ads 728x90 B

Shida siyo Banda, tatizo wanaoongoza soka!




Luqman Maloto
Beki wa Klabu ya Simba, Abdi Banda, aliye na uwezo mkubwa wa kusimama kama kiungo mkabaji, yupo kwenye karantini! Kwamba hayupo kikosini kwa sasa akisubiri hukumu ya kocha.
Beki fundi wa Simba, Hassan Isihaka, yeye yupo kifungoni. Kosa lake ni utovu wa nidhamu. Banda na Isihaka tatizo lao ni mgogoro na kocha.
Upo pia mgogoro mkubwa kati ya uongozi wa Klabu ya Simba na beki wake wa kulia, Hassan Kessy. Na unaendelea!
NINI KOKORO?
Sasa hivi inawezekana kabisa kuutazama mgogoro wa Banda na Kocha wa Simba, Jackson Mayanja kwa upande mmoja.
Hiyo ni kama ilivyokuwa kwa Isihaka, alivyowekwa kando katika program ya kocha, baada ya kutofautiana na mwalimu huyo raia wa Uganda.
Kwamba Kessy ni mgogoro tu wa mkataba, kama ambavyo hata Haruna Niyonzima ‘Fabregas’, alivyopata kutofautiana na menejimenti yake.
Utaona kuwa angalau mgogoro wa Niyonzima na Yanga, ulimalizwa kwa Mwenyekiti wa klabu hiyo, Yusuf Manji kutangaza kumwondoa klabuni, aliyekuwa katibu mkuu, Dk. Jonas Tiboroha kwa kusababisha matatizo yaliyokuwepo.
Manji alisema kuwa Niyonzima alihujumiwa na Tiboroha. Angalau hilo liliwekwa wazi kisha aliyekutwa na hatia akawekwa kando, wakati huohuo mchezaji akarejeshwa kundini.
Hivi sasa, Kocha wa wa Stand United, Mfaransa Patrick Liewig, naye imeshaelezwa kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kutokuwepo na timu hiyo msimu ujao. Kisa haelewani na wachezaji.
Wapo viongozi wanahoji, ni kwa nini Leiwig anasababisha straika Elias Maguri asifunge tena magoli kama ilivyokuwa zamani?
Nakumbuka mwaka 2007, wakati Kelvin Yondan akicheza vizuri nafasi ya beki ya kati Simba kwa kushirikiana na mkongwe, Victor Costa ‘Nyumba’, Makamu wa Rais wa klabu hiyo, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ wakati huo akiwa mdau tu wa timu, alisema beki huyo hafai.
Kaburu kama mdau na memba wa kundi la Friends of Simba, ni mmoja kati ya wanene wa klabu hiyo, waliokuwa na michango ya kusajili wachezaji kwa niaba ya klabu.
TUWEKE MZANI SAWA
Mfano wa Kaburu, ukupe jibu moja kuelekea kuondoka kwa Yondan Simba.
Kama Kaburu alipokuwa mdau tu wa Simba alimkataa mchezaji huyo, inakuwaje baada ya kushika umakamu wa rais? Yondan aliondoka, yakafuata maigizo na hayakusaidia kitu.
Tatizo ni watu wanaoongoza soka. Wachezaji lazima wawe na utovu wa nidhamu kwa kocha kwa sababu viongozi wa timu hutaka waonekane wao ndiyo kila kitu kuliko makocha.
Kocha anaandaa kikosi, anaambiwa ampange mchezaji ambaye hayupo kwenye program ya kocha. Kesho mchezaji hawezi kuwa na nidhamu kwa kocha wake. Anajua bila kiongozi fulani, singecheza.
Ulaya kocha ndiye mwalimu, vilevile meneja wa timu. Huku kwetu Bongo kocha ni mkufunzi tu wa mazoezi.
Kwetu Bongo, kocha ujanja wake unaishia kwenye mazoezi na kuwapika kwa mbinu za mchezo lakini katika mechi, wanageuka maroboti, rimoti wanakaa nazo viongozi jukwaani.
Banda anajitetea, eti: “Kocha aliniambia nipashe niingie kucheza nikamwambia amwachie kwanza Tshabalala anaweza.”
Pamoja na makosa, bado mchezaji anajiona alikuwa sahihi. Ukifuatilia, unakuja kugundua kuwa yapo kiongozi anamjaza upepo, kichwa kinavimba.
Sir Alex Ferguson, alipokuwa meneja wa Klabu ya Manchester United, alimuuza David Beckham kwa Real Madrid, baada ya kuona mchezaji huyo anataka kumpanda kichwani.
Na kwa kawaida, uamuzi wa kocha lazima uheshimiwe. Kocha anapewa kila anachohitaji kisha anabanwa katika matokeo. Ndiyo maana Beckham na ustaa wake, jumlisha mapenzi makubwa kwa Man United aliyokuwa nayo, aliuzwa na timu iliendelea.
Hapa kwetu, kocha anaingiliwa kisha timu ikifanya vibaya kocha anatimuliwa. Shida ipo kwa wanaoongoza timu.
MAMLAKA YA KOCHA YAHESHIMIWE
Viongozi waache tabia ya kutengeneza matabaka kwa wachezaji. Wanawaharibu kuliko kuwasaidia, vilevile kusaidia soka la nchi.
Wapo wachezaji wengi walimaanishwa kutisha Ulaya lakini hawakufika popote kutokana na malezi mabaya ya viongozi.
Ni kawaida kabisa kwa mchezaji kuharibika anapotetewa katika nyakati anapoonesha vitendo vya utovu wa nidhamu.
Msingi wa malezi unakataa mtu kutetewa anapokosea. Hata kama atakuwa anaonewa, nguvu ya juu kutetea husababisha mhusika avimbe kichwa.
Yanga kama Toboroha angeonywa kisha Niyonzima akatetewa, kusingekuwa na maelewano wala nidhamu kati yao. Ndiyo maana uamuzi uliochukuliwa umekuwa wa busara mno.
Viongozi wanatakiwa kutanguliza weledi. Waache kuwavimbisha vichwa wachezaji mbele ya makocha wao.
Lazima kutambua menejimenti za klabu na kamati zao, zinahusika tu mikataba ya wachezaji na utekelezwaji wa vijazilizi vya ajira, lakini benchi la ufundi, bosi wake ni kocha, yeye ndiye mwalimu na anajua ni wakati gani mchezaji yupi anamfaa kutokana na mazingira ya mchezo.
Maisha lazima yabadilike, soka la Tanzania linapaswa kukua. Wachezaji wa Kitanzania wanastahili kukua, waende kisasa. Nafasi ya kocha itambulike. Nidhamu kwa wachezaji halipaswi kuwa suala la kuomba.
Malezi yasiyofaa ya viongozi kwa wachezaji imekuwa sababu ya wachezaji wengi kushindwa maisha ya soka nje ya Tanzania. Wanapenda kukumbatiwa na viongozi wao. Kudekezwadekezwa. Shida sana!


  
Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment