Luqman
Maloto
ELIMU huleta
heshima, hupandisha daraja la msomi. Ni nyezo inayosababisha chakula kifike
mezani bila usumbufu. Ni silaha inayorahisisha maisha kwa upana kabisa.
Elimu ndiyo
silaha rahisi inayoweza kumfanya mtoto wa maskini kunyenyekewa na kuogopwa hata
na matajiri! Mtoto wa mtumwa msomi, aliweza kuwafanya Wazungu wakae mezani na
kujadili uhuru wa mtu mweusi.
Pamoja na
mambo mengine yote yanayoweza kutamkwa lakini ukweli ulionyooka ni kuwa ni
elimu ndiyo iliwafanya Wamarekani kunyoosha mikono kwa Jaluo wa Kenya, Barack
Obama kisha kumkabidhi nchi awaongoze.
Obama
asingesoma, hata angekuwa na karama ya aina gani Wamarekani wasingemchagua. Hata
chama chake, Democrats, kisingempitisha kuwa mgombea urais. Waliompendekeza
wasingeshawishika kumuona anafaa. Hata yeye mwenyewe binafsi, asingekuwa na
jeuri ya kujitokeza.
Elimu
humjengea mtu hali ya kujiamini. Wapo watu wengi wenye uwezo mkubwa lakini
hushindwa kunyoosha maneno mbele ya wasomi. Na hatua muhimu ya mtu kuyaelekea
mafanikio yake binafsi ni kujiamini. Mpe mwanao elimu ili ayaone haya maisha ni
mepesi!
Rais wa
zamani wa Afrika Kusini, hayati Nelson Mandela, aliwahi kusema: “Education is
the most powerful weapon which you can use to change the world.”
Kiswahili: Elimu
ni silaha yenye nguvu kuu ambayo unaweza kuitumia kuibadili dunia.
Mwanasaikolia,
msomi wa Botania na mvumbuzi mashuhuri wa Marekani, George Washington Carver,
aliwahi kusema: “Education is the key to unlock the golden door of freedom.”
Kiswahili:
Elimu ni ufunguo wa kufungulia mlango wa dhahabu wa uhuru.
Wito na
msisitizo wa muda mrefu umeshatolewa kuhusu umuhimu wa kumuelimisha mtoto wa
kike. Ipo kaulimbiu maarufu kuwa ukimuelimisha mtoto wa kike, umeelimisha jamii
nzima.
Ursula Burns
ni mmoja wa wanawake wa kuigwa mno katika ulimwengu wa sasa. Yeye bila shaka
yoyote, ameweza kuyafanya yasiyowezekana kuwezekana.
Mtoto wa
mkimbizi, aliyelelewa na mama maskini, tena Mwafrika katika jamii iliyojaa
ubaguzi wa rangi. Sasa ni mwanamke wa mfano, tajiri na mwenye kunyenyekewa mno.
Anaingiza
fedha nyingi kutokana na mshahara anaolipwa. Siyo maskini tena, kwani mamilioni
ya dola lakini mabilioni ya fedha kwa kulinganisha na sarafu ya Tanzania
(shilingi), yanaingia kwenye akaunti yake kila mwaka.
Ni kweli
anastahili pongezi lakini upande wa pili hakuna maajabu yoyote hapo, ni elimu
ndiyo imefanikisha kila kitu. Kama upo shuleni soma, ikiwa upo mitaani lakini
unayo fursa, nenda kasome. Elimu ni fedha, ni heshima, vilevile ni mamlaka.
Ursula
anazungumziaje hatua aliyofikia? Anasema: “Dreams do come true.” Akimaanisha:
“Ndoto hutimia kuwa kweli.”
Anasema:
“Ndoto huwa kweli, lakini siyo bila ya msaada wa wengine, elimu nzuri, kuwa na
maadili imara ya kazi na ujasiri wa kufikia makusudio yako.”
