BINADAMU
tunaongozwa na hisia ambazo hutengeneza pupa. Kila mja huumba mambo yake na
kutaka kuyatimiza kwa wakati anaotaka.
Ni vizuri
kujiwekea malengo na matarajio lakini subira ni muhimu zaidi. Amini kuwa
hayatimii mambo kwa matakwa ya binadamu, bali kwa ridhaa ya Mungu Mfalme.
Umesingiziwa,
imekuuma sana. Lakini kosa ambalo unafanya ni kuwaza ulivyosingiziwa kupita
kiasi. Unataka ukweli udhihirike mapema ili waliokusingizia waumbuke.
Kadiri muda
unavyosogea ndivyo unazidi kuumia. Unataka matokeo ya haraka. Unasononeka na
hata usingizi hupati. Mara unashindwa kula, presha inashuka, vidonda vya tumbo
navyo vinabisha hodi.
Niruhusu
nikwambie kitu ndugu yangu; Sononeko lako ni kwa sababu hutambui kuwa ukweli
una kawaida ya kuchelewa na hungonja wakati mwafaka ndipo ujidhihirishe.
Unaweza
kutamani ukweli udhihirike leo lakini kumbe siyo wakati mwafaka. Kwa fikra zako
unaweza kudhani ndiyo muda hasa, lakini kumbe sivyo. Ni kwa sababu Mungu ndiye
huamua kipindi gani mwafaka cha ukweli kufanya kazi yake.
Umedhalilishwa?
Vuta subira, usilazimishe heshima ya haraka. Amini kuwa wakati ukifika
utaheshimiwa. Na si ajabu waliokudhalilisha ndiyo wakadhalilika wao. Ukweli una
tabia ya kulipa kisasi, muda wake unapowadia.
Kosa la
kiufundi ambalo wengi wetu hulifanya ni kutaka kulazimisha kuheshimiwa pale
wanapokuwa wamefanyiwa kitendo au vitendo vya udhalilishaji. Amini katika
kusubiri, heshima yako utaipata tu.
Ndugu yangu
ambaye nilipata kufanya naye kazi, marehemu Adolph Balingilaki, alikuwa na
msemo wake aliopenda kuurudia mara kwa mara: “Mtaka heshima kwa nguvu, utalipwa
dharau kwa bei nafuu.”
Hekima za
Balingilaki, Mungu amuweke mahali pema, ni msisitizo uleule kuwa ukifanyiwa
jambo lenye kudhalilisha , ukitaka ulazimishe kuheshimiwa, unaweza kujikuta
unadhalilika zaidi.
George
Stinney Jr, angekuwa na umri wa miaka 87 sasa kama Mungu angemuweka hai.
Aliuawa akiwa mtoto mwenye umri wa miaka 14.
Maskini
George, aliponzwa na Uafrika wake ndani ya Marekani ambako nyakati hizo ubaguzi
wa rangi ulikuwa umekithiri.
Akasingiziwa
ameua mabinti wawili wa Kizungu ambao walikutwa wamekufa. George akakamatwa,
eti kwa sababu ndiye alionekana nao kwa mara mwisho. Akalazimishwa kukiri kosa.
Majaji
Wazungu (all-white jury), walijifungia na kumhukumu George, bila hata utetezi.
Hakuwekewa wakili wa kumtetea. Akahukumiwa kuuawa kwa shoti ya kiti cha umeme.
George
alikuwa mtoto, na aliweka rekodi ya kuwa mtoto mdogo zaidi kuuawa kwa adhabu
hiyo ya kiti cha umeme. Taarifa zinasema kuwa mateso yalikuwa makali mno,
alipasuka mpaka kichwa, maana kiti kile cha umeme hakikutengenezwa kwa ajili ya
watoto. Kililazimishwa kutumika kumuua George.
Jaribu
kujiuliza George aliumia kiasi gani kuuawa kwa kosa ambalo hakulifanya? Wazazi
na ndugu zake waliumia kiasi gani? Unadhani George hakupenda ukweli ujulikane
kabla hajauawa?
Mungu
alitaka kuwaumbua Wazungu! George aliuawa Juni 16, 1944. Mwaka 2014, yaani
miaka 70 baada ya kifo chake, ndipo Mahakama Kuu Marekani, ilitoa hukumu ya
kukosoa hukumu ya mwaka 1944 (Conviction vacated), kwamba George alionewa.
Ikaamriwa familia yake ilipwe fidia.
Mwaka 2004,
mwandishi Mmarekani ambaye ni mbobezi wa historia, George Frierson, ndiye
aliyeibua kila kitu. Baada ya kufanya marejeo na rekodi mbalimbali, kesi
ilirudishwa mahakamani na hukumu tofauti ilitolewa
Mbona Yusuf
alitumbukizwa kisamani na ndugu zake kisha wakamwambia baba yake kuwa ameliwa
na wananyama wakali? Mbona Yusuf huyohuyo alisingiziwa amembaka Zulaikha ambaye
ni mke wa aliyekuwa Mfalme wa Misri, Potiphar.
Matokeo yake
Yusuf alifungwa jela. Siku ukweli ulipodhihirika, Yusuf alitoka jela kama
shujaa, na mwokozi wa taifa la Misri. Ndugu zake pia walifedheheka kwa kumtenda
ubaya na kusingizia kuwa ameliwa na wanyama.
Nini
kilimpata Zulaikha? Zipo taarifa kuwa Potipher alimuua Zulaikha kimyakimya
baada ya kubaini ukweli kuwa alimsingizia Yusuf, na kwamba ni yeye ndiye
aliyemtaka kimapenzi.
Jiulize,
hapo ulipo una wasiwasi gani? Mbona unakuwa na haraka? Vuta subira, muda
utafika na wewe utakuwa huru. Usijiumize kwa kutaka matokeo ya papo kwa papo.
Karne 12
kabla ya Yesu (BC), walikuwepo ndugu wawili, Anubis ambaye alijulikana pia kama
Anpu na mdogo wake, Bata. Waliishi vizuri sana na walisaidiana kwenye shughuli
za shamba.
Siku moja
wakiwa shamba Anubis alimtuma Bata nyumbani kwenda kuchuchukua mbegu ili
wapande shambani.
Bata
alipofika nyumbani, alikuta mbegu ni nyingi, kwa hiyo ili isiwe mizunguko ya
nenda rudi, aliamua kubeba mzigo wote kwa wakati mmoja.
Uwezo huo wa
kubeba wa Bata, ulimuonesha ni kijana mwenye nguvu. Mke wa Anubis (kaka yake
Bata) aliyekuwa nyumbani, alivutiwa na msuli wa Bata, akamtongoza.
Bata
alishangazwa na namna ambavyo mke wa kaka yake alivyomtamkia maneno ya
kimapenzi. Kwa hasiri Bata alimwambia shemeji yake: “Usirudie siku nyingine
kuniambia maneno ya kishenzi kama hayo.”
Baada ya
kumjibu hivyo, Bata alibeba mbegu zote mpaka shambani kisha wakaendelea na
shughuli za shamba pasipo kumsimulia chochote kaka yake kwa kutambua,
angemweleza bila shaka ndoa ingeweza kuvunjika.
Hata hivyo,
yule mwanamke, yaani mke wa Anubis, aliona kitendo alichofanyiwa na Bata ni cha
dharau, na kumkosea heshima, kwa hiyo aliamua kumkomoa kwa kumchonganisha na
Anubis.
Anubis na
Bata waliporudi nyumbani, mke wa Anubis alimwita mumewe chumbani watete, wakati
huohuo Bata aliingia zizini kulisha mifugo.
Kule ndani,
mke wa Anubis alimuonesha mumewe nguo iliyochanika, alama za mwili kama vile
alipata kashkashi nzito, akasema akiangua kilio: “Bata, huyuhuyu mdogo wako
unayempenda, alinitaka kimapenzi, nilipomkatalia, alinilazimisha mpaka kutaka
kunibaka. Ndiyo hii hali unaiona hapa.”
Bata akiwa
kwenye mifugo, anapewa taarifa kupitia wale wanyama kuwa Anubis anataka kumuua
baada ya kupewa maneno ya uchonganishi na mkewe. Anaelekezwa akimbie haraka
kabla hajauawa, kwani Anubis ana hasira sana.
Kweli,
Anubis akiwa na hasira kali, anakwenda zizini akiwa na panga ili amtenganishe
Bata kichwa na kiwiliwili kama adhabu ya jaribio lake la kumbaka shemeji yake.
Anubis aliumia sana mdogo wake kipenzi ambaye wameishi kwa mapenzi yote miaka
nenda rudi, kuthubutu kumtaka kimapenzi mkewe na hata kujaribu kumbaka.
Anubis
alipofika zizini hakumkuta Bata. Alimtafuta huku na huko bila mafanikio. Bata
alikimbilia mbali mno.
Bata aliumia
mno kusingiziwa, alitamani ukweli ujulikane haraka ili yeye na ndugu yake
waelewane. Haikuwa hivyo. Ukweli una kawaida ya kuchelewa lakini ukiwadia hutoa
adhabu kali kwa mlengwa na walengwa.
Anubis
aliishi kwa hasira, akimuwinda mdogo wake. Alitamani kumuua. Nyakati hizo
nchini Misri, ukimtongoza mwanamke wa mtu, adhabu yako ni kifo. Anubis alitaka
Bata afe kufidia makosa ya kujaribu kuingilia ndoa yake.
Ngoja sasa
nikwambie. Vuta pumzi kwanza japo kidogo. Haya sasa, uongo uliopikwa na mke wa
Anubis, ulizunguka siku zote kwenye kichwa cha Anubis, na kujenga hasira kali
kwa Bata.
Sasa tambua
kuwa ilifika wakati Anubis aliuelewa ukweli, na siku hiyohiyo hakumkwawiza
mkewe, alimuua kikatili, kwa hasira zenye ujazo wa aina mbili. Kwanza
kumsaliti, hadi kumtaka mdogo wake, pili kumfitinisha na mdogo wake kipenzi.
Hiyo ndiyo
inaitwa hasira za ukweli. Tambua kwamba uongo unaweza kutawala hata miaka 10,
lakini siku ukiamua kujidhihirisha huwa na matokeo makubwa.
Ona hata
sasa, zimefika nyakati ambazo wafu wanakumbukwa. Wanahitajika mno kuliko wakati
wowote.
Waliitwa
magaidi na majina mengine chungu nzima. Walisemwa ni wao wanaoifanya dunia kuwa
mahali hatari. Waliandamwa na kuuawa kinyama.
Chuki ya
Marekani dhidi ya aliyekuwa Rais wa Iraq, Saddam Hussein, ilikuwa kubwa mno.
Kizazi kwa kizazi. Mwisho wakafanikiwa kumuondoa na kumuua.
Wamarekani
walidhamiria hasa kuhakikisha aliyekuwa Kiongozi wa Libya, Muammar Gaddafi
anang’oka. Hawakufanikisha hilo tu, bali pia na mauti yake.
Na Gaddafi
alionya: “Marekani na wenzake wa Magharibi wanataka niondoke lakini wanatakiwa
kufahamu kwamba uwepo wangu ni salama mno kwao.” Maneno hayo hawakuamini,
wakamuua.
Leo hii
Wamarekani wanawalilia Saddam na Gaddafi! Ted Cruz ni mgombea urais,
anayetafuta tiketi ya uteuzi kupitia Chama cha Republican, moja ya mambo ambayo
amekuwa akiyasimamia ni kuwa nchi yake ilifanya makosa kuwavamia Saddam na
Gaddafi.
Anasema:
“Mashariki ya kati ingekuwa salama zaidi kama Saddam na Gaddafi wangeendelea
kuwepo. Kuuawa kwa watu hao wawili kumesababisha machafuko kuwa mabaya.
Mashariki ya Kati imekuwa sehemu hatari zaidi ya kuishi.”
Mgombea
mwingine wa urais wa Marekani, anayewania tiketi ya Republican, Donald Trump,
anasema: “Siyo Mashariki ya Kati tu, dunia nzima ingekuwa salama kama Gaddafi
na Saddam wangekuwepo.”
Trump
anasema kuwa Marekani imefanya kosa kubwa kuivamia Syria na kutaka kumng’oa
Bashar al-Assad, kwani machafuko yamekuwa makubwa zaidi.’
Wana haki ya
kulia; Kwa mujibu wa ripoti za Serikali ya Marekani, vitendo vya ugaidi
Mashariki ya Kati kuanzia mwaka 2002 na 2014, vimeongezeka kwa asilimia 4,500.
(Msisitizo asilimia 4,500).
Ripoti
zinaonesha pia kuwa kabla ya mwaka 2003 wakati Marekani ilipoivamia Iraq, taifa
hilo halikuwahi kuwa vitendo vyote vya ugaidi na kujitoa mhanga chini ya
Saddam. Ilala sasa kuna mashambulizi 1,892.
Taarifa za
Serikali ya Marekani zinaonesha kuwa nchi hiyo imetumia dola trilioni 6, ambazo
kwa fedha za Kitanzania ni karibu shilingi trilioni 13,000 (quadrillion 13).
Idadi hiyo
ya fedha, inakadiriwa kuwa sawa na kila makazi nchini Marekani kupewa gawio la
dola 75,000 (shilingi milioni 161). Na inashtumiwa kuwa fedha nyingi kati ya
hizo ni za kukopa.
Ongezea kuwa
zaidi ya wanajeshi 7,000 wa Marekani wamesharipotiwa kufariki dunia kutokana na
vita hizo. Makumi elfu ya wanajeshi wamekuwa hawatambuliki walipo.
Hakika,
ukweli unapotokeza huwa na nguvu sana. Hutoa kishindo kizito. Una kelele
nyingi.
Ndimi Luqman
Maloto
0 comments :
Post a Comment