Na Luqman
Maloto
MASIKITIKO
yapo, mshangao unakuwepo na kuvunjika mbavu nako kupo. Zanzibar ya tangu
kufutwa kwa matokeo ya Uchaguzi Mkuu 2015 kisha kuahirishwa kabla ya kuitishwa
wa marudio ni mazingaombwe tupu.
Kwanza vuta
subira kidogo nikwambie Zanzibar ni pacha na nchi gani. Kwa kinachotokea sasa
kuelekea uchaguzi wa marudio Machi 20, mwaka huu na yale yaliyojiri kabla,
utadhani Zanzibar ina unasaba na Haiti. Ni kama mapacha!
Ingekuwa na
mataifa yanapimwa undugu kwa kutumia teknolojia ya ugunduzi wa vinasaba (DNA),
basi tungeziingiza Zanzibar na Haiti maabara tupate majibu. Tatizo nchi
hazipimwi kama mwanamuziki Diamond Platnumz na mwanaye Tiffah. Nimechomekea!
Undugu wa
Zanzibar na Haiti; Kwanza zote zilifanya Uchaguzi Mkuu Oktoba 25, 2015 lakini
hazikuweza kupata rais.
Tofauti yao;
Zanzibar, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec), Jecha Salim Jecha,
alifuta matokeo kwa maelezo kuwa uchaguzi ulikuwa na kasoro nyingi.
Haiti,
uchaguzi ulifanyika lakini matokeo ya jumla hayakufanikisha kumpata rais kwa
sababu hakuna aliyepata kura zaidi ya asilimia 50. Hivyo basi, wagombea wawili
wa juu, Jovenel Moise aliyepata asilimia 32 na Jude Celestin asilimia 25
walipaswa kurudia uchaguzi (runoff election).
Zanzibar,
Dk. Ali Mohamed Shein (CCM) alikuwa anatetea kiti chake, lakini Haiti, rais
wake, Michel Martelly hakuwa mgombea, baada ya kuongoza taifa hilo tangu mwaka
2011, hivyo kuwa na kikomo cha kikatiba lakini anampigania Moise kushinda kiti
hicho.
Zanzibar na
Haiti, kote wapinzani wamegoma kurejea kwenye uchaguzi wa marudio, japo sababu
ni tofauti. Zanzibar, mgombea wa Cuf, Seif Sharif Hamad alitaka atangazwe kwa
kuwa alishinda. Haiti, Celestin alilalamika kuwa atachezewa rafu.
Haiti
uchaguzi wa marudio ulipangwa Desemba 27, 2015 ukaahirishwa, ukatangazwa
kufanyika Januari 17, mwaka huu, ukapigwa tena kalenda mpaka Januari 24, mwaka
huu, Celestin akasisitiza kutoshiriki.
Wachambuzi
walitoa uelekeo wa uchaguzi kwenda kufanyika kwa ushiriki wa mgombea mmoja
yaani Moise. Hata hivyo, kelele zilipokuwa nyingi, Februari 7, mwaka huu,
seneti (bunge) ilimuweka kando Martelly na kumteua rais wa mpito, Jocelerme
Privert ambaye ni Rais wa Seneti, Jamhuri ya Haiti.
Sasa
uchaguzi wa marudio (runoff) wa Hait umepangwa kufanyika Aprili 24, mwaka huu.
Itakuwa ni ama Moise na chama chake cha PHTK na Celestin wa LAPEH.
Zanzibar,
baada ya matokeo kufutwa, ilifuatwa ile hali ya “nitangazeni… turudie.” Mara
tukashuhudia tukio la kiungwana mno, Seif na Shein kwa kushirikisha pande zao,
walikutana kufanya mashauriano.
Mara safari
za Ikulu kumuona Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe
Magufuli zikachukua nafasi. Alianza Seif, akafuata Shein, lugha ikawa:
“Tunaendelea vizuri na mazungumzo.”
Upepo
ulibadilika siku Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Seif Ali Iddi, alipokwenda
Ikulu, Magogoni kumwambia Dk. Magufuli: “Wazanzibar wanangoja uchaguzi kwa
hamu. Amani imetamalaki.”
Seif na Cuf
wakasisitiza kutoshiriki. Baada ya kauli ya Iddi, Jecha akatangaza uchaguzi Machi
20, mwaka huu na akasisitiza hakuna mgombea kujitoa.
Dk. Magufuli
akaambiwa simamisha uchaguzi, maridhiano yachukue nafasi. Siku ikawa nzuri na
jua lake, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Jaji Damian Lubuva,
akamtembelea Magufuli, walizungumza pembeni.
Kisha Lubuva
mbele ya waandishi wa habari akasema: “Nilikwenda kumwabia Rais Magufuli sisi
ni tume huru na hatupendelei. Hata Zanzibar watu wanasema Magufuli aingilie
kati, Zec ni tume huru, Rais hawezi kuiingilia.”
Bila shaka
Dk. Magufuli alipumua, maana baada maneno hayo ya Lubuva, naye aliitisha
mkutano na wazee wa Dar es Salaam, akasema: “Zec ni tume huru, siwezi
kuiingilia.”
Hebu jiulize
kama mimi; Ikiwa ni kweli Zec ni huru na haiingiliwi, iweje Jecha hakutangaza
uchaguzi wa marudio mpaka mazungumzo ya Seif na Shein yalipokwama?
Ni kwa nini
Jecha alitangaza uchaguzi wa marudio muda mfupi tu baada ya Iddi kuzungumza na
Dk. Magufuli kuwa Wazanzibar wanajiandaa kwa uchaguzi na kwamba amani ni tele
visiwani?
Ni sababu
gani uchaguzi wa marudio ulichelewa kutoka Oktoba 25, 2015 mpaka Machi 20,
mwaka huu? Yaani miezi mitano kasoro siku siku tano (siku 147).
NGOJA SASA
NIMSHANGAE SEIF
Awali kabisa
nimpe pole kwa kuumwa. Namuombea kwa Mungu amponye ili arejee kwenye afya yake
imara.
Mshangao
wangu ni kuwa kitendo chake cha kususa kushiriki, hakina faida kwake binafsi
wala chama, ni sawa tu na kumsusia fisi bucha au nguruwe shamba la mihogo.
Uamuzi wa
kusuia uchaguzi una faida tu ya kutaka kuhurumiwa na mataifa ya kigeni lakini
hayamjengi katika ushindani wa kisiasa.
Ni kwamba
kwa uamuzi wake, maana yake wafuasi wake wengi hawatapiga kura, hivyo Shein
atapata urahisi wa kushinda.
Itatokea
kama ya Angola mwaka 1992. Uchaguzi wa awali Eduardo dos Santos wa MPLA alipata
asilimia 49 na Jonas Savimbi wa Unita alipata asilimia 40. Hakuna aliyezidi
asilimia 50.
Uchaguzi wa
marudio ulipoistishwa Savimbi alisusa kwa madai ya kuibiwa kura. Haikumsaidia,
Santos aliendelea kuongoza, Savimbi akarudi msituni. Mwisho aliuawa.
Seif
angeweza kusimama imara kutetea ushindi wake kwa kukubali kushiriki, ila tume
ifanyiwe mabadiliko. Ahamasishe watu wake kumpigia kura, hakika kama ipo ipo
tu!
Kususa kwake
ni chereko kwa Shein ambaye akili yake yote ni kuhakikisha amani inakuwepo.
Mengine atavumilia tu. Kumsusia uchaguzi kiongozi aliye madarakani kwa nchi
zetu za Kiafrika ni sawa na kumpa urahisi wa kushinda.
JECHA
ANADUWAZA
Hafanani na
Sam Kivuitu (marehemu), yule alikuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Kenya,
aliyetangaza matokeo kinyumenyume na kusababisha damu imwagike mwaka 2008, ila
kuna hatua wanaendana.
Kivuitu
alibadili matokeo, ila Jecha alifuta matokeo. Jecha alisema uchaguzi
uliharibika, ila hakusema nani aliharibu. Kasoro hazikufafanuliwa. Mambo
yamekwenda kibubu-bubu.
Jecha
anaduwaza maana kama watu waliharibu uchaguzi ni kwa nini hawakuchukuliwa
hatua? Nani anaweza kuelewa uchaguzi uliharibika bila walioharibu kutambuliwa
na kubainishwa waziwazi?
SHEIN
ANASTAAJABISHA
Uchaguzi
utafanyika na bila shaka atashinda, maana Seif kamsusia. Swali kwake, ataongoza
kwa raha ipi akiwa na watu wengi ambao hawana furaha wala radhi na uongozi
wake?
Tunajua
wanasiasa wanapenda sana kupendwa, matokeo yaliyofutwa yameshatoa uelekeo jinsi
asivyokubalika Pemba. Hali ikiwa hivyo, halafu serikali yake inakosa uungwaji
mkono. Bila shaka atakuwa rais mwenye wakati mgumu.
Yeye ndiye
Rais wa Zanzibar, anapaswa kuwa mkali kwa rasilimali za Wazanzibar na Tanzania
kwa jumla. Kama ndivyo, ni kwa nini hajachukua hatua za kushughulikia
waliovuruga uchaguzi, maana wameharibu rasilimali za umma?
Ni kwa nini
hajamfukuza kazi Jecha kwa uzembe, baada ya tume yake kushindwa kufanya kazi
yake inavyotakiwa hadi kukaribisha uchaguzi wa marudio? Utaona kuwa uchaguzi
unakwenda kufanyika ila kwa hakika, Shein anastaajabisha.
Unaweza
kulazimisha uchaguzi na ukatawala kwa chereko zote katika mazingira ya mfumo wa
ukiritimba wa chama kimoja (one-party dominant system), Zanzibar kwa sasa ni
mlinganyo wa vyama viwili (two-party system) kati ya CCM na Cuf, na wananchi
wamegawanywa hivyo.
Hata kama
machafuko hayatatokea, lakini kundi kubwa litakuwa na kinyongo na uongozi wa
Shein. Kama hili halifikirii, kweli anastaajabisha!
Mungu
Ibariki Zanzibar, Ibariki Jamhuri ya Muungano wa Tanznaia.
Mwandishi wa makala
haya ni mwandishi wa habari, mwandishi wa vitabu, vilevile mchambuzi w masuala
ya siasa, utawala, jamii na sanaa.
0 comments :
Post a Comment