ads 728x90 B

Soko la muziki halina huruma hata kidogo!




Na Luqman Maloto
Mfalme wa Temeke, Juma Kassim Kiroboto ‘Sir Nature’, ameomba mpambano na janki pedeshee wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul Juma ‘Diamond Platnumz’.
Nilipoona habari hizi nilicheka, nikakumbuka mbali. Kweli muziki ni katili na soko lake halina huruma hata kidogo.
Diamond amekuwa mkubwa mno kimuziki, siyo tu Bongo, bali Afrika yote. Wakati dogo huyo kibopa wa Bongo wa Fleva akinawiri kimuziki, ndiyo kipindi ambacho Mfalme Nature ‘Kibla’ alikuwa anamalizia enzi yake.
Kwa kifupi Nature alipishana na Diamond. Wakati Baba Zari, samahani, namaanisha Baba Tiffah Dangote, alipokuwa bize akiwasha taa zake za kumng’arisha kimuziki, ndipo Nature alipozima taa zake za mng’aro wake.
Nature yule ambaye alipendwa na mashabiki wa Bongo Fleva kuliko chakula, leo hayupo kwenye mzunguko wake wa soko. Wakati huohuo, Diamond ndiye mbabe wa soko lenyewe. Huu muziki hauna mfalme wa kudumu!
Akumbukwe Nature wa Ugali. Ukumbi wa Diamond Jubilee, pale Upanga, haukutosha mwaka 2003.
Nature wa Hili Game na Sitaki Demu. Nature wa Kighetto Ghetto na Inaniuma Sana. Nature wa Hakuna Kulala na Sonia. Huyu mtu alifanya ‘mabalaa’ ya uhakika kwenye muziki wa Tanzania.
Alitikisa kwenye rap, alipoimba Kwaito watu walimwelewa. Nature alikuwa juu kabisa ya kilele cha muziki.
Kipindi ambacho Bongo Fleva uliitwa muziki wenye utamu wa Big G, Nature alivuka mwaka mmoja mpaka mwingine akiwa juu kabisa. Nature apewe heshima yake.
Nature na ubabe wake ule wa kimuziki, leo hii anatamani kufanya mchuano wa jukwaani na Diamond. Tena amesema: “Hakuna mwanamuziki mwingine anamuweza Diamond jukwaani kasoro mimi.”
Soko la muziki halina huruma! Ni Nature mwaka 2006 alivuka mipaka na kushiriki Tuzo za MTV Ulaya (MTV Europe Music Awards), akishindania Tuzo ya Mwanamuziki Bora Afrika (Best African Act).
Katika tuzo hizo, Nature alishindana na kundi la Freshlyground (Afrika Kusini), Nameless (Kenya), P-Square (Nigeria) na Anselmo Ralph (Angola). Kundi la Freshlyground ndilo lililonyakua tuzo hiyo.
Kituko cha tuzo hiyo ni kuwa Nature hakwenda kuhudhuria tuzo hizo, zilizofanyika kwenye Ukumbi wa Bella Center, Copenhagen, Denmark. Nature kwa kutokuhudhuria kwake, alimlaumu aliyekuwa meneja wake, Said Fella ‘Mkubwa’ kwa kutomfanikishia safari!
Soko halina huruma! Godfrey Tumaini ‘Dudubaya’ na Nice Lucas Mkenda ‘Mr. Nice’, walitikisa vilivyo na bifu lao. Walipogombana ikawa gumzo nchi nzima.
Mwaka jana, Dudubaya na Nice walikutana na kutangaza kumaliza bifu kisha wakafanya maonesho kadhaa ya muziki pamoja na hakuna mtu aliyeshtuka. Ni kipindi ambacho soko lao lilikuwa limeshahama.
Hakuwa Dudubaya wa Mwanangu Huna Nidhamu, Dege la Jeshi, Tupa Mawe, Nakupenda Tu, Mpenzi na nyinginezo.
Mr. Nice huyo hakuwa yule wa Kidali Po, King’asti na nyingine zilizotamba. Maisha yameshabadilika kwa kasi kubwa.
Bado huamini kuwa soko la muziki halina huruma? Hapo jiulize yupo wapi Joslin na MB Dog? Amekwenda wapi Z Anto? 
Maisha ya kimuziki mbona yamekuwa siyo rafiki tena kwa Matonya? Wakati wake ilikuwa ni vigumu kumpata kwa shoo, maana alijaza kila tarehe kwa mwaka.
SIYO BONGO TU
Ngoja nikukumbushe; DMX aliposhika usukukani wa soko la rap Marekani, aliuza platinum nyingi mno.
Ghafla akaibuka Ja Rule, hapo ndipo ufalme wa DMX ukapotea. Soko la rap duniani likawa halifunui kinywa upande wake. Sauti zege, tungo tamu za kimalovee. Ja Rule bwana!
Soko halina huruma! Alipoibuka 50 Cent ndiyo ikawa mwanzo wa kupotea Ja Rule. Hata hivyo, 50 Cent wa leo, siyo yule! Naye biashara siyo asali upande wake.
SHULE NDANI YAKE
Hakuna jambo zuri kama mwanamuziki kutambua soko la muziki linapomuelekea.
Kinachotakiwa kwa mwanamuziki ni kuhakikisha anakuwa na wakati mzuri wa kupanua soko lake.
Vema kutambua kuwa itafika wakati mwanamuziki mwenye soko leo, kesho hatakuwa na soko hilo.
Haiwezekani wewe ukawa mwanamuziki mwenye kuuza kila siku. Upo wakati utafanya kazi unayoiona nzuri na hutauza.
Kumbuka Michael Jackson ‘The Jacko’ ambaye unaweza kumwita Mfalme MJ, aliuza nakala milioni 100 kwa albamu moja. Itambue albamu ya Thriller na maajabu yake.
Mwaka 2001, Jacko alitoa albamu yenye maandalizi makubwa inayoitwa Invincible. Akatanguliza singo babkubwa You Rock My World. Kilichotokea ni kuwa aliuza nakala milioni 10 tu.
Ni ukweli kuwa nakala milioni 10 ni nyingi kwa biashara lakini siyo kwa hadhi ya Jacko. Ni kwamba alidhani zilikuwa zama zake lakini hazikuwa zile.
Tupac Shakur tangu alipotoa albamu yake ya kwanza 2pacalyps mwaka 1991, aliweka rekodi ya kuuza platinum tu.
Aliweka rekodi ya kuuza platinum mpaka mara 10 (diamond), na kuweka rekodi ya kuwa mwanamuziki wa Hip Hop wa kwanza kufikia mauzo hayo.
Alipokufa, mauzo yake yalipaa zaidi na zaidi. Kila albamu yake aliyotoka ilipiga platinum. Mwaka 2006, ilipotoka albamu ya Pac’s Life, ilidorora kabisa na mauzo yake hayakufika hadhi ya dhahabu (nakala 500,000). Soko lilishahama!
Ifahamike kuwa utafika muda Diamond hatakuwa anauza kama sasa, kama ambavyo juhudi za Q Chiller kurejea sokoni zinavyogonga ukuta.
Mwanamuziki heshimu wakati wako. Ukiwa kwenye wakati mzuri wa kuuza, jitahidi kuwekeza, upo wakati utafika hutaweza kuuza. Kitakachokufaa ni uwekezaji wako.

  




Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment