ads 728x90 B

Polisi wawavutisha unga mateja




Luqman Maloto
POLISI Tanzania hugeuka watumwa wanapowakamata watumiaji wa madawa ya kulevya, kwani hulazimika kuwatafutia mihadarati hiyo na kuwapa watumie ili kuwapa ahueni wakiwa mahabusu.
Watumiaji wa madawa ya kulevya, maarufu kama mateja, hupatwa na maumivu makali, kukosa nguvu, mwili kulendemka na kuwashwa mwili mzima pindi wanapopitisha muda bila kutumia mihadarati hiyo, hivyo kuwa usumbufu mkubwa kwa polisi waliowakamata.
www.luqmanmaloto.com inazo taarifa mpya na za muda mrefu kuhusu madhila ambayo polisi huyapata kutokana na kuwakamata mateja na kuwahifadhi mahabusu, hivyo kuwafanya wakae muda mrefu pasipo kupata madawa yao.
Mkuu wa kituo kimoja cha polisi, ndani ya Mkoa wa Kinondoni, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, amemweleza mwandishi wetu kuwa kumfungia teja mahabusu ni mateso, kwani zipo nyakati hulazimika kutafuta unga ili kuwapa watumie.
Mkuu huyo wa kituo aliyeomba kuhifadhiwa jina kwa sababu za kikazi, alisema: “Kukaa na mateja mahabusu ni utumwa, ukiwa nao lazima ujiandae kuwatafutia madawa yao wavute. Na huwa inatubidi tufanye hivyo ili kuwasaidia wawe sawa.”
Aliongeza, mateja huwaelekeza mahali ambako huwa wanauziwa unga, hivyo kwenda kuwakamata wauzaji na madawa yao ambayo badala ya kutumika kama kizibiti cha wauzaji mahakamani, huwapa watumiaji waliothirika kwa kukosa madawa.
Alisema, ugonjwa wa mateja unaosababishwa na kukosa madawa ya kulevya, unaojulikana kama alosto, ni mbaya mno na husababisha kero kubwa kwa watuhumiwa wengine waliopo mahabusu ambao siyo watumiaji.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, ACP Wilibroad Mtafungwa, alisema kuwa nyakati alipokuwa Kamanda wa Polisi Wilaya (OCD), Kinondoni, alishuhudia kadhia ya mateja kuchafua mahabusu kutokana na kuzidiwa na alosto.
“Wakishazidiwa na ugonjwa wao unaweza kukuta mahabusu imejaa kinyesi, maana wanatokwa na haja bila ya wao kujitambua. Hapo utaona ni usumbufu kiasi gani kwa watu ambao siyo watumiaji, wanaokuwa mahabusu pamoja na mateja,” alisema Mtafungwa.
Alichokisema Mtafungwa, kipo sawa na kilichoelezwa na wakuu wa vituo kadhaa jijini Dar es Salaam ambao walizungumza na Jambo Leo kwa ombi la kutotajwa gazetini kwa sababu wao kwa nafasi zao hawaruhusiwi kuwa wasemaji wa jeshi.
“Ukiwafungia mahabusu mateja, jiandae kusafisha kinyesi, wale watu wakishaharibika, kuwaweka muda mrefu bila kutumia ulevi wao ni kuzidi kuwaumiza,” alisema mkuu wa kituo kimoja cha Mkoa wa Kipolisi, Ilala, Kanda Maalum ya Dar es Salaam.
Mwenzake wa Mkoa wa Kipolisi, Temeke, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, alisema kuwa suala la kuwasaidia kupata madawa ya kulevya mateja, halina maana ya kuwaunga mkono kwa uteja wao, ispokuwa ni kuwanusuru na kifo cha haraka.
“Wewe mwenyewe ukiwaona wanapokuwa kwenye alosto utaogopa, utaona wanakufa, sasa kama binadamu unafanyaje? Kuweka msimamo wa kukataa kuwapa madawa yao ni kuharakisha kifo chao,” alisema mkuu huyo wa kituo.
Akaongeza: “Afadhali siku hizi tuna utaratibu mzuri wa kuwapeleka mateja kwenye rehab (kliniki za kuwaponya mateja), huko angalau kuna wataalam ambao huwasaidia kupona taratibu.”
DAKTARI WA POLISI AELEZA MSAADA WAO
Ndani ya Jeshi la Polisi Tanzania, vipo vituo kadhaa vina hospitali za polisi na kwa mujibu wa uchunguzi wetu, wapo mateja kutokana na hali zao kuwa mbaya hupelekwa kwenye vituo hivyo kwa matibabu.
Mmoja wa madaktari katika hospitali za polisi, naye kwa sharti la kutotajwa jina gazetini, alisema kuwa wakati mwingine inakuwa vigumu kutambua kama mtu anayepelekwa kwa ajili ya matibabu anakuwa anasumbuliwa na alosto au maradhi ya kawaida.
“Anaweza kuletwa mtu ambaye anakuwa na homa kali sana, vilevile analalamika anasikia maumivu makali. Ukimwangalia ni kama ana malaria, typhoid au amiba. Unaweza kudhani labda anayo matatizo pia kwenye njia ya mkojo,” alisema daktari huyo.
Aliendelea kusema: “Tukishampima, matokeo ya vipimo yanakuwa hayana uwiano na hali yake. Ukikaa vizuri na mgonjwa anakwambia ukweli kuwa anasumbuliwa na alosto. Hali ikishakuwa hivyo, tunakuwa hatuna namna zaidi ya kumsaidia.
“Sisi kwa upande wetu humpa dawa ya usingizi, mara nyingi ni valium (dawa ya usingizi). Akishalala na kuamka anakuwa na nafuu kiasi. Hawezi kulalamika yale maumivu kama mwanzoni, ingawa nguvu ya valium ikiisha malalamiko yake hurejea palepale.”
Alizidi kufafanua kuwa pale inapotokea mgonjwa anaonesha dalili zote kuwa tayari ni mwathirika wa madawa ya kulevya, madaktari huwa hawajisumbui, kwani humpa valium kwa haraka ili apate usingizi na kumpa nafuu ya maumivu yake.
“Alishawahi kuletwa kijana kimoja kwa macho ya kawaida huwezi kudhani kama ni mwathirika. Alikuwa bado anaonesha ana afya, kwa kifupi alikuwa hajaariwa sana na madawa ya kulevya.
“Yule kijana alikamatwa kwenye oparesheni za kipolisi za kukamata vibaka. Alipofikishwa kituoni baada ya kama saa 12 alianza kulalamika maumivu. Alitolewa mahabusu kuletwa hospitalini kwetu akipiga kelele,” alisema dokta huyo. “Tulidhani mgonjwa wa kawaida maana hakuonesha kama ni teja.
“Nilipozungumza naye pembeni alikiri anasumbuliwa na alosto, ikabidi palepale nimpe valium. Na kwa kawaida nikishampa valium, namweleza mpelelezi wa kesi yake kuhusu hali ya mgonjwa wake ili kuangalia namna bora ya kuendelea.”
Kuhusu askari kuwapa mateja unga ili kuwasaidia, alisema: “Nasikia kitu kama hicho lakini siwezi kukitolea ushahidi kwa sababu sijawahi kushuhudia moja kwa moja. Ila sisi wote ni askari, sema tu nipo upande wa afya, tunazungumza na kupeana michapo ya hapa na pale, mambo kama hayo yanasemwa kuwa yapo.”
MAKAMANDA WA DAR ES SALAAM WAZUNGUMZA
Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi, Temeke, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, ACP Andrew Satta alisema kuwa ni ukweli kuwa watumiaji wa madawa ya kulevya huchafua mahabusu wanapopatwa na hali ya ukosefu wa madawa ya kulevya kwa sababu ya kushikiliwa na polisi.
Alisema: “Wanapochafua tunasafisha. Unajua haya mambo ni vigumu kuyaelezea sisi kwa sababu yapo kitaalamu zaidi. Madaktari wanaweza kusema ni kwa nini wanakuwa hivyo, ila upande wetu sisi wanapochafua tunasafisha.
“Polisi tunakamata watu wa aina mbalimbali. Mfano vichaa, unakuta mtu amejitapakaza kinyesi mwili mzima au amejisaidia na kutapakaza kinyesi mahabusu yote. Sisi hapo tunachofanya ni kusafisha tu mahabusu.”
Kuhusu kuwasaidia watumiaji wa madawa ya kulevya kupata madawa yao ili wapate nafuu, alisema: “Sisi kwanza kama polisi huwa hatujui hayo madawa yanauzwa wapi, kwa hiyo inakuwa vigumu kuwatafutia. Kitu kama hicho hakipo.”
Majibu ya ACP Satta, yalishabihiana na yale ya Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi, Ilala, Dar es Salaam, SACP Lucas Mkondya, aliyesema kuwa mahabusu husafishwa ila kuwasaidia mateja kupata madawa ya kulevya ni jambo lisilowezekana.
“Sisi ndiyo tunakamata wauzaji na watumiaji wa madawa ya kulevya, sasa inawezekana vipi tena sisi wenyewe ndiyo twende tukawasaidie watumiaji kutumia?
“Ni kweli kwamba wale watu wanapokosa madawa yao hupatwa na hali fulani hivi mbaya, tena wakati mwingine unaweza kudhani anakaribia kufa, lakini ile hali ni sumu na baada ya muda huwa inaondoka. Kitu ambacho huwa tunafanya, wanapozidiwa huwa tunawapeleka hospitali,” alisema SACP Mkondya.
Upande wa Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi, Kinondoni, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, ACP Christopher Fume alisema kuwa kuwatafutia madawa ya kulevya mateja ni jambo ambalo halina ukweli.
“Yapo masuala umesema kuhusu hali zao jinsi zinavyokuwa mbaya, unajua kwa nafasi yangu nakuwa sishughuliki moja kwa moja na hao mateja, kuweza kuona wanapokuwa na alosto inakuwaje. Hayo mambo ya kuhusu mahabusu nitakuunganisha na mkuu wa kituo aseme inavyokuwa,” alisema ACP Fume.
