ads 728x90 B

ULINZI WA BUNDUKI NI DHAIFU MNO!




ALIPATA kutokea kijana mzuri lakini maskini kwenye utawala wa Kifalme. Wazazi wa kijana huyo walikuwa kwenye daraja la huruma kutokana na ufukara waliokuwa nao. Kijana huyo aliitwa Jamal.
Kwa uzuri wake Jamal alipendwa mno na wanawake. Hata hivyo, Mungu alimjalia unyenyekevu, kadiri alivyopendwa ndivyo alivyozidisha nidhamu.
Sifa ya kuwa kijana mwenye nidhamu, iliongeza mvuto wa Jamal. Wanawake kwenye makutano yao ya ususi, visimani, mitoni, sokoni na kwingineko walimzungumzia Jamal kwa kumpamba.
Jinsi wanawake walivyokuwa wakimzungumzia, ndivyo na wengi wao walivyopata hamu ya kuwa na Jamal kimapenzi. Miongoni mwa wanawake hao, walikuwepo pia wake za watu.
Jamal alimpenda Daniya, msichana mrembo aliyezaliwa na wazazi wenye uwezo wa wastani. Jamal alifanya kazi kwa bidii ili kufanikisha malengo yake ya kuwa na maisha bora, vilevile kutimiza ndoto zake za kumuoa Daniya.
Ikaja kutokea, kati ya wanawake waliompenda Jamal, alikuwepo pia mke wa mfalme. Alitamani mno kuyapata mapenzi ya kijana mwenye kuimbwa kwa nyimbo nzuri za kupendeza na kila mwanamke.
Mzozo ukawa mkubwa zaidi baada ya mfalme naye kudhamiria kumtwaa Daniya ili awe mkewe. Yaani akawe mke wa pili wa mfalme.
VITA YA MAPENZI
Wazazi wa Daniya walikubali binti yao aolewe na mfalme. Si unajua tena, mzazi anawezaje kukataa mtoto wake kuolewa na mfalme?
Hata hivyo, haikuwa rahisi kwa mfalme kumpata Daniya. Vivyo hivyo, haikuwezekana kwa mke wa mfalme kulipata penzi la Jamal.
Mfalme baada ya kuona dhamira yake ya kumuoa Daniya inashindikana, alimuona Jamal adui, kwamba Daniya hisia zake zote zipo kwa Jamal. Hivyo, mfalme akapanga kumuua Jamal.
Mke wa mfalme naye kutokana na wakati mgumu ambao aliupata katika mpango wake wa kulinasa penzi la Jamal, akili yake ikamtuma kumuua Daniya.
Mipango ikasukwa! Kuna kipindi Jamal alifungwa gerezani na kuandaliwa kuuawa lakini mke wa mfalme alimtorosha.
Mke wa mfalme pia akaagiza Daniya akamatwe na kuwekwa jela, mfalme alipopata taarifa alitoa amri aachiwe huru.
Kuna wakati mke wa mfalme alimnyatia usiku na mchana Jamal. Alitengeneza mpaka funguo za mlango wa Jamal. Mke wa mfalme aliingia chumbani kwa Jamal. Jamal alipoingia chumbani kwake, alimkuta mke wa mfalme akiwa mtupu kisha kumlazimisha washiriki mapenzi.
Siku moja kulitokea mtifuano mzito chumbani kwa Jamal baada ya kuingia na kumkuta mke wa mfalme amejilaza akiwa mtupu. Mke wa mfalme alilazimisha mapenzi, Jamal alikataa katakata kuwa hawezi kumsaliti Daniya wake.
Baada ya mvutano wa muda mrefu, mke wa mfalme alisema: “Nilijitahidi kukulinda mfalme asikuue, ila kwa hivi ulivyonidhalilisha, sasa huna budi kufa.”
Mke wa mfalme alitoka chumbani na kuwapitia walinzi wake nje kisha wakarejea kwenye kasri la mfalme akiwa na hasira kali.
Njia nzima hakuzungumza na mtu yeyote. Alichotaka ni kufika kwa mumewe (mfalme) na kumshawishi atume vikosi vyake vikamuue Jamal.
Mke wa mfalme aliingia ndani himahima, moja kwa moja mpaka chumbani kwa mfalme. Alimkuta mfalme katikati ya jaribio la kumbaka Daniya.
Hasira za mke wa mfalme ziliongezeka, alimsukuma mfalme na kwenda kumkaba shingo Daniya, ugomvi ukawa mkubwa mno.
Mfalme baada ya kuona hali ni mbaya, aliita askari wake, wakawatenganisha mke wa mfalme na Daniya ambaye alibaki analia. Muonekano wake ulithibitisha unyonge wake na maumivu makali juu ya uonevu aliokuwa anafanyiwa.
Mke wa mfalme na Daniya baada kushatenganishwa, kila mmoja alifungiwa kwenye chumba chake. Upande wa pili mfalme alipokea taarifa kutoka intelijensia yake kuwa mkewe alionekana mara kadhaa akiingia na kutoka chumbani kwa Jamal.
Taarifa hizo ziliamsha hasira kali kwa mfalme. Yeye aliamini kuwa Jamal ana uhusiano na mkewe. Akajiongeza pia kwamba Daniya hamtaki kwa sababu ya kiburi anachopewa na Jamal.
Mfalme akaagiza askari wake wakamteke na kumuua Jamal. Askari 20 wa mfalme wakiwa na silaha zao, walivamia nyumbani kwa Jamal na kumteka kisha kwenda kumuua porini.
Jamal alipigwa mno, alipata mateso makali kupita kiasi. Agizo la mfalme ni kuwa Jamal atenganishwe kichwa na kiwiliwili kisha kichwa apelekewe ushahidi.
Pale walipokuwa wanamtesa Jamal ni chini ya mwembe. Hivyo kabla Jamal hajafa na wakiwa wanajiandaa kumchinja kama walivyoagizwa na mfalme, tawi kubwa la mwembe lilikatika na kuwaangukia walinzi watatu kisha kundi kubwa la nyuki liliwashambulia.
Walinzi 17 walikimbia na nyuki waliwakimbiza na kuwang’ata kadiri walivyokimbia. Walinzi watatu walikuwa hoi kwa maumivu ya kuangukiwa na tawi kubwa la mwembe na walishindwa kulisukuma pembeni ili watoke. Lilibaki limewakandamiza huku wakipiga kelele, mwisho fisi walitokea na kuwala.
Nyuki wote waliwakimbiza wale askari wa mfalme waliokuwa wanakimbia. Jamal akiwa na maumivu makali alinyanyuka na kukimbia kwa kujikokota kuelekea usawa wenye usalama.
Mfalme alishangaa giza linaingia askari wake hawarudi. Akiwa anasubiri kwa hamu kubwa, aliona askari sita wakiwa wanaingia kichovu, wamevimba. Wakasimulia madhila ya tawi la mwembe na nyuki, vilevile kutokewa na chatu ambaye alimmeza mwenzao mmoja. Na kwamba wengine walipoteza maisha kwa shambulio la nyuki pamoja na kuangukiwa kisha kubanwa na tawi la mwembe.
Upande wa pili Daniya alipofunguliwa kwenye jumba la mfalme, aliona akirejea nyumbani kwao, angetafutwa na kuuawa, hivyo akaamua kwenda porini ili apotelee mbali.
Safari ya usiku na mchana, akila matunda, akinywa maji kwenye madimbwi na chemchemi za porini, hatimaye aliishiwa nguvu na kupoteza fahamu.
Jamal baada ya kunusurika kifo, aliamua kufanya maisha yake porini. Alitengeneza kibanda na kuishi kwa kuwinda wanyama pori. Akiwa kwenye mawindo yake, siku moja alimuona mwanamke amelala, akamsogelea.
Hakuamini macho yake alipogundua ni Daniya. Mwanamke anayempenda kuliko uhai wake. Alimbeba mpaka kwenye kibanda chake. Alipomfikisha, alichukua maji na kumkandakanda. Daniya alizinduka na kupigwa na mshangao kuona anayemhudumia ni Jamal wake. Mwanaume anayemiliki kila kitu ndani ya moyo wake.
Jamal alimpa chakula Daniya, alimpa maji akanywa. Walizungumza mengi. Wakapeana ahadi kuwa kifo pekee kitawatenganisha. Wakakumbatiana na kusemezana kuwa jinsi walivyokutana na changamoto, ndivyo mioyo yao inavyoshibana. Kwamba misukosuko imekuza mapenzi yao.
Siku moja Jamal akiwa kwenye mawindo yake, alisikia nyasi zinatikisika akajua ni myama, akalenga mshale lakini ajabu ikatoka sauti ya binadamu. Ghafla Jamal akawa amezungukwa na askari wa mfalme.
Kumbe, mfalme baada ya kumtafuta sana Daniya, aliamua kuchukua askari wake na kuingia nao porini kumsaka. Wakiwa katikati ya pori, aliwaaga askari wake na kwenda pembeni kujisaidia. Ni hapo ndipo Jamal alihisi ni mnyama, pale nyasi zilipokuwa zinatikisika.
