Luqman
Maloto
PUMZI
unayovuta ina maana kubwa mno. Kila unapoingiza oksijeni na kupokelewa na
mapafu yako, hilo ni deni kwa Mungu. Jiulize unaitumiaje?
Tundu zako
za pua zinapotoa nje hewa ya kabon (carbon dioxide), kinachomaanishwa ni kuwa
uhai unao, kwa hiyo unalo jukumu la kufanya.
Kila nukta
inayokwenda kwa Mungu, humaanishwa kukatishwa kwa uhai wa binadam kwa makundi.
Ukiona umemaliza sekunde 60 ukiwa hai, tambua kuwa Muumba bado anao mpango
mahsusi na wewe.
Hebu itikia
mpango wa Mungu juu yako. Acha kuwazia ugumu wa maisha unaokukabili, anza
kupiga hesabu za kufanikiwa.
Watu wengi
huumiza kichwa kwa unyonge wao, wakifikiria shida na changamoto za maisha,
badala ya kuupa ubongo nafasi ya kupumua kisha uutumie kuwaza njia za
mafanikio.
Chukua hii;
Matumizi mabaya ya muda ni kuusotesha ubongo wako kufikiria magumu ya maisha,
katika kipindi ambacho unatakiwa kupiga hesabu makini za namna bora ya kubadili
kibao cha maisha, kutoka dhiki za kila siku mpaka faraja na neema.
Ni kwamba
kama unavyoishi hutambui kuwa umeachwa kwa sababu maalum, hutafanya chochote
cha maana. Ni kwa sababu hujui hata sababu za wewe kuishi.
Ukiwa
mnyonge maana yake hujiamini. Hutambui kuwa wewe ni mteule wa Mungu, kwa hivyo
kama ambavyo anaendelea kukupa pumzi, ndivyo na ulinzi wake unavyoandamana na
wewe. Kama Mungu ndiye mlinzi wako, sasa unyonge wa nini?
Tambua kuwa
maisha ya binadamu yana mengi katikati yake. Zipo kumbukumbu nyingi za kuumiza,
zipo pia za kufurahisha. Ni kosa kubwa kwa kesho yako, endapo utaruhusu
kumbukumbu za maumivu ziteke hatma yako.
Umetendewa
jambo baya, umeumia, sema “asante Mungu”, unachotakiwa kufanya ni kuelewa kuwa
kwa vile bado upo hai basi unalo jukumu la kufanya. Maumivu yote weka pembeni.
Ni ukweli
kuwa huwa vigumu kusahau unapotendwa mambo mabaya lakini hiyo isikutawale.
Amini kuwa ni mapito kisha mwenyewe jisemee moyoni: “Nyakati zijazo zina neema
kubwa!”
Wapo wanaume
wenye hulka za kinyama, wao bila kubaka wala hawaoni fahari. Je, imekutokea
hivyo, ni kweli inauma kupita kiasi, lakini unayo nafasi ya kumshikisha adabu
mbakaji wako hata kama hukumfikisha kwenye mkono wa sheria.
Ni adabu
gani? Tafuta fedha mama! Nakuhakikisha ukishafanikiwa, huyo mbakaji wako
hatakuwa na amani, maana atahisi wakati wowote unaweza kumrudi kwa kitendo
kibaya alichokufanyia.
Chukua hii; Watu
waovu, huombea kila siku wale waliowatendea mambo mabaya wasifanikiwe katika
maisha yao. Akili zao za dhambi huwatuma kuwaza kwamba watalipiziwa kisasi.
Unadhani una
haja ya kulipa kisasi? La hasha! Utapoteza muda, endelea kutengeneza fedha na
utaona jinsi ambavyo mbaya wako anavyosulubika.
Alikuwa na
akili sana yule aliyeanzisha ombi kwa Mungu, kuwapa umri mrefu maadui zake ili
washuhudie mafanikio yake.
Chukua hii;
Huhitaji bunduki wala upanga kumsulubu adui yako, tafuta fedha mpaka uzikamate.
Hatua zako za mafanikio ni sawa na silaha ya maangamizi kwa adui yako. Kadiri
unavyojitanua kwa mafanikio, ndivyo anavyotaabika na maisha.
Ni kama
Hilary Devey, alibakwa, akapewa mimba akiwa binti mdogo mwenye umri wa miaka
12.
Devey baada
ya kufanyiwa kitendo hicho, hakuona kama maisha yamemuelemea, alichukulia kuwa
ni ajali kama ambavyo huwakuta wengine, kwa hiyo alijikita kuitazama kesho
yake.
Ona matunda
ya kuyawazia mafanikio ya maisha, leo hii Devey ni mwanamke tajiri. Yupo kwenye
namba za juu katika matajiri wanawake nchini Uingereza.
Akiwa na
mtoto mgongoni huku na yeye akiwa mtoto, alikumbana na misukosuko mingi ya
kimaisha, malezi bila fedha, kula ya shida, mahitaji ya mwanaye kwa ngama,
lakini yote hayo ni historia.
Devey bila
elimu, amethibitisha kuwa mafanikio katika maisha hayana tafsiri ya kukaa
darasani peke yake, bali inawezekana kabisa kuitwa tajiri pasipo kuwa na shule
kichwani, muhimu ni kujitambua na kujituma.
Kwa nini
kujitambua? Ni kwamba kwa mtu anayetambua kuwa anao upungufu wa kielimu, atajua
namna ya kuenenda ili kuziba mwanya ambayo unaweza kuonekana. Devey aliweza.
Nchini
Uingereza ni nani ambaye hampi heshima yake Devey leo. Hata yeyote anayepata nafasi
ya kumsoma, alivyohangaikia maisha mpaka kufika alipo akilimiliki mamilioni ya
pauni (mabilioni ya shilingi), ni lazima atie adabu kwa mwanamke huyo shujaa.
Devey ni
mwanamke wa shoka, amethibitisha bila kuacha shaka yoyote kwamba mafanikio
yanatafutwa na yanapatikana. Kwamba hayajaumbiwa wengine, bali yanamhusu kila
mwenye kujituma.
ILIKUWAJE
AKABAKWA?
Machi 10,
mwaka huu, Devey atatimiza umri wa miaka 59, anasema kumbukumbu ya tukio la
kubakwa ilimuumiza kupita kiasi na ilikaribia kumfanya akate tamaa ya maisha.
Anasema:
“Moyoni mwangu kila siku nilijisemea mwenyewe kuwa lazima nitafanikiwa. Hiyo
ndiyo sababu pekee ambayo ilinifanya nisikate tamaa. Niliamini kuwa nitakuwa
mtu fulani mwenye hadhi.”
Kwa mara ya
kwanza, Devey alifichua siri yake ya kubakwa na kupewa mimba mwaka 2013,
alipofanya mahojiano na gazeti la The Sun la Uingereza.
Alieleza
siri hiyo ikiwa ni baada ya kuificha kwa zaidi ya miaka 43, alisema:
“Niliponzwa na dada mmoja jirani yetu ambaye alikuwa mkubwa kwangu, nakumbuka
jina lake ni Sandra. Nilikuwa ndiyo nafika nyumbani, hata sare za shule
nilikuwa sijabadilisha. Sandra aliniita, name kwa kumheshimu niliitikia wito.”
“Nilikuwa na umri wa miaka 12. Tukio lenyewe
lilitendeka jirani na pub ya wazazi wangu. Kipindi hicho wazazi wangu walikuwa
wakimiliki pub hiyo kama biashara pekee ya kuendeshea familia.
“Sandra
alinichukua mpaka kwenye nyumba hiyo jirani na pub ya wazazi wangu.
Akanikutanisha na mwanaume. Ghafla nikashangaa Sandra anaondoka, yule mwanaume
akanivamia. Alikuwa ananuka harufu mbaya.”
Devey
anaendelea: “Nilikuwa msichana mdogo, yeye alikuwa mkubwa. Kwa nguvu sikuweza
kushindana naye kabisa. Alinizidi kwa kila kitu. Mwisho alinibaka na ikawa mara
yangu ya kwanza kuingiliwa na mwanaume.
“Baada ya
kumaliza hakuniacha nirudi nyumbani, aliendelea tena na tena mpaka asubuhi.
Nilipata maumivu makali sana. Na kwa tukio hilo ndiyo ikawa sababu ya kunasa
ujauzito.”
Je, ujauzito
huo uliharibu ndoto za maisha yake? Devey anapinga hilo, anasema: “Ndiyo maana
nipo hapa. Hatua ambayo nimefikia haifanani na mtu aliyewahi kupoteza matumaini
ya kutimia kwa ndoto zake.
“Tena kwa
sasa naweza kukujibu kwa kujiamini kuwa ndoto zangu zimetimia. Pamoja na mengi
magumu niliyokutana nayo lakini nilibaki kwenye mstari wangu. Hii ndiyo sababu
leo najivunia kufanikiwa kwa ndoto zangu.”
Akikumbuka
tukio la kubakwa, Devey anasema: “Sandra aliniwinda kwa muda mrefu.
Nikimfikiria ni kama alikuwa na lengo baya na mimi tangu muda mrefu. Alianza
kwa kujipendekeza kwangu, akijifanya anataka kuwa rafiki yangu. Alinisumbua
sana kutafuta urafiki na mimi.
“Mwanaume
aliyenibaka ni raia wa Italia na alinichania mpaka nguo zangu za shule.
“Nililia na
kupiga kelele lakini hakuna msaada wowote ambao nilipata. Nilimuomba yule
mwanaume aniruhusu niende nyumbani lakini hakunijibu chochote. Msisitizo wake
ulikuwa kwenye kitendo alichokuwa anafanya. Ni mwanaume katili mno.”
Pamoja na
kufanyiwa unyama huo, Devey hakufunua kinywa, anasema: “Yule mwanaume alinionya
kuwa kama ningethubutu kusema chochote angenifanyia kitu kibaya sana.
“Kwa
kumbukumbu ya unyama alionifanyia na kile kitisho alichonipa, niliamini kuwa
usalama wangu ni kunyamaza kimya. Niliogopa kusema kitu wala kufanya chochote
chenye kuashiria kutoa siri. Nilijua angejua na kunibaka tena, vilevile
kunifanyia unyama mkubwa zaidi.
“Kikubwa
zaidi niliogopa kuuawa, maana katika vitisho vyake alisema pia anaweza kuniua.
Ndiyo maana tukio hili limebaki kuwa siri yangu. Nimekaa nalo mpaka leo nikiwa
mtu mzima ndiyo nathubutu kutamka.”
Aliporudi
nyumbani ilikuwaje? Devey: “Baba na mama walikasirika sana, waliamini
kilichonilaza nje ya nyumba ni kupenda kwangu, kwamba nilikuwa na mvulana,
kumbe haikuwa hivyo.
“Baba
hakusema sana, alisema tu nilikuwa na mvulana usiku mzima. Alikasirika na
hasira zake niliziona waziwazi. Mama alikwenda mbali zaidi, maana zilipita siku
kadhaa akawa hanisemeshi kwa chochote. Hili pia liliniumiza sana.”
Devey
anasema kuwa kitendo cha mama yake kutozungumza naye, kilikuwa adhabu kubwa
kwake, ambayo ilimfanya awe anakaa peke yake lakini hakuwahi kulia wala kutokwa
machozi.
“Nilijikuta
nimepatwa na roho ngumu ajabu. Nilihimili presha yote. Sikuwahi hata kufikiria
kuomba msamaha. Nilijua ulimwengu wangu umebadilika lakini sikujilaumu kwa
sababu sikuwa na kosa. Niliumizwa lakini nilihofia maisha yangu kuwaambia
wazazi wangu.”
UMASKINI WA
WAZAZI WAKE ULISABABISHA ABAKWE
Hili huwezi
kupingana nalo, kwamba uwezo wa mzazi ni ulinzi madhubuti kwa mtoto wake.
Ni vigumu
mno kusikia mtoto wa tajiri amebakwa, labda huyo mwana wa tajiri awe ndiye
ametengeneza mazingira ya ‘kujibakisha’.
Inawezekana
vipi mtoto wa kiongozi mkubwa serikalini abakwe? Huyo mwenye jeuri ya kutenda
ubakaji huyo ni nani? Hajipendi?
Na hivyo
ndivyo ilikuwa sababu ya Devey kubakwa. Wazazi wake walikuwa hohehae, kwa hiyo
Sandra na Muitaliano wake, waliamini wasingefanywa chochote.
Chukua hii;
Unawajibika kuushinda nguvu umaskini wako kisha uukaribishe utajiri.
Ukifanikiwa hilo, utakuwa umefanikiwa kujitengenezea ulinzi binafsi na wa
familia yako. Hakuna atakayethubutu kuleta dharau wakati anajua una uwezo
mkubwa wa kumshughulikia.
Devey
alizaliwa na kukuta familia yake ni bora kabisa. Wazazi wake walikuwa na uwezo
mzuri wa fedha na mali, maana baba yake alikuwa mfanyabiashara mkubwa.
Tangu akiwa
mdogo, Devey alijionea utamu wa maisha yenye kutosheleza. Hata hivyo, alikutana
na matokeo tofauti alipofikisha umri wa miaka sita, baada ya baba yake
kufilisika.
“Baba
alipofilisika, maisha yalihama kutoka kuwa na maisha ya kuheshimiwa hadi
kuonekana watu tusiokuwa na thamani. Tulichekwa na majirani. Baba yangu
alibadilika na kuwa mnyonge.
“Hakuna
wakati mgumu katika maisha kama kuwa na mali kisha ziondoke. Baba alihangaika
na baadaye ilibidi afungue pub angalau kufanikisha mahitaji ya familia.”
Anaongeza:
“Sandra na mwanaume wa Kiitaliano, waliona nguvu ya baba yangu haipo tena,
waliniona ni mtu wa familia maskini, ndiyo maana waliandaa na kufanikisha mtego
wao wa kunibaka kwa imani kwamba sitaweza kufanya chochote.”
UTAJIRI BILA
ELIMU
Baada ya
kupata mimba Devey alijitahidi lakini ilishindikana, ilibidi akubali matokeo ya
kuachana na shule.
Anasema:
“Katika familia yetu ninao kaka wawili, wote wamefika mpaka chuo kikuu. Mimi
pekee sijafika hatua nzuri kielimu. Lakini Mungu ni mkubwa kuwa mafanikio yangu
yameweza kuziba kasoro ya kutofika chuo.”
Devey
anaeleza kuwa baada ya kujifungua mtoto wake wa kiume ambaye ndiye wa pekee
mpaka sasa, aliamua kujishughulisha na kazi mbalimbali kwa lengo la kujitafutia
riziki pamoja na huduma kwa mtoto wake.
“Kazi yangu
ya kwanza ilikuwa kumsaidia baba katika pub, nilifanya kwa muda. Baadaye
nilipata kazi Jeshi la Anga la Uingereza kitengo cha wanawake, nilifanya kazi
pale kama mhudumu.”
Tukipitia
maisha ya Devey mpaka kuwa tajiri, hili liweke kwenye ubongo wako kuwa wakati
mwingine unapokuwa unafanya kazi huku na huko, bila kujali taaluma, eneo ambalo
utaliona jepesi kwako, pengine ni hapohapo pa kutilia mkazo.
Kwa kawaida
upo mvutano wa asili kati ya utashi binafsi na kazi ya maisha yako. Kazi ya
maisha yako utaiona nyepesi hata kama ina changamoto nyingi kiasi gani. Kazi ambayo
haikumaanishwa yako, haiwezi kukuvutia kuifanya hata kama ni rahisi, japo ujitume
kiasi gani.
Uthibitisho
wa hilo ni kuwa baada ya Devey kuondoka kwenye utumishi wa Jeshi la Anga la
Uingereza, alifanya kazi mbalimbali lakini akajikuta anapendelea kazi ya
usambazaji wa vifurushi.
Na kwa
taarifa yako, kazi hiyo ndiyo ilimpa mawazo ya utajiri mkubwa ambao anang’ara
nao leo hii.
“Nilikuwa na
umri wa miaka 20 nilipoanza kufanya kazi kwenye kampuni za upokeaji na
usambazaji wa vifurushi. Nilifanya kazi kama karani wa mauzo. Nilijikuta
navutiwa sana na kazi hiyo,” anasema Devey.
Wakati huo,
mtoto wake Mevlit alikuwa anazidi kukua. Na alikuwa anamlea peke yake bila
uwepo wa baba, yaani akisimama mama pekee (single mother).
Hii
ilimfanya aachane na kazi za kuajiriwa kwa muda wote wa kazi, hivyo kuwa ofisa
masoko huru, akijishughulisha na makampuni tofautitofauti kisha alipata malipo
kulingana na jinsi alivyofanikisha upatikanaji wa kazi.
Sababu ya
kuwa ofisa masoko huru na mshauri ni ni ili apate muda mzuri wa kuwa karibu na
mtoto wake.
Mwaka 1996,
kipindi hicho akiwa na umri wa miaka 39, Devey alisikia redioni maelezo ya
mteja kuwa ilikuwa inachukua siku 12 kupata kifurushi chake kwa sababu mtoa
huduma alitaka mpaka apate mizigo ya kutosha kujaza lori, ndipo isafirishwe.
“Ilizungumziwa
miji ya Cardiff na Carlisle, nilijiuliza inakuwaje kufikisha siku 12 kati ya
miji hiyo. Na hiyo ndiyo ilinipa wazo la kuanzisha kampuni yangu ya Pall-Ex
ambayo sera yake ni kufikisha kifurushi mahali husika siku inayofuata. Yaani tukipokea
leo, kesho tunafikisha kifurushi mahali kinapotakiwa kufika,” anasema Devey.
Msingi wa
mawazo ya Devey ilikuwa kumaliza kero kwa watu, kwamba kifurushi kikitumwa
kifike mahali panapokusudiwa haraka. Aliona suala la uchelewaji wa vifurushi ni
tatizo, na kwake tatizo hilo aliliona ni fursa, hivyo alijikita kutaka
kulitatua.
UKIJIAMINI
WAZO LAKO NI ZAIDI YA BENKI
Haikuwa
rahisi, ingawa mwanzoni alijiamini. Alizunguka kwenye mabenki na taasisi za
mikopo kuomba kukopeshwa mtaji bila mafanikio.
Siku zilikuwa
zinakwenda, na alijiamini kuwa hiyo ndiyo njia pekee. Nyakati hizo alihitaji
pauni 125,000, ambazo ni zaidi ya shilingi milioni 400.
Baada ya
kuona mambo magumu, aliamua kuuza nyumba yake, aliyorithi kutoka kwa wazazi
wake, gari lake pia alilipiga bei, ndipo alipata mtaji wa kuanzisha kampuni
yake hiyo ya vifurushi.
Tambua kuwa
uamuzi huo wa Devey ulimfanya akose mahali pa kuishi, bila usafiri, fedha zote
alizielekeza kwenye uanzilishi wa kampuni.
Maisha
yalikuwa magumu zaidi. Alikosa mpaka pesa ya kula, aliishi kama mwanamke wa
mtaani.
Hata kampuni
ilipoanza kazi, alijikuta akiwa mfanyakazi peke yake. Yeye mwenyewe atafute
wateja, kisha apokee oda na kusimamia kusafirisha vifurushi kwa haraka na kwa
namna ilivyotakiwa.
“Ni kampuni
iliyoanza kama ya mwanamke pekee lakini leo hii ina wafanyakazi wengi,” anasema
Devey, anaongeza: “Tumetoka mbali. Baada ya muda niliweza kuajiri wafanyakazi
35 na leo hii tunatengeneza faida ya pauni milioni 75 kila mwaka.”
Kiasi hicho
cha fedha ambacho Devey anakisema ni karibu sawa na shilingi bilioni 250 kwa
mwaka. Je, mpaka hapo maisha yanataka nini?
Na kwa sasa,
kampuni hiyo ya Devey, Pall-Ex, inafanya kazi zake bara zima la Ulaya, hivyo
kumfanya mwanamke huyo kuwa mwenye nguvu mno.
Katika
kitabu chake kinachoitwa How I Made My First Million, Devey anaandika kuwa
mafanikio yake ni matokeo ya kutokata tamaa na kutofikiria ya nyuma, zaidi
kujikita kwenye yajayo ambayo ndiyo yanakuwa na umuhimu mkubwa katika maisha ya
kila mtu.
Hivi sasa,
Devey anamiliki utajiri unaokadiriwa kuzidi pauni milioni 100 ambazo ni
takriban shilingi bilioni 350.
UTAJIRI TU?
Hapana,
Devey alinenepa na kupoteza muonekano wake. Hali hiyo ilimnyima raha, maana
alitamani kuwa na tumbo bapa kama wanawake wengine.
Hiyo
ilimlazimisha mwaka 2009 kufanyiwa oparesheni ya kutengeneza tumbo ambayo
ilimsababishia madhara ya kupooza sehemu ya mwili wake.
Alilala
kitandani, maana hakuweza kunyanyuka na theluthi moja ya ubongo wake
iliharibika. Hiyo ilimchukua muda mpaka kupona.
Vilevile
mwanaye, Mevlit aligeuka mtumia madawa ya kulevya wa kutupa. Kila kilichokuwa
ndani alibeba na kuuza ili apate fedha za kununua heroin. Alipambana kwa miaka
saba kumsaidia mwanaye ambaye alipona kabisa mwaka 2011.
HITIMISHO
Jiongeze
mwenyewe sasa, kwani Devey amefanikiwa kibiashara akiwa mwanamke tu ambaye hata
shule alikimbia kutokana na hali duni ya kwao, hasa baada ya baba yake
kufilisika.
Ukiachana na
biashara, Devey amekuwa mtangazaji mwenye mafanikio makubwa, akitikisa
televisheni ya BBC kupitia program ya Dragons’ Den. Mpaka sasa anaendelea kuwa
staa wa televisheni mwenye mafanikio.
Amekuwa
akiandaa vipindi vyenye kuhamasisha watu kuajiamini kuwa wanaweza kufanikiwa,
kwa kuwapa historia za matajiri mbalimbali, changamoto walizopitia kabla ya
kufanikiwa. Kazi hiyo pia inamuongezea fedha kila siku.
Mwenyewe
umejionea ushujaa wa Devey. Ni kwa nini asiitwe Mama Mhujaa? Nawe amka
upambane.
0 comments :
Post a Comment