ads 728x90 B

UKIWA MZURI UTAMJUA MZURI




KUNA siku niliombwa na waandishi wenzangu wa habari, tukutane tuweze kubadilishana mawazo kuhusu ujenzi wa maandishi yenye mvuto na yasiyochosha katika uandishi wetu wa kila siku.
Tulipokutana, jambo la kwanza ambalo niliwapa ni kuwa inahitaji mtu binafsi kwa utashi wake, awe mzuri ndipo atamjua mzuri.
Kwamba mwandishi mzuri ni lazima awe mpenda kusoma, tena usomi wa kidadisi. Ni katika kusoma ndipo itakuwa rahisi kuyajua maandishi mazuri pamoja na mwandishi mzuri.
Na ukishayajua maandishi mazuri na mwandishi mzuri, ndipo utaweza kuandika vizuri, maana taratibu utajifunza njia mbalimbali za uandishi wenye ladha tamu kwa kuiba maarifa ya uliowasoma na kuongezea ubunifu wako kisha kuunda njia zako.
Nimeshakutana na baadhi ya waandishi wa habari, wananiambia: “Najitahidi sana lakini sifikii kiwango cha kuitwa mwandishi mzuri.”
Jawabu langu huendana na maswali mawili: “Je, unayajua maandishi mazuri? Je, unawajua waandishi wazuri?” Siku majibu hayo yakiwa “ndiyo”, basi na wewe ni mwandishi mzuri na utafikia daraja la kuitwa bora.
Na huo ndiyo hasa mfumo wa maisha ya kila siku. Unahitaji kuwa muungwana ili uwajue waungwana wapoje.
Haiwezekani wewe uwe muongo halafu umtambue mkweli. Zipo njia ambazo mnapishana, kwa hiyo hamtaweza kwenda sambamba hata siku moja.
Ni kwa sababu wewe umezoea kuongopa, ndivyo utaona na maneno ya ukweli kutoka kwa mkweli ni uongo mtupu. Lazima uyatie kasoro, maana umezoea kusema uongo, wewe unaendana na waongo wenzio.
Ndoa nyingi zipo kwenye misukosuko, mume na mke wanaparurana. Wananyoosheana vidole, kila mmoja anamuona mwenzake ni tatizo.
Niliwahi kukutana na mke na mume wenye migogoro. Tulipozungumza pamoja kila mmoja alikuwa anatetea upande wake.
Nikaomba kuzungumza na mmoja-mmoja, na kila mmoja nilimwambia: “Hutafikia pointi ya kutambua uzuri wa mwenzako mpaka wewe mwenyewe uwe mzuri. Utatambua kwamba mwenzi wako ni bora kama wewe mwenyewe utabadilika na kuwa bora. Badilika na uwe bora halafu ufanyie kazi malalamiko ya mwenzio ili asiendelee kulalamika.”
 Nilipompa maneno hayo kila mmoja, baadaye niliwaita wote nikawaambia wakafuate yale ambayo niliwaambia. Baada ya mwezi mmoja, walinipigia simu, mke akaniambia: “Mwalimu asante sana, nilichelewa kufahamu kuwa nina mume bora kuliko wanaume wote chini ya jua.”
Kisha mume naye akaniambia: “Nilikuwa nimeshajidanganya kuwa nilikosea kuchagua na kuoa, nikadhani wapo wanawake wazuri zaidi. Tangu tumetoka kwako mwezi uliopita, na kufanyia kazi ushauri ulionipa, nimeweza kuona mabadiliko makubwa ya kimaisha kutoka kwangu binafsi na mke wangu.
“Na sasa nathubutu kusema nimekuwa mwanaume mwenye bahati kubwa kumpata na kummiliki mke wangu. Upendo wangu kwake umeongezeka, amekuwa mwanamke bora kupata kumshuhudia. Sidhani yupo mwingine wa kumfikia. Nakushukuru, hakika huyu ndiye mke wangu chaguo nililoelekezwa na Mungu.”
 Pokea ukweli huo kwamba ndoa bora na yenye furaha hujengwa na watu wawili wazuri. Usikimbilie kusema mwenzangu hafai, jiulize wewe mwenyewe kwanza, je, unafaa?
Upo kazini na unagombana na wenzako kila leo, unasema hawakuheshimu, wanakubagua. Jiulize, je, wewe unayo heshima kwa wenzako na huwabagui?
Ni rahisi mno kwa mtu asiye na heshima kwa wenzake kuona haheshimiwi. Kama ilivyo kwa mbaguzi, ni mwepesi kunyoosha kidole kuwa anabaguliwa.
Ndoa nyingi zinapata misukosuko kwa sababu roho wa kukosa uaminifu ndiye ametawala. Kila mmoja anakuwa anamhisi mwenzake anachepuka.
Sikiliza ndugu yangu; Unahitaji kuwa mwaminifu ndipo utabaini kuwa mwenzako ni mtu mwaminifu kuliko wote duniani.
Ukosefu wa uaminifu ni roho mchafu. Akishakutawala, nawe utapoteza imani kwa mwenzako. Hata awe mtulivu vipi, bado utamtilia shaka kwenye mawasiliano yake. Utanyata upekenyue simu yake, hata usipopata unachohitaji, utajiambia: “Amefuta, ipo siku nitamkamata.”
Na siku zote utamuona mwenzako ni tatizo. Lakini siku ukiamua kumfukuza roho wa kukosa uaminifu kwenye mzunguko wa maisha yako. Ukawa mwaminifu na mwenye kujiamini, utajikuta unakuwa na imani kubwa kwa mwenzako.
Ukimpigia simu asipopokea, hutasema yupo maeneo mabaya, utaona ni bahati mbaya, kwamba labda simu ipo mbali au amebanwa na kazi. Uaminifu lazima uanze na wewe.
Wapo watu wengi waliwapa akili ya usaliti wenzi wao kutokana na kuwatuhumu. Kila siku anatuhumiwa, anajiuliza hapa na uaminifu wangu siaminiwi sasa uaminifu wa nini? Anaamua kuchepuka, mwisho anakuwa mtaalamu wa kucheza nje cup.
Aliyekwambia nani kama inaweza kutokea mwizi akamwamini mtu? Uwe mwaminifu kiasi gani lakini atakuona tu unamwibia.
Bosi kila siku anafukuza wafanyakazi kwa sababu anaamini wanamuibia. Sababu ni kuwa yeye mwenyewe ni mwizi, sasa atawezaje kumwamini mtu?
Wanasiasa wengi wana hulka za kilaghai pamoja na udanganyifu, ndiyo maana nyakati za uchaguzi duniani kote lazima kutokee malalamiko ya kuchezeana rafu au hata kuibiana kura. Huo ndiyo mwendo.
Unatakiwa kuwa jirani mzuri ili uwaone majirani zako ni watu bora kuishi nao. Wewe ukiwa mbinafsi, uungwana wa majirani zako unaweza kuutafsiri kama kujipendekeza kwao kwako.
Utauona ubora wa marafiki zako kama wewe mwenyewe utakuwa rafiki bora. Ukijitengeneza kirafiki daima kila mmoja atapenda kukusogelea na utaitwa mtu wa watu.
Watu wanapokuwa mbali na wewe usiseme umetengwa, jaribu kujiuliza, je, tabia yako inavuta watu au inawakimbiza? Nidhamu ya kuishi inakutaka uanze kujinyooshea kidole wewe kabla hujafanya hivyo kwa wenzako.
Nidhamu ya maisha ilimtaka Winnie Mandela kuwa mwanamke bora ndipo angeutambua utukufu wa Nelson Mandela. Ni kwa sababu hakuwa bora, hivyo hakumwelewa mwanaume bora, na matokeo yake heshima ambayo alistahili kuipata, ilikwenda kwa Graça Machel.
Ni watu wengi tu kwa kushindwa kwao kuwa watu wema, hupatwa na upofu wa kutowatambua watu wazuri na matokeo yake kupoteza fursa kubwa baadaye kama ilivyotokea kwa Winnie alivyompoteza Mandela.
James Sirleaf hakujua safari njema ya Ellen Johnson Sirleaf, matokeo yake alipomuoa hakutaka asome, alilazimisha kumfanya mama wa nyumbani na tegemezi kwake.
Sirleaf hakuwa na macho mazuri ya kuitazama kesho, kwa hiyo hakugundua kuwa Ellen ni mwanamke mkubwa mno. Wenyewe humwita tembo.
Ndiyo maana juhudi za Ellen kuitafuta kesho yake, Sirleaf aliichukulia kama kupoteza muda na kutozingatia majukumu yake ya nyumbani kama mama wa familia. Sirleaf aliamini Ellen ni golikipa tu, yaani mke mwenye kutegemea tu mfuko wa mume wake.
Ellen alipokuwa analazimisha kusoma ili kubadili maisha yake na kuyafikia malengo ya kuwa kiongozi katika Taifa la Liberia, Sirleaf aliinua mikono, akampa talaka. Alitaka Ellen awe mke mpika chakula, muosha vyombo, mpiga deki sakafu, mfua nguo na mbembeleza watoto tu.
Nini kimetokea leo, Ellen ndiye Rais wa Liberia. Na ameweka rekodi ya kuwa mwanamke wa kwanza mwafrika kuwa kiongozi mkuu wa taifa. Sirleaf hakuyaona, Ellen aliyaona.
Sirleaf alimuona Ellen msumbufu na mwanamke asiyefaa kuwa mke na mama bora. Ellen alijiona anaweza kupanda milima na kufika alipo sasa. Inahitaji macho yenye kuona vizuri ndipo mtakuwa na ushuhuda unaofanana. Siyo mmoja aone, mwingine haoni, kisha wote muwe mashahidi. Haiwezekani!
Inahitaji watu wawili wenye ndoto za kufanana ndipo itawezekana kusafiri pamoja. Kama mnapishana hamtaelewana. Ni rahisi mwenzako kukuelewa kama wewe mwenyewe ndiye utaanza kumwelewa.
Binadamu ni kama kioo, jinsi unavyotabasamu ndivyo na taswira yako kwenye kioo itakavyokuwa hivyohivyo. Na ukinuna, kioo chako kitakununia.
 Ukitabasamu mbele mbele ya mwenzako naye atatabasamu. Mtu mwenye kabila moja na Shetani ndiye pekee anaweza kumkasirikia mwenzake mwenye kumuonesha tabasamu.
Cheka na mwenzako ili akuchekee. Kuwa na furaha wakati wote ndipo utaona na wenzako wanaonesha furaha wanapokuwa na wewe.
Siku zote uzuri wa mwenzako unaanza na wewe. Uungwana ukiuanzisha utakufuata. Ukikunjua tabasamu utakunjuliwa. Ukijishirikisha kwa wenzako nao watashiriki kwako. Siku zote ushirikiano humuelekea mpenda ushirika.
Asante.
Ndimi Luqman Maloto
Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment