Na Luqman
Maloto
Uchaguzi umepita
ila sasa kije kipindi cha maridhiano. Mgogoro wa Cuf na CCM sababu ni uchaguzi
wa Oktoba 25, 2015, basi baada ya marudio kukamilika, upande wenye mnofu
ufungue ukurasa mpya.
Vema
kukumbusha kuwa tangu ruhusa ya mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992,
kipindi kizuri cha utawala Zanzibar kilikuwa kati ya mwaka 2010 na 2015, Dk.
Ali Mohamed Shein alipoongoza Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Hapa ni
kumaanisha kuwa Awamu Pili ya Dk. Salmin Amour mwaka 1995 mpaka 2000 na vipindi
viwili vya Dk. Amani Abeid Karume kati ya mwaka 2000 mpaka 2000 kulikuwa na
ghasia nyingi.
Afadhali awamu
ya pili ya Dk. Karume, miaka yake miwili ya mwisho, aliongoza bila kokoro baada
ya kukamilisha mazungumzo yaliyofanikisha kuandikwa kwa Katiba Mpya yenye
kuruhusu muundo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Uchaguzi wa
mwaka 2010, ndiyo pekee kokoro haikuwa kubwa baada ya nguli wa siasa za
Zanzibar, Seif Sharif Hamad wa Cuf, kukubali mapema matokeo ya kushindwa, hivyo
Shein kuongoza kwa baraka zote.
Kuna mambo
mawili vema kuyaweka wazi. La kwanza ni kwamba pamoja na Seif kukubali matokeo
kisha Serikali ya Umoja wa Kitaifa kuundwa mwaka 2010, bado minong’ono ilikuwa
mingi kwamba Shein hakushinda, isipokuwa Cuf iliridhia ushindi wake kwa
uungwana pamoja na dhamira ya kuijenga Zanzibar moja baada tofauti za muda
mrefu.
Jambo la
pili ni kukumbusha ni kuwa watu wengi walijenga kijiwe Hoteli ya Bwawani na
kupiga kelele matokeo yatangazwe. Kelele nyingi zilikuwa Seif alishinda lakini
mwenyewe alipokubali kushindwa, zogo likaondoka.
KUMBUKUMBU
NI MWALIMU
Baada ya
Uchaguzi Mkuu 2000, Cuf walikataa matokeo na kwa hivyo, walifanya uamuzi wenye
sura mbili.
Kwanza
walitangaza kuwa wabunge na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wa Cuf waliotangazwa
kuwa wameshinda, wasingehudhuria wala kushiriki vikao vya bunge na baraza kwa
sababu ya kutokukubaliana na matokeo kwa jumla.
Pili,
waliandaa maandamano ya kupinga matokeo ambayo yalipangwa kufanyika Januari 26,
2001. Ni maandamano hayo yaliyosababisha maafa ya watu, raia wa kawaida na
askari wa Jeshi la Polisi, Januari 26 na 27, 2001.
Ni kipindi
ambacho Tanzania iliingia doa la kuzalisha wakimbizi. Ipo sehemu ya Wazanzibar
ilikimbilia Kenya na Somalia kutokana na machafuko hayo.
Hata baada
ya machafuko hayo, Cuf waliendelea na msimamo wao kwa wabunge na wajumbe wao wa
Baraza la Wawakilishi kutohudhuria vikao vya bunge na baraza.
Msimamo huo
ulisababisha nguvu ya upinzani ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kupwaya, huku kwenye Baraza la Wawakilishi kukosekana kabisa.
Bungeni,
wapinzani wa vyama tofauti walijiunga na kumchagua aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la
Kigoma Mjini (Chadema), Dk. Aman Walid Kabourou kuwa Kiongozi wa Kambi ya
Upinzani.
Mgomo wa Cuf
ulifikia kikomo baada ya mwafaka kati ya chama hicho na CCM, uliosaniwa Oktoba
2001 mbele ya waliokuwa wenyeviti wa vyama hivyo, Benjamin Mkapa (CCM) na
Profesa Ibrahim Lipumba (Cuf).
Ni kwamba
mgomo wa Cuf uliisha kwa wabunge na wajumbe wao wa Baraza la Wawakilishi kuanza
kuhudhuria vikao kuanzia Januari 2002. Hata hivyo, utekelezaji wa jumla wa
mwafaka ulikwama hadi Uchaguzi Mkuu wa 2005 ambao pia matokeo ya urais
yalipingwa na Cuf.
Hali ilikuwa
tete Zanzibar baada ya Uchaguzi Mkuu 2005, na vilevile tuwe na kumbukumbu kuwa
baada ya Uchaguzi Mkuu 1995, hali haikuwa shwari, na mwaka 1997, baada ya
uchaguzi mdogo wa Jimbo la Mkunazini kuwania ujumbe wa Baraza la Wawakilishi,
mwanasiasa mkongwe Juma Duni Haji na wenzake walikamatwa kwa kosa la uhaini na
kuwekwa mahabusu mpaka mwaka 2000.
Katika
uchaguzi huo, Duni alishinda lakini hakufanya kazi yake kama mjumbe kutokana na
kesi hiyo ya uhaini.
Nimeweka
muhtasari huo wa kumbukumbu, kama mwalimu wa kukumbusha nyakati ngumu za
maelewano mabovu ya kisiasa, kupitia hapo itoshe kuonesha umuhimu wa
maridhiano.
MARIDHIANO
NI LAZIMA
Msimamo wa
Cuf ulikuwa na taswira nyoofu ni kuwa hata kama kuna kiongozi wa chama hicho
atashinda, bado hawatakubali.
Taswira
hiyohiyo na unyoofu wake ilionesha hali ya kususia uchaguzi huo hasa kwa upande
wa Cuf, hivyo CCM si maajabu kushinda kwa kishindo.
Na kwa vile
Zanzibar inatawaliwa na siasa za vyama viwili, CCM na Cuf, muundo wa Serikali
ya Umoja wa Kitaifa ambao hautashirikisha moja kati ya vyama hivyo, utakosa
vionjo stahiki. Bila uzandiki ni kuwa serikali ‘itaboa’.
Katiba ya
Zanzibar inaelekeza mtu atakayeshika nafasi ya pili awe Makamu wa Kwanza wa
Rais na chama chake kishirikiane na Chama Tawala kuunda Serikali ya Umoja wa
Kitaifa.
Hamad Rashid
Mohamed wa Chama cha ADC ameshika nafasi ya pili. Japo kura hazimpi uteuzi
kikatiba, Shein anaweza kumteua kiungwana.
Na kama
atafanya hivyo, basi ifahamike kuwa CCM na ADC kuunda Serikali ya Umoja wa
Kitaifa Zanzibar, haitakuwa serikali yenye hadhi yake, bora tu CCM ijitegemee
yenyewe katika kutawala visiwa hivyo.
CCM na Cuf
ni vyama vyenye nguvu karibu sawa Zanzibar. Na Visiwani humo, siasa za vyama
hivyo ni kama dini.
Nguvu ya
viongozi wa kisiasa Zanzibar na maneno yao ambavyo hugusa nyoyo za wafuasi wao,
ni karibu sawa na mashehe, wachungaji na mapadri wanaponena maneno ya Mungu kwa
waumini wao. Mazingatio huwa ni makubwa mno.
Siasa hizo
za Zanzibar, ndizo ambazo zinatoa picha ya ugumu wa serikali kuongoza na
kutimiza malengo yake, kwa kususiwa na upande mmoja kati ya vyama hivyo.
Hivyo basi, CCM
ambao ndiyo washindi wa uchaguzi, baada ya kutangazwa na Mwenyekiti wa Tume ya
Uchaguzi Zanzibar (Zec), Jecha Salim Jecha, hawapaswi kushangilia sana,
watatakiwa kurudi mezani na Cuf.
Maridhiano
ni deni la Wazanzibar kwa CCM na Cuf. Wazanzibar wanatakiwa kutengenezewa daraja
la ushirikiano. Vyama hivyo vinaweza kujenga au kubomoa daraja.
Ikiwa CCM na
Cuf watakaa mezani, watakuwa wamejenga daraja la ushirikiano kwa wananchi,
mgomo ukiendelea chuki itakuwa kubwa na hakutakuwa na ushirikiano.
Machafuko
ambayo yamekuwa yakiendelea kuripotiwa. Wapo watu wanaoitwa mazombi wamekuwa
wakifanya matukio ya kihalifu ambayo yanahusishwa na siasa za chuki visiwani
humo.
Hali na
matukio hayo, ni kuonesha kuwa suala la maridhiano Zanzibar halina hiari. CCM
na Cuf wanapaswa kutambua kuwa Zanzibar ni kubwa na muhimu kuliko vyama vyao.
Wazanzibar watangulizwe mbele kabla ya matakwa ya kisiasa.
NINI
KIFANYIKE?
Baada ya
matokeo ya Uchaguzi Mkuu 2015 kufutwa Zanzibar, Seif na Shein walifanya mkutano
wa kutafuta mwafaka. Suluhu ilikuwa ngumu kupatikana kwa sababu kila mmoja
alishika lake.
Seif
alisisitiza kuwa alishinda uchaguzi, hivyo atangazwe, wakati Shein alishikilia
msimamo wa Zec kuwa uchaguzi urudiwe. Ilitakiwa mmoja akubali kushindwa, jambo
ambalo halikuwa rahisi.
Ni afadhali
kila mmoja angekuwa anasema ameshinda, hivyo suluhu ilikuwa kuwafanya wote
wakose kwa kufuta matokeo na kuitisha uchaguzi wa marudio. Tatizo mvutano wao
ulikuwa mtego mkali, na wa kukubali kushindwa hakuonekana.
CCM kama
washindi, wanatakiwa kutambua hali halisi, hivyo kuwaangukia Cuf ili
washirikiane kuiongoza Zanzibar.
Cuf
wanaihitaji Zanzibar yao ikiwa moja. Msimamo wao wa sasa ni kinyongo cha kuona
hawatendewi haki na wenye mpini.
Baada ya
uchaguzi, na kama wataitwa mezani ili washirikiane kuijenga Zanzibar yao, hapo
watakuwa ni ama wakubali au wakatae.
Ipo wazi
kuwa tatizo la Zanzibar lipo kwenye nafasi mbili za juu, ile ya Rais na Makamu
wa Kwanza wa Rais, nani awe mkuu na yupi bosi namba mbili.
Na kwa vile Shein
alishatangazwa na kula kiapo, hapo bila shaka nafasi itakuwa imejaa. Hata
hivyo, deni lake ni kuhakikisha Seif anashirikiana naye.
Shein
akifanikiwa kumshawishi Seif akubali kuwa bosi namba mbili, yaani Makamu wa
Kwanza wa Rais, maana yake kila kitu kitakuwa kimemalizika. Nafasi za chini
zitajitengeneza zenyewe.
Natambua
ugumu wa Seif na Cuf kukubali kushawishika, lakini naiona zaidi Zanzibar ikiwa
ngumu kuliko nyakati zote kama Shein atashinda na kula kiapo kisha kuongoza
serikali bila baraka za Cuf na Seif.
Ugumu huo wa
Zanzibar ni deni kubwa kwa Shein. Hivyo basi, baada ya uzuri wa kutangazwa
mshindi, sasa atambue umuhimu wa Zanzibar kubaki moja, hivyo ajishushe na kumshawishi
Seif mpaka akubali ili salama ya kweli ipatikane.
Ikumbukwe;
Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliundwa kwa msuli mkubwa, haipendezi ikabezwa na
kuvunjwa kirahisirahisi.
Serikali ya
Umoja wa Kitaifa ilifanikishwa kwa fedha nyingi. Mabadiliko ya Katiba, Kura ya
Maoni, vikao vya maridhiano bila kusahau safari za nje na mialiko ya wataalamu,
kupata ushauri wa namna bora ya kumaliza misuguano na kuibakiza Zanzibar kuwa
moja.
Tumesahau?
Haiwezekani kukawa na usahaulifu wa kiwango hicho. Hatupaswi kusahau.
Nisisitize;
Bila maridhiano, naiona Zanzibar ngumu kama ile ya Dk. Salmin, yenye uhasama wa
wazi. Naiona Zanzibar tata kama ile ya muhula wa kwanza wa utawala Dk. Karume.
Mungu
Ibariki Zanzibar, Mungu Ibariki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
0 comments :
Post a Comment