Fume, alimwahidi mwandishi wetu kumpa namba ya Mkuu wa Kituo cha Oysterbay, yalipo makao makuu ya Mkoa wa Kipolisi, Kinondoni, lakini hakuweza kutimiza ahadi hiyo.
MATEJA WATOA USHUHUDA
Hemedi Jacha, maarufu kama Ngololo, mkazi wa Kinondoni, Dar es Salaam, aliliambia Jambo Leo kuwa yeye binafsi amewahi kusaidiwa kupata unga pale alipokuwa amezidiwa. Jina la kituo limehidhiwa kiusalama.
Alisema, aliwekwa siku mbili mahabusu ndipo hali yake ilipokuwa mbaya kupita kiasi na kupoteza fahamu.
“Kumbe wakati sina fahamu polisi walinisaidia kubembea (kutumia madawa ya kulevya). Kiukweli wale masoja (askari) niliwaona waungwana sana kwa sababu pengine ningekufa,” alisema.
Alieleza kuwa hata baadhi ya mateja wenzake waliwahi kukamatwa na kusaidiwa kupata unga baada ya kuzidiwa na alosto.
“Unajua ukiwa na alosto, mtu ambaye anaweza kuacha kukusaidia unga ni katili sana, ni kama kunusa kifo,” alisema Ngololo. “Mimi nimewahi kupewa ngada (unga), na nilipopata nafuu nilipelekwa mahakamani lakini baadaye niliachiwa kwa dhamana, na sasa hivi napeta mitaani.”
Mtumiaji mwingine James Nubi, alisema kuwa wamewahi kusomwa na polisi pamoja na mateja wenzake kwenye maskani yao ya Detroit, Kijitonyama, Dar es Salaam.
“Tulipokamatwa tulizidiwa sana, baadaye ilibidi tutafutiwe madude (unga) ndiyo tukaweza kurejea kwenye usawa wetu. Ni ukweli kuwa mahabusu ilichafuka, si unajua tena mambo ya alosto?” alisema Nundu kwa mtindo wa kuhoji. Jina la kituo walichowekwa limehifadhiwa.
Kwa upande wa hali wanayojisikia wanapopatwa na alosto, Nundu alisema kuwa hupatwa na maumivu makali mwili mzima na wakati mwingine huchemka mwili mithili ya mtu mwenye homa kali.
Alisema: “Mimi natumia, nashindwa tu kuacha. Nasikia kuna kliniki, nitajitahidi kwenda ili nione nawezaje kupona. Ushauri wangu kwa wale ambao hawajawahi  kutumia wasithubutu kabisa, maana ni hatari.
“Kuna wakati mtu unajisikia kama vile upo kuzimu, unajiona kabisa upo karibu na kifo. Ukishakuwa mteja unajiona haupo sawa na binadamu wengine wa kawaida. Unakuwa katikati ya binadamu na mnyama.”
VITUO VINGI WAOGOPA KUKAMATA MATEJA
Uchunguzi wa Jambo Leo umepata majibu kuwa vituo vingi vya polisi hukwepa kukamata mateja kwa sababu ya kuhofia usumbufu wa kuchafua mahabusu na kuwatafutia tiba wanapokuwa na alosto.
Mkuu wa mmoja wa kituo kidogo (post), ndani ya Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, alisema: “Hakuna mtu ambaye anataka usumbufu wa mateja, wale watu ni hatari sana. Mimi nimejionea mwenyewe.
“Tukiwakamata basi ujue kuna kosa la moja kwa moja kumhusu teja husika lakini misako ya kuwalundika mahabusu hapana. Usumbufu ni mkubwa mno wanapokuwa na alosto. Siyo kwetu tu hapa, vituo vingi pia wanawakwepa.”
Katika kueleza uzoefu wake kuhusu mateja, mkuu huyo wa kituo (jina limehifadhiwa), alisema kuwa ni watu wenye vitendo vingi vya ajabu.
Mkuu huyo wa kituo alitoa simulizi ya jinsi ambavyo walikutana na tena msumbufu aliyefanya uhalifu nyumbani kwa mtoto wa aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) nchini, Said Mwema.
“Yule teja alipoiba nyumbani kwa mtoto wa IGP Mwema, alipoona anakaribiwa kukamatwa, alijisaidia kisha akajipaka kinyesi mwili mzima ili asikamatwe. Tulipomkamata na kumuweka kwenye gari, alijisaidia tena na kuchafua gari lote,” alisema mkuu huyo wa kituo.
Akaongeza: “Hayo mambo kwa kweli ni usumbufu mkubwa. Na ndiyo sababu vituo vingi tunakwepa kuwakamata mateja, labda inapotokea tunawachukua na kuwapeleka moja kwa moja kwenye kliniki zao, vinginevyo unaweza kujikuta ni mtumwa, awachafulie chumba cha mahabusu, na ulazimike kumtafutia dawa ili kumsaidia apone.”
    
     
Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment