletwa na Mwenyezi Mungu kuwa mafanikio yako ila wewe unayakataa.
Baba;
Usikatae mimba, usiwe chanzo cha mimba kutolewa, usikimbie damu yako, hakikisha
unakuwa mlezi bora wa mwanao kwa hali na mali. Huwezi kujua ni zawadi gani
ambayo mtoto huyo ametumwa na Mungu akuletee.
Wazazi;
Hakikisha mnatoa malezi bora kwa watoto. Kile ambacho mnakifanya, kiwe ndiyo
uwezo wa juu kulingana na nafasi. Wapeni watoto mapenzi makubwa na muwafanye
wawe na furaha. Hao ni hazina yenu ya baadaye.
Mtoto; Wewe
siyo nchochote bila wazazi wako. Wangeamua, ungetolewa ukiwa mimba changa.
Unapopata mafanikio, elewa kuwa wazazi wako wana thumni yao kwenye kila jasho
lako. Wafanye wazazi wako wafurahie kipato chako, usiwaache wakipata shida na
wewe upo ilhali uwezo wa kuwasaidia unao.
Mafanikio
yako yatapaa zaidi, vilevile utakuwa ni mwenye kubarikiwa mno kama wazazi wako
utawalinda kadiri kipato chako kinavyoruhusu.
PATRICIA
HICKEY ANAVUNA ALICHOPANDA
Patricia
Hickey ni mama wa mwanamuziki mkubwa duniani, Mariah Carey. Anavuna
alichopanda, alichostawisha na alichokitunza. Anaishi kwa uhakika mkubwa.
Maisha yamekuwa bora mno.
Maisha ya
Pattie wakati anamzaa Mariah yalijaa dhiki mno. Kwanza alitengwa, yeye ni
Mzungu mwenye asili ya Ireland, akaenda kuzaa na mtu mweusi, Alfred Roy,
Mmarekani –Mwafrika mwenye asili ya Venezuela.
Babu yake
Mariah, Francisco Nunez, alipohamia Marekani kutokea Venezuela, alijiongeza
jina la Carey na ndiyo maana staa huyo anaitwa Mariah Carey.
Pattie
alifanya kazi kama mkufunzi wa sauti (vocal coach), vilevile alijishughulisha
na kuimba muziki wa Opera ambao asili yake ni jamii ya Latini, ukiimbwa zaidi
makanisani, hasa Roman Catholic.
Pattie na
Alfred walikutana wakati mama akiimba Opera, baba akifanya kazi ya uinjinia wa
vyombo vya muziki. Na hapo ndipo mapenzi yao yalipoanza.
Walipofunga
ndoa, familia ya Pattie iliwatenga kwa sababu hawakuona sawa mtoto wao Mzungu
kuolewa na mwanaume mwenye asili ya Afrika.
Tabu ya
kwanza ya Pattie ilianzia hapo. Alimpenda Alfred wake, wakati huohuo wazazi
wake ndiyo hawakutaka kabisha kumsikia. Uamuzi wake ukawa kuziba masikio, akasikiliza
moyo unavyoongea kisha akasonga mbele.
Wakiwa ndani
ya Jiji la New York, kila kona waliishi Wazungu, na katika miaka ya 1960,
Mwafrika alionekana kama kituko vile.
Familia ya
Carey ilipata wakati mgumu sana. Jamii iliwasimanga na kuwatenga. Mama yake
Mariah (Pattie), alibezwa kwa kufanya uamuzi ambao Wazungu waliuita wa
kipumbavu, kuolewa na Mwafrika.
Mwaka 1969
wakati Mariah anazaliwa, alikuta maisha ni magumu mno kwa sababu ya jinsi
familia yao ilivyokuwa inachukuliwa kama kituko.
Mariah
aliwahi kusema: “Yalikuwa maisha magumu sana. Kila kona nilikutana na wasichana
wa Kizungu, mimi nilionekana kituko. Niliishi kwenye familia isiyokubalika
kabisa.”
Pattie naye
alizungumza: “Nilitengwa na kuitwa kila jina baya lakini sikuweza kuiacha
familia yangu. Watoto wangu ni muhimu sana kwangu, sikujali wana rangi gani.
Kwao walionekana wabaya ila kwangu ni malaika bora kabisa.”
Mateso hayakuwa hayo tu, msoto mwingine
ulifuata baada ya Alfred na Pattie kuachana. Malezi ya mama tu bila uwepo wa
baba, na kukosa kipato cha uhakika, vilisababisha changamoto kubwa.
Dada mkubwa
wa Mariah, Allison aliambatana na baba yake, huku na Mariah mwenyewe na kaka
yake Morgan wakibaki na mama yao.
Wakati
wazazi wake wakitengana, Mariah alikuwa na umri wa miaka mitatu. Alianza
kushuhudia maisha ya kuhamahama kwa sababu mama yake hakuwa na uwezo mzuri wa
kumudu kulipia makazi ya kudumu.
Pattie
aliendelea na kazi yake ya kuimba Opera, vilevile kufundisha sauti, kiasi
alichopata alikielekeza kwa wanaye ambao aliota kuwapa maisha bora na ya
uhakika.
Mariah
alipokuwa na umri wa miaka minne, alianza kupenda muziki na mara nyingi akiwa
nyumbani alipenda kuwa karibu na redio ili kusikiliza nyimbo na kukariri.
Alipoanza
shule ya msingi, mapema sana alifanya vizuri masomo ya muziki, fasihi na sanaa
kwa jumla.
Wakati
Mariah anamaliza shule ya msingi, mama yake (Pattie), alikuwa ndiyo anafanikiwa
kupata kipato cha uhakika, angalau akaweza kupata nyumba (apartment) ya kuishi
na familia yake.
Mariah
alipojiunga Shule ya Sekondari ya Juu (High School) ya Harborfields, iliyopo
Greenlawnd, New York, tayari alikuwa na uwezo wa kuandika mashairi na
kuyatungia sauti. Hivyo uwezo wa kutunga nyimbo aliupata kipindi hicho.
Kuhusu
muziki, Maria anasema kuwa tamaa ya kufanikiwa kupitia muziki aliipata tangu
akiwa mtoto kwa sababu ya namna ambavyo aliona maisha ya shida kwenye familia
yao.
“Ilikuwa
ngumu sana kwangu, kuhamahama kila mara, nikaona bora nijikuze mimi mwenyewe.
Fikiria mwenyewe wazazi wangu wameachana, na kila siku nilijiona wa tofauti
ukilinganisha na wengine waliokuwa majirani zetu.
“Nilikuwa
mtu wa jamii tofauti, Mwafrika. Na hiyo wakati mwingine ni tatizo kabisa. Kama
unaangalia njia fulani, kila anayepita ni msichana wa Kizungu, inabidi na mimi
nipite, baadaye unagundua upo peke yako. Najikuta sifanani nao,” anasema
Mariah.
Akiwa high
school, Mariah alianza kujitahidi kuonesha kipaji chake katika matukio
mbalimbali na kila aliyepata kumsikiliza, alimuelewa kwa haraka na kukubali
kwamba hakika ana kipaji kikubwa.
Mariah
alimtafuta mwanamuziki mkongwe wa R&B, Gavin Christopher, akawa anatunga
naye nyimbo na kufanya mazoezi pamoja, hivyo kuendelea kukuza kipaji chake.
MARIAH NA MAISHA
YA KUTANGATANGA
Pamoja na
hali ya mama yake kuimarika, Mariah alipomaliza high school hakutaka tena
kuendelea kukaa nyumbani, aliamua kujitupa kutafuta mafanikio ya kimaisha
kupitia muziki.
Mariah
anasema kuwa msukumo mkubwa kutafuta mafanikio ya muziki wake ulitokana na
dhiki ndani ya familia yake lakini zaidi ya ubaguzi wa rangi aliokuwa
anakabiliana nao.
Kazi kubwa
alianza kuifanya baada ya kuondoka nyumbani kwao ni uhudumu katika migahawa. Alipata
vibarua vya hapa na pale kwenye migahawa mbalimbali ili kupata fedha za kulipia
pango na mahitaji mengine.
Rekodi
zinaonesha kuwa Mariah alikuwa akitimuliwa kazi mara kwa mara. Inaelezwa kuwa
hakuna mahali ambako aliwahi kufanya kazi na kudumu kwa wiki mbili.
Sababu ya
kutimuliwa mara kwa mara ni kwa kuwa hakuwa akitoa muda mzuri kwenye kazi,
badala yake aliwaza zaidi muziki wake na jinsi ya kutoka mpaka kufikia kuwa staa.
Alihangaika
usiku na mchana kutengeneza kanda, kama demo iliyokuwa na nyimbo nne kisha
kuanza kutafuta makampuni ya kuingia nayo mkataba kwa ajili ya kuundeleza
muziki wake.
Baada ya
kukamilisha demo yake, haikuwa rahisi kupata mkataba, kwani kila alipokwenda
kwenye makampuni ya muziki, alifeli, zaidi aliambiwa hajui kuimba.
Katika
kuhangaika huku na huko, ndipo Mariah alipokutanishwa na mwanamuziki wa Pop
aliyekuwa akiinukia kwa wakati huo, Brenda K. Starr ‘The Freestyle Queen’.
Mariah
alipokutana na Starr, waliunganisha urafiki ambao umuwezesha kuwafikia wadau
wakubwa wa muziki. Hii ni kwa sababu kwa kipindi hicho Starr alikuwa
ameshatengeneza jina kwenye muziki.
Hata hivyo,
mambo bado hayakufunguka, mwaka 1988, Starr alimshirikisha Mariah kwenye demo
yake yenye nyimbo kadhaa. Demo hiyo Starr aliipeleka kwa Tommy Mottola ambaye
ni Bosi Mkuu wa kampuni kubwa ya muziki Marekani na duniani kote, Columbia
Records.
Mottola
alipopata demo hiyo, aliichukua na kuisikiliza akiwa kwenye gari, baada ya
nyimbo tatu alijikuta anavutiwa na sauti ya Mariah.
Baada ya
hapo Mariah ndiye aligeuka dhahabu, maana Mottola alimtafuta usiku na mchana
ili amsainishe mkataba waanze kazi.
Zilipita
wiki mbili Mottola akimtafuta Mariah, ndipo alifanikiwa kukutana naye, kufanya
mazungumzo kisha kumsainisha mkataba ambao ulimuwezesha kuingia kwenye ramani
ya biashara kubwa ya muziki.
Albamu yake
ya kwanza yenye jina Mariah Carey, ilitikisa mauzo Marekani, Ulaya na duniani
kote, vilevile ilifanikiwa kushika nafasi ya kwanza kwenye chati za Billboard
200, huku nyimbo nne zikikamata namba moja katika chati za Billboard Hot 100.
Hiyo ilikuwa
rekodi ya peke yake, kwani kabla ya hapo ni Kundi la The Jackson 5, lililowahi
kufanikiwa kuingiza nyimbo nne kwenye Billboard Hot 100 kutoka kwenye albamu
moja.
UNADHANI
NINI KILIFUATA?
Hakuna
kingine zaidi ya kuogelea kwenye mafanikio na utajiri. Kuonana na Mottola
kulibadili kila kitu, maana bosi huyo alihitaji fedha ambazo aliziona zipo kwa
wingi kupitia kipaji kikubwa cha muziki alichonacho Mariah.
Ghafla
Mariah akageuka bosi, kuanzia mwanzoni mwa miaka ya 1990, magari ya kifahari na
kuishi kwenye majumba mazuri yenye umiliki wake, siyo kitu cha ajabu tena.
Chini ya
Columbia Records, Mariah aliendelea kufyatua kazi zenye mafanikio kwa miaka 10
mfululizo mpaka mwaka 2000 walipovunja mkataba.
Bosi Mottola
alivutiwa na Mariah, wakavutiana, penzi jipya lilizaliwa, ikafuata ndoa lakini
mwaka 1998 walitengana. Na hiyo ndiyo ilikuwa sababu ya mkataba na Columbia
kufikia ukingoni.
Mwaka 2000,
alisaini mkataba wenye thamani ya dola milioni 100, na Kampuni ya Virgin
Records America lakini ilibidi Mariah alipe dola milioni 50 kuununua mkataba
huo ili apumzike.
Kipindi
hicho Mariah alikuwa na msongo wa mawazo ya kutengana na Mottola. Mwaka 2002,
Mariah alisaini mkataba wa fedha nyingi na Island Records ambao ulimrudisha
kwenye soko, vivyohivyo kuendelea kutengeneza pesa nyingi.
Mpaka sasa,
Mariah anakadiriwa kuwa ameshauza zaidi ya nakala milioni 200 katika kazi zake,
hivyo kumfanya kuwa mmoja wa wanamuziki ambao wameuza zaidi katika historia ya
muziki duniani.
UTAJIRI WA
MARIAH
Mariah
anakadiriwa kuwa na utajiri unaofikia dola milioni 550 ambazo kwa chenji ya
shilingi ya Kitanzania, unapata takriban trilioni 1.1.
Kwa utajiri
huo, Mariah amekuwa na wakati mzuri wa kumpa mama yake (Pattie), mahitaji yote
muhimu na kuongezea starehe.
Pattie wa
sasa, siyo yule wa kuungaunga maisha, anaendeshwa kwenye magari ya kifahari na
madereva walioajiriwa na mwanaye (Mariah).
Umri
unakwenda lakini afya bado ipo, maana anapata matunzo ya kutosha. Sasa anakula
matunda matamu ya kuzaa na kulea mtoto katikati ya chuki na manyanyaso.
Pattie ana
umri wa miaka 78 kwa sasa lakini hakuna usumbufu wa umri anaoupata, maana
mahitaji yote muhimu anayapata kwa ukaribu, mwanaye amemuwekea watumishi
wanaomuangalia kwa ukaribu sana.
Mariah yupo
naye kwa ukaribu mno, anamtoa out na vizuri ni kuwa anajua kwamba mama yake
anapenda maonesho ya muziki wa Opera, kwa hiyo humpeleka kuburudika.
USHUJAA WA
PATTIE
Kama
angefuata masharti ya wazazi wake na ndugu wengine kwamba hatakiwi kuwa na
mwanaume mwenye asili ya Afrika, maana yake Mariah asingezaliwa.
Maana
ukamilifu wa Mariah ni mchanganyiko wa Kibaiolojia kati ya Pattie na Alfred.
Hakuna namna nyingine ya kumpaka Mariah nje ya hapo.
Hii inakuja
na maana kuwa uamuzi wa kukubali kutengwa ndiyo ushujaa uliosababisha ujio wa
Morgan, Allison na Mariah.
Pointi ya
pili ni jinsi alivyopambana kuwalea watoto wake. Alikuwa maskini lakini
hakuchoka kutafuta mpaka kuhakikisha wanaye wanasoma japo kufikia kumaliza high
school.
Pattie
alifanya kazi usiku na mchana kwa kuungaunga mpaka kufanikisha kipato kizuri
chenye kuwahakikishia mahitaji watoto wake, hasa Mariah na Morga, maana Allison
alikwenda kuishi na baba yake.
Pattie
aliigundua sauti nzuri ya Mariah na ndiye ambaye alianza kumtafutia njia za
kukuza kipaji chake. Alimpeleka mpaka kwenye muziki wa Opera lakini Mariah
hakuvutiwa nao. Alitaka kuimba Pop na R&B ili atengeneze fedha.
USHUJAA WA
MARIAH
Kutambua
kipaji ni jambo moja lakini kukifuatilia ni jambo la pili na lenye umuhimu
mkubwa. Huwezi kukaa nyumbani kusubiri kwamba ndoto zako zitatimia.
Tafakari
jinsi alivyokuwa binti mrembo lakini kwa sababu alikataa umaskini na dharau ya
ubaguzi wa rangi, aliamua kutomsumbua mama yake, akakubali kufanya vibarua vya
uhudumu wa migahawa ili apate fedha za kujisukuma kulipia pango, vilevile za
kumuwezesha kutengeneza demo.
Ni
mihangaiko hiyo ndiyo iliyomuwezesha kukutana na Starr kisha Mottola. Na zaidi
ni uchapakazi wake ndiyo umewezesha kuwa mwanamuziki tajiri.
Ana umri wa
miaka 46 kwa sasa, ni mama wa watoto wawili, wa kiume anaitwa Moroccan Scott
Cannon, wa kike ni Monroe Cannon.
Baada ya
kuachana na Mottola, mwaka 2008 alifunga ndoa na rapa, Nicholas Scott Cannon
‘Nick Cannon’ ambaye pia ni muigizaji, vilevile comedian.
Cannon ndiye baba wa watoto hao wawili wa
Mariah, kwani katika ndoa yake ya kwanza na Mottola, hawakubahatika kupata
mtoto.
SOMO LA
KUJIFUNZA
Vumilia
manyanyaso na ukatize katikati ukijiamini kwa sababu hakuna gumu lenye kudumu.
Mungu aliamua kumtengeneza Mariah kuwa malkia katikati ya familia dhalili
kabisa.
Watu
waliokuwa wakimcheka Mariah na ndugu zake kwa sababu ya Uafrika wao, leo hakuna
mwenye ubavu wa kuinua sauti kufanya hivyo.
Mariah
amewaacha mbali kabisa. Ni vizuri kujifunza kuwa unaweza kumdharau mtu kwa
mtazamo wa juu lakini kumbe ndiye mwenye mbegu ziletazo matajiri, wafalme na
malkia wa fani mbalimbali.
Mheshimu
kila mtu na usibague, maana huijui kesho yako na yake. Amini tu kwamba kila mja
na bahati yake.
0 comments :
Post a Comment