Hapo utaona
kuwa Ursula anaeleza umuhimu wa elimu nzuri kama nyenzo muhimu ya kufikia
mafanikio kama yake. Mengine yote yanawezekana, kwa maana ya msaada kutoka kwa
watu wengine, kuwa na maadili na ujasiri lakini elimu je? Lazima usome kwanza.
URSULA NI
NANI?
Ursula ndiye
Ofisa Mtendaji Mkuu (CEO) , vilevile Mwenyekiti wa Shirika la Xerox, Marekani.
Kutokana na ukuu huo, Kampuni ya Fortune 500 ambayo huchapisha jarida maarufu
Marekani la The Fortne 500, limekuwa likimtambulisha kama mwanamke mwenye nguvu
zaidi.
The Fortune
500 ni jarida ambalo hutoka mara moja kwa mwaka, likiwa na orodha ya mashirika
500 makubwa.
Katika
orodha hiyo, huangaliwa mapato kwa mtindo wa ile ambayo imefanya vizuri zaidi
hadi nafasi ya 500 katika mwaka husika wa fedha.
Ursula akiwa
bosi bosi wa Xerox, alitokea kuwa mwanamke wa kwanza mwenye asili ya Afrika,
kuongoza orodha ya mashirika 500 katika jarida la The Fortune 500, kutokana na
mafanikio anayopata.
Vilevile
akawa mwanamke wa kwanza kuongoza katika The Fortune 500 akimrithi mwanamke
mwenzake, Anne Mulcahy.
Mulcahy
ndiye alikuwa CEO wa Xerox, nafasi ambayo alimwachia Ursula ambaye anaendelea
kuishikilia kwa mafanikio makubwa.
Xerox ni shirika ambalo linajikita kwenye mauzo ya
huduma za kibiashara na nyaraka za kiteknolojia kwa ajili ya bidhaa za
kibiashara na kwa serikali katika ukubwa na viwango vya aina mbalimbali.
Makao makuu
ya Xerox yapo Norwalk, Connecticut, kabla ya hapo, yalikuwa Stamford,
Connecticut, Marekani. Makao hayo yalihamishwa Octoba 2007 kwa sababu za kibiashara
na kihuduma.
Ni shirika
linalotengeneza faida kubwa na ndiyo maana kwa miaka mfululizo, limekuwa
likishika namba moja. Hii ni kwa sababu limekuwa likitengeneza faida kubwa kila
mwaka.
Kutokana na
mafanikio hayo, ukiachana na jarida la Fortune 500, upande mwingine jarida la
The Fortune, limekuwa likimtaja kama mwanamke mfanyabiashara bora kwa miaka
sita mfululizo, tangu mwaka 2009.
Mwaka juzi
(2014), jarida maarufu kwa takwimu mbalimbali ulimwenguni, Forbes, lilimtaja
Ursula kuwa mwanamke wa 22 kati ya 100 wenye nguvu zaidi ulimwnguni.
Ni bilionea,
mwaka 2014, mshahara wake ulitajwa kuwa dola milioni 18.7 ambazo kwa
ubadilishaji wa fedha kwa Shilingi ya Tanzania ni sawa na bilioni bilioni 40.9.
Fahamu ya
kwamba hizo siyo mali zake, huo ni mshahara tu kwa mwaka husika, yaani 2014.
Mafanikio
yote hayo, yamefuata baada ya msoto wa hali ya juu. Mwenyewe anakumbuka kila
kitu na shukurani zake za kipekee huzielekeza kwa mama yake mzazi kwamba
alikuwa bora sana katika kumsimamia na kumjenga hadi kufikia mahali alipo hivi
sasa.
Ursula
anasema: “Nimelelewa na mama bora sana, mama mzuri mno. Hakuwa na fedha lakini
mapenzi yake kwa mimi mtoto wake yalikuwa ni zaidi ya kitu chochote kile.
Hakuwa na maisha ya uhakika, lakini alihakikisha naishi na kupata elimu bora.
“Mimi na
mama yangu tuliishi katika makazi duni yaliyo kwenye mpango wa msaada wa
serikali, katika bonde la Mashariki ya Mji wa Manhattan katika Jiji la New York.