Mshale uliingilia mkono wa kushoto na kuzama moja kwa moja kwenye moyo. Mfalme alifikwa na mauti palepale. Askari kuona mfalme wao amekufa, wakaanza kumsulubu Jamal.
Wakiwa wanataka kumuua, walitokea simba watano, wale askari kila mmoja akakimbia upande wake, simba wakawafukuza.
Jamal alipona kwa mara nyingine, alirejea kwenye kibanda chake na kumsimulia Daniya. Wote walishikwa na woga juu ya kile ambacho kingetokea.
Askari wengi waliuawa na simba, huku wengine ikishindwa kujulikana walipopotelea. Askari nane walirejea salama na kutoa taarifa za kuuawa kwa mfalme, aliyepigwa mshale na Jamal.
Kati ya askari hao nane, watatu walikuwepo kwenye jaribio la kwanza la kung’atwa na chuki, hivyo waliwasimulia maajabu wazee kuwa Jamal anaweza kuwa siyo binadamu wa kawaida.
Baada ya tafakuri ya wazee kwa wiki nzima, lilipatikana jawabu la kumtafuta Jamal ili asimikwe ufalme kutokana na historia ya nidhamu yake, jinsi ambavyo amekuwa akipona katika mkono wa kifo, hujuma alizofanyiwa za kutaka kuuawa, vilevile anavyopendwa na watu.
Ujumbe wa wazee wanne kwa kuongozana na askari sita, uliingia porini kumtafuta Jamal. Baada ya majuma mawili, waliweza kukizingira kibanda cha Jamal kisha kumpata mwenyewe na kuzungumza naye.
Wazee walirejea kishujaa. Ilifanyika sherehe kubwa ya kumsimika Jamal ufalme. Baada ya hapo ndoa ilifungwa kisha Daniya naye alisimikwa umalkia. Jamal akawa mtawala mkuu, Daniya akatambulika kama first lady.
NINI TAFSIRI?
Mungu analinda wakati wote. Akiamua usipate baya lolote na halitakutokea.
Hapo ulipo, hujui ni mipango mingapi miovu imewahi kupangwa ili kuondoa uhai wako na Mungu akaidhibiti.
Jamal na Daniya, walikula raha, heshima na madaraka makubwa baada ya kulindwa na Mungu.
Jiulize tawi la mwembe lilikatwa na nani? Nyuki walitokea wapi? Simba walinusa nini? Na kwa nini Simba hawakujishughulisha na Jamal, badala yake waliwafuata askari waliokuwa wanakimbia?
Ni kwa nini Jamal na Daniya hawakuwahi kushambuliwa na wanyama hata mara moja? Shika jibu; Ulinzi wa Mungu upo karibu mno na waja wake wema. Waja wake wenye kuonewa. Mungu hapendi mja wake aonewe.
Dk. Steven Ulimboka alipona vipi Msitu wa Pande? Unadhani waliomfanyia unyama ule walitaka leo awe hai? Nani aliyempeleka Msitu wa Pande mtu yule aliyemuona kwa mara ya kwanza? Polisi nao walimkuta akipumua. Acheni Mungu apewe utukufu wake!
Ukidhani Absalom Kibanda yupo hai kwa sababu waliomvamia na kumfanyia unyama uliogharimu afya na macho yake hawakutaka kumuua, utakuwa unajidanganya.
Hata wewe hapo ulipo, inawezekana kabisa imeshakuwepo mipango kadhaa ya kuukatisha uhai wako lakini ulinzi imara zaidi wa Mungu, unateketeza silaha za adui bila wewe kutaarifiwa.
Wengi hudhani bunduki ni silaha bora zaidi ya kujilinda. Mbona tunao viongozi wengi waliouawa na kupinduliwa wakati walikuwa wanalindwa na bunduki?
ISHI KWA IMANI
Huna fedha, tena wewe ni maskini, lakini unayo sababu moja tu muhimu ya kuringa. Kwamba wewe ni mteule wa Mungu ambaye ndiye mlinzi mkuu wa maisha yake.
Ni nani mwenye kuweza kufanikisha dhamira ovu juu yako kama Mungu Mfalme hataki? Ukielewa hivyo, hutakuwa na hofu ya kitu. Mungu anakulinda mno.
Acha maadui waje, Mungu atakuongoza kuwashinda. Bunduki silaha dhaifu mno, makombora na vifaru ambavyo Mungu ameviweka kukulinda vina uwezo mkubwa kuliko Jeshi la Marekani. Kaa na Mungu kila siku, kisha jiamini!
Ndimi Luqman Maloto
Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment