
Luqman
Maloto
NAPATA picha
ni kwa nini viongozi wengi hutamani kukaa madarakani mpaka kifo kiwakute wakiwa
wanatawala.
Kenneth
Kaunda ‘KK’ alipokabidhi usukani wa nchi ya Zambia kwa Fredrick Chiluba
(marehemu) mwaka 1991, ilikuwa kama ameruhusu kibao kimgeukie.
Askari
waliokuwa watiifu kwake kipindi chote cha miaka 27 ya utawala wake, waligeuka chungu
ya Kaunda kwa agizo la Chiluba. Zipo nyakati walielekeza bunduki kwa mwasisi
huyo wa Taifa la Zambia.
Wapo viongozi
waliokuwa watiifu kwa Kaunda lakini walijipendekeza kwa Chiluba, na kwa
kujipendekeza kwao ikabidi wamsaliti Kaunda kwamba alikuwa kiongozi mbovu.
Ni kwa
mwendo huohuo, waliomsifu Chiluba kwa uongozi uliotukuka, ndiyo baadaye
walimlamba miguu mrithi wake, Levy Mwanawasa, kwamba yeye ndiye hasa mkombozi
wa Zambia, huku wakimwita Chiluba mharibu nchi, dikteta, fisadi na mpoka haki
za binadamu.
Chiluba angesoma
mabadiliko ya waliokuwa watiifu wa Kaunda walivyogeuka wapambe wake kipindi
ambacho yeye anamshughulikia rais huyo wa kwanza wa Zambia, labda angeshtuka.
Kilichotokea
ni kuwa Chiluba alishtuka pale watiifu wake walipogeuka wapiga makofi wa
Mwanawasa, kipindi hicho akimshughulikia yeye. Ni nyakati, ukishakabidhi
madaraka lazima uisome namba, hata kama ni kimyakimya.
Hata Bakili
Muluzi aliisoma namba Malawi alipokabidhi rungu la utawala kwa Bingu wa
Mutharika.
Wapo waliopata
kumgeuza Muluzi Mungu wao, kumpelekea umbea na kumpa sifa kemkemu za kipambe,
wakinywa kahawa pamoja Ikulu ya Malawi, Lilongwe, baadhi yao walimuimbia
mapambio Mutharika (Bingu), alipokuwa anamshughulikia Muluzi.
Na
hawakusita kusema kuwa Muluzi ndiye aliibomoa nchi. Huu usiuite usaliti, bali
ni fikra maslahi za binadamu. Kwamba ukiwa na ugali utanyenyekewa na kuimbiwa
mapambio ya aina yote, ukiondoka, sifa zote zitamwelekea mwenye ugali kwa
wakati wake.
Ni kama
sasa, Rais wa Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Kikwete, yupo
kwenye kipindi cha mgeuko. Waliokuwa watiifu wake ndiyo wanaosema kipindi chake
kilikuwa hovyo kabisa.
Haiwezekani
hii ikawa haimuumi! Ila bila shaka naye kwa wakati wake alipokea ‘visifa’ vingi
vya kipambe, vilevile aliambiwa mengi kuhusu mtangulizi wake, Benjamin Mkapa.
Unadhani
Mkapa alifurahi kuitwa fisadi wakati wa utawala wa JK? Ilimuuma lakini alikosa
namna ya kufanya kwa sababu ni kipindi ambacho alikuwa ameshakabidhi mamlaka.
Hakuwa mtoa amri, mtengua uteuzi wala msitisha ajira.
Sura hiyo
iende hata kwa Rais wa Pili, Ali Hassan Mwinyi, naye alipoitwa kiongozi goigoi
na waliokuwa wasaidizi wake kwa sababu ya kutetea ugali wao kwa Rais Mkapa,
aliumia, na vile Mungu alimuumba mpole, basi akavumilia na kuacha yapite.
Hivyo basi,
huu ni wakati ambao JK anakumbuka mamlaka yake, anajikuta nyakati zimepita, na
sasa waliokuwa wasaidizi wake wanathubutu kuingiza vidole machoni mwake.
Maneno ya
hivi sasa kutoka kwa waliokuwa watiifu wake, ni sawa kabisa na kumchezea
sharubu na kumpiga masingi, yaani ule mtindo wetu Uswahilini, wa kusukuma
kichwa cha mtu kwa vidole.
Akiwa pale
Msoga, Bagamoyo, Pwani, JK anaweza kukumbuka jinsi wanaomsema leo kuwa yeye
ndiye alikuwa tatizo kuu katika awamu yake, walivyokuwa wakimnyenyekea na
kumpongeza kwa uongozi uliotukuka.
Anaweza
kukumbuka jinsi watu hao walipokuwa wakipokea simu yake kwa unyenyekevu wenye
nakshi za woga huku wakijiuliza, “sijui mkuu anataka kuniambia nini?” na
katikati ya mazungumzo jibu lao likuwa “ndiyo mkuu… ndiyo mkuu!”
Wazungu
wanao msemo wao kuwa Things Will Never be the Same Again, kwamba mambo hayawezi
kuwa na sura ileile tena. Kwa hiyo wanajua JK siyo rais tena, zama zake
zimeshaondoka, kwa hiyo wanampigia zumari mkuu wa sasa.
Hivi
karibuni, Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga, aliripotiwa akisema kuwa tatizo
la serikali iliyopita ni mkuu wa nchini.
Kwa maana
hiyo, anakosoa aina ya uongozi wa JK kwamba yeye ndiye alikuwa tatizo kuu.
Kauli ya
Kitwanga inaweza kubeba tafsiri chanya au hasi kulingana na mapokeo, ila
ukakasi ulio wazi ni kuwa yeye alikuwa sehemu ya uongozi uliopita, na alikuwepo
kwenye Baraza la Mawaziri la JK mpaka mwisho.
Kwanza
tumuelewe Kitwanga. Alikuwa Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia
kati ya mwaka 2010-2012, akawa naibu pia katika Wizara ya Nchi, Ofisi ya Makamu
wa Rais, Mazingira, kati ya mwaka 2012-2014.
Na kuanzia
mwaka 2014 mpaka JK alipokabidhi rungu la uongozi kwa Magufuli, Novemba 5, 2015
alikuwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini.
Kitwanga
alidumu miaka yote mitano katika awamu ya pili ya JK kwa maono yapi? Ni dhambi
kubwa kwenye uongozi kuhudumia wananchi chini ya mtawala ambaye anakufanya ushindwe
kutimiza maono yako ya kutoa huduma.
Muongozo wa
taaluma ya uongozi, unaelekeza kwa mtu kujiweka pembeni pale anapoona kuna hali
ya kusigana kati ya dhamira yake na ile ya kiongozi wa juu.
Ni busara na
uungwana kujiuzulu, unapoona maono yako au mtazamo ulionao siyo pacha na ule wa
kiongozi wa juu.
Uongozi ni
maono ambayo hujengwa na mtazamo. Ni usaliti wa hali ya juu kwa watu wenye
kusigana mitazamo, kufanya kazi serikalini kama mtu na bosi wake.
Mtu kuwepo
kwenye uongozi ambao hakubaliani nao, kisha akadumu mpaka mwisho, huyo anakuwa
si mtumishi mwenye utashi, bali mtumikia maslahi.
Kwamba
anafanyia kazi maslahi yake, wakati kile anachokifanya na maagizo ambayo
anayatekeleza kama anavyotakiwa na bosi wake, ni kwa shingo upande.
Tafsiri ya
kiongozi mwenye kufanya vitu kwa shingo upande pia ni usaliti. Ama anamsaliti
kiongozi wake wa juu au wananchi wenye kuhitaji kuhudumiwa kwa nyoyo zenye
ukunjufu usio na shaka.
Kitangwa
hakupaswa kuibuka sasa na kusema JK ndiye alikuwa tatizo. Alitakiwa kujiondoa mapema.
Zipo njia nyingi kwa waziri au mteule yeyote kujiuzulu bila kutengeneza rabsha na mkuu wa nchi.
Kama
angesimama leo akasema kuwa JK alikuwa tatizo ndiyo maana alijiuzulu uongozi au
alikataa uteuzi, angekuwa na hoja yenye mantiki, ila anachokizungumza sasa
hakina ladha nzuri masikioni.
Sanasana
anajichonganisha na JK mwenyewe, vilevile anajitafutia uhusika wa ndumilakuwili
ambao siyo mzuri kuwa nao kiongozi kama yeye.
Kiongozi
anapaswa kuwa na msimamo thabiti, na hatakiwi kuwa na kauli zenye viashria vya
kushindwa na visingizio. Alichokisema Kitwanga ni kutaka kujivua kasoro za
utawala uliopita, kwa hiyo anataka JK ndiye atajwe kama tatizo sugu.
Ni dhambi
kubwa kufanya jambo pamoja halafu yakionekana makosa, mtu aibuke aseme tatizo
alikuwa mwenzake. Utendaji wa pamoja unakuwa na matokeo ya kuwajibika kwa
pamoja. Ni utoto kunyoosheana vidole.
Kitwanga
alipaswa kusema “utawala uliopita tulikosea sehemu kadha wa kadha”, siyo
kumvalisha lawama zote JK. Kama aligundua mapema kuwa JK ndiye alikuwa shida,
hakupaswa kukaa barazani mpaka mwisho wa utawala wake.
Kabla ya
Kitwanga, alinukuliwa pia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na
Mazingira, January Makamba akisema: “Serikali iliyopita watu walifanya kazi kwa
mazoea.”
Kimsingi
kumekuwa na hoja za hapa na pale kumsema Rais Kikwete na utawala wake kuwa
ulileta au ulilea matatizo.
Hii kwa
hakika inamuuma Rais Kikwete kwa namna ambavyo anasemwa. Anarushiwa maneno
utadhani hajawahi kuihudumia nchi hii kwa mengi yenye kupaswa kupongezwa na
kupigiwa mfano.
Yote hayo
yanatokea kwa sababu Things Will Never be the Same Again! Ndiyo zama za JK
haziwezi kujirudia tena, hivyo watu wanapata fursa ya kumsema kwa namna
watakavyo.
Mwingine
atasema ili ajioneshe kwa mkuu wa nchi aliyepo kuwa yeye ndiye mwarobaini wa
matatizo ya nchi, kwa hiyo yaliyokwama sababu ni JK.
Bila shaka
hata JK mwenyewe anaumia na kufikiria watu aliowaamini na kuwapa nafasi katika
serikali yake, tena pengine walifanya makosa ya hapa na pale lakini
aliwavumilia. Aliamini anawalea, ila sasa wanamsimanga. Shida ni kwamba hana
jinsi, maana hizi ni zama za Magufuli.
Angekuwa na
nafasi sasa au kama angefunuliwa kabla, bila shaka asingewapa nafasi kwenye
serikali yake wale wote ambao wanamsema kuwa aliharibu.
Ni somo pia
kwa Dk. Magufuli kutambua kuwa watu wanaomuimbia mapambio leo, si ajabu baada
ya mwaka 2020 au 2025 akishakabidhi nchi kwa mrithi wake, atajikuta naye
anasimangwa.
Ushauri
wangu kwa Dk. Magufuli ni kuwa achunge sana msitu wa watu ambao leo hii
wanampamba na kumsifu sana kuwa yeye ndiye kiongozi wa mfano, ikiwemo kumwahidi
kuwa watakuwa naye pamoja daima, ipo siku atakapogeuka atajikuta peke yake.
Kugeukageuka ndiyo zetu binadamu!
0 comments :
Post a Comment