“Wakati wa
ukuaji wangu, watu wengi walianiambia nilikuwa na majanga ya aina tatu
yaliyokuwa yakinikabili. Kwanza nilikuwa mtoto mweusi, pili nilikuwa msichana,
tatu nilikuwa maskini.
“Kwa
kujumlisha mambo hayo matatu, watu walisema nilikuwa na bahati mbaya na kwa
hivyo, nisingeweza kufanikiwa. Leo hii ninapojitazama na kugundua
nimethibitisha tofauti kwa wale walioamini sitaweza kufanikiwa kutokana na
kasoro tatu nilizokuwa nazo, hakika namshukuru Mungu.”
Ursula
anasema kuwa siyo uongo kwamba kulikuwa na changamoto pevu. Anaeleza kuwa
maisha yalikuwa magumu, yenye kujaa ubaguzi na manyanyaso ambayo ilitaka moyo
kuvumilia.
Anabainisha
kuwa kama siyo mama yake kumtia moyo na kumjaza maadili ya namna bora ya
kuenenda katika maisha, pengine angeharibikiwa akiwa binti mdogo au hata kukata
tamaa.
Ursula
anasema: “Watu walisema nina upungufu kwa umaskini wangu, weusi wangu na
vilevile ni mtoto wa kike, lakini mama hakunitazama kwa macho ya aina hiyo.
Aliamini ningeweza kutoka nilipokuwa na kufika mahali bora zaidi.”
Chukua hii;
Kama mzazi, mtoto wako anahitaji neno kutoka kwako. Huwezi kuamini lakini ni ukweli
kuwa neno la kumtia moyo na kumfariji linaweza kumjenga mpaka kuona anaweza
kuubeba Mlima Kilimanjaro begani.
Mwambie
mwanao anaweza kushinda. Anafanya vibaya darasani lakini hilo lisikuvunje moyo,
mweleze kuwa yeye ni bora na ana akili nyingi. Huwezi kutambua lakini ndiyo
ukweli kuwa utakuja kugundua baada muda anatengeneza A badala F ulizozizoea.
Ni hivyo
ndivyo Ursula alivyojengwa na mama yake. Katika jamii iliyokuwa inamdharau na
kumuona siyo kitu, mama wa Ursula alimwambia mwanaye: “Elimu ndiyo njia pekee
ya kukupandisha na kukutoa kimaisha. Wewe ni bora kuliko wao.”
Ursula
anasema: “Kwa kipato duni ambacho mama yangu alipata, alijinyima na kudunduliza
kisha kunipeleka kwenye shule nzuri. Nilisoma kwenye shule nzuri za Kanisa
Katoliki. Haikuwa rahisi lakini mama yangu alijituma kufanya kazi na kupata
fedha za kutosha kunilipia ada na michango mingine.
“Nyakati
hizo, nilitamani kusoma ili nipate kazi ya haraka angalau niweze kumsaidia mama
yangu. Nilitamani kuwa mhubiri, mwalimu au nesi. Hizo ndizo zilikuwa ndoto
zangu kwa kipindi ambacho nilikuwa binti mdogo wa shule. Sikujua kama ningemudu
kufika kwenye daraja nililopo kwa sasa.”
Ursula
anaendelea kusema: “Katika vipaumbele vyangu hivyo vitatu, uhubiri, ualimu na
unesi, hakuna hata kimoja kiliweza kudumu kwenye mapenzi yangu. Nilipokuwa
napanda madarasa ya juu, nilitamani kuwa mhandisi. Na hii ni kwa sababu
nilikuwa namudumu vizuri masomo ya Sayansi na Hisabati. Kila muda niliwaza
uhandisi. Nilitamani kuwa mhandisi mashuhuri.
“Baada ya
kufuatilia ndoto zangu na maendeleo yangu shuleni, chuo cha Brooklyn
Polytechnic Institute kilinipa ofa kujiunga nao kwa ajili ya masomo ya
uhandisi. Wakati ilitarajiwa kuwa kwa ofa hiyo ningeshangilia na kuona ndoto
zangu zinakwenda kuwa kweli, mimi nilichanganyikiwa.”
Ursula
anasema kuwa kilichomfanya achanganyikiwe ni kwamba hakuwa mwangalifu tangu
mapema juu ya kipi hasa ambacho alikuwa anahitaji kusomea, maana uinjinia
ulikuja tu kama wimbo kutokana na jinsi alivyokuwa anazungumza na wanafunzi
wenzake na matokeo ya masomo yake.
“Ni ofa sawa
lakini niliona natakiwa kuwa mwangalifu kuhusu kipi hasa napenda kukifanya.
Nilikuwa sijajifanyia maandalizi ya kutosha. Kingine niliona chuo kilikuwa na
mazingira tofauti, maana Brooklyn niliona ipo tofauti na maeneo mengine ya New
York.
“Nilihofia
pia umbali, kwa hiyo niliona nitakuwa kama mgeni na mazingira yote yangekuwa
mageni kwangu. Kingine kilichonipa hofu ni wanafunzi wengine, niliamini
wangekuwa na akili sana kuliko mimi,” anasema Ursula.
Hatma yake
ilikuwaje? Ursula anasema: “Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nilikuwa
nipo njiapanda. Upande mmoja akili yangu iliniambia niende chuo, upande wa pili
inanirudisha nyuma kwa kuamini mazingira yangenipa shida.
“Ilikuwa
rahisi zaidi kuacha ndoto zangu ziende kisha kupanga upya safari ya maisha
yangu kwa namna ambavyo ningeona ni rahisi. Asije kukwambia mtu, ukiwa na mama
mzuri ni mtaji mkubwa sana katika maisha yako. Mama yangu ni mtaji mkuu.
“Mama
alinipa ujasiri, aliniambia Brooklyn isingenishinda na wanafunzi wasingekuwa na
akili kuliko mimi. Alinijenga kiakili na nikakomaa kisaikolojia. Ukijumlisha na
mafunzo ya kiroho niliyoyapata katika shule ya Kikatoliki ya Cathedral High
School, nilijikuta napata moyo na kuamua kujiunga na chuo hicho.
“Nilipofika
shule mambo hayakuwa mepesi. Ilibidi nisome kwa bidii ili niweze kwenda sawa na
wenzangu. Nilikuwa kiumbe wa ajabu baharini. Chuo kilikuwa na wanafunzi wengi
wanaume Wazungu. Mimi nilikuwa mwanamke, Mwafrika.”
Anaeleza
kuwa alijitahidi kuzoea mazingira na kutokatishwa tamaa, ingawa kwa muda mrefu
alikuwa akijihofia kila alipokuwa akiwatazama wanafunzi wenzake waliokuwa
wamemzunguka.
“Nilianza
kusoma chemical engineering, ambayo nilijikuta naichukia, na baada ya muda
nilibadilisha na kusoma mechanical engineering, ambayo niliipenda. Na taratibu
nilijikuta naweza, napenda mazingira ya shule, kuwaelewa na kuwakubali
wanafunzi wenzangu, na hapo ndipo nilianza kufanya vizuri zaidi katika masomo.
“Kuanzia
wakati huo, maisha yangu yalibadilika na kuwa na mtiririko mzuri. Nikiwa bado nasoma,
nilijiunga na Xerox, ofisi zao za New York, kwa ajili ya mafunzo ya mafunzo ya
vitendo kisha nikaenda Ivy League school ambako nilifanikiwa kumaliza shahada
yangu ya kwanza ya uhandisi.
“Baada ya
kuhitimu shahada yangu, niliajiriwa na Xerox, nilifanya kazi lakini baadaye
nilirudi tena chuo ambako nilisoma shahada yangu ya pili, na hapo ndipo
nilipoanza kupanda ngazi mpaka juu kabisa katika kampuni.
“Nikiwa CEO
wa Xerox, nimelifanya shirika kutoka katika mkondo wa nakala na uchapishaji,
kisha kuliingiza kwenye ulimwengu wa kiteknolojia pamoja na upana wa huduma
zake.”
Ursula
anasisitiza: “Ndoto hutimia lakini ni rahisi zaidi ukiwa na elimu nzuri pamoja
na watu. Ndiyo maana nimetumia muda mwingi na shirika ambalo linajihusisha na
utoaji wa msaada kwa mtu mmojammoja.
“Wito wangu
kwa wanawake ni kuwa kutafuta elimu na kuipata, vilevile kuheshimika inatakiwa
juhudi, kuota ndoto kubwa na natumaini ipo siku kila kitu kitalipa kwa yeyote
mwenye kuweka bidii na kudhamiria kweli kufanikiwa.”
NI BOSI WA
MUME WAKE
Ursula ni
mke wa Lloyd Bean, ambaye alikuwa mfanyakazi wa Xerox. Na kipindi akiwa
mfanyakazi kwenye shirika hilo, mume huyo alikuwa chini kicheo kwa Ursula.
Wanaishi Manhattan,
New York. Ursula na Bean wana mtoto mmoja wa kike anaitwa Melissa lakini mume wake,
ana mtoto mwingine wa kiume Malcolm ambaye alimpata kabla hajafunga ndoa na
Ursula.
Alizaliwa September
20, 1958, hivi sasa ana umri wa miaka 57. Hujishughulisha na siasa na chama
chake ni Democrats.
Asili ya
Ursula ni Panama ambako ndiko asili asili ya wazazi wake wote wawili. Mama yake
alihamia Marekani na kuchukua uraia wa nchi hiyo na ndiyo ikawa sababu kwa
Ursula kuwa Mmarekani.
MWANAMKE
SOMA
Michelle
ambaye ni mke wa Rais wa Marekani, Barack Obama, aliwahi kuwaambia watoto wa
kike: “Unapokuwa shule ni eneo la
kujenga msingi wako wa maisha. Unaweza kuwa unamaanishwa kuwa na nafasi kubwa
lakini macho ya karibu yakikupotosha utapoteza fursa kubwa ya baadaye.
“Mimi
sikuruhusu mvulana achezee maisha yangu, nilipokuwa high school nilisoma
kwelikweli na kila siku nilizingatia masomo yangu, leo hii najivunia kuwa mke
wa Rais wa Marekani. Usiwe na haraka, soma!”
Michelle
aliongeza: “Hakuna mvulana katika umri wenu ambaye ni mzuri (handsome) sana au
ana mvuto sana kiasi cha kukufanya wewe usisome, hakuna.
“Kama
ningeingia wasiwasi kuhusu nani alinipenda na yupi alifikiri kwamba mimi ni
mzuri. Ningefikiria vijana wazuri (ma-handsome), leo hii nisingekuwa mke wa
Rais wa Marekani.”
Michelle
aliwaambia wanafunzi wasichana kuwa wavumilivu na kujipa msukumo katika miaka
minne wanapokuwa ‘high school’ na kuachana na vitu vidogo ambavyo vinaweza
kuwachanganya.
“Hutakiwi
ukiwa na umri wa miaka 60 uwe unakumbuka na kujuta kwa miaka minne ambayo
hukujituma inavyotakiwa. Utakuwa na fursa, na utakuwa na udhibiti wa maisha
yako kufanya uchaguzi wa mambo yako mwenyewe. Na hutakuwa na ulazima wa
kusikiliza wazazi kwa sababu utakuwa na kazi yako na bili zako utazilipa
mwenyewe. Unataka uhuru. Uhuru utakuja baadaye, kwa sasa soma kwanza.
“Sasa
unawekeza. Sasa unajenga uwekezaji wako. Sasa unatakiwa kuwa mvumilivu. Hii ni
kwa sababu kama hutakuwa hivyo sasa, utakwenda kuishi maisha ya hovyo katika
uhai wako wote uliosalia,” alisema Michelle.
0 comments :
Post a Comment