Luqman
Maloto
MWAKA 1992,
ulifanyika Uchaguzi Mkuu wa Angola, hiyo ikiwa ni baada ya miaka 17 ya vita vya
kiraia (Civil War).
Uchaguzi
ulikutanisha vyama 11 lakini mchuano ulikuwa mkali kati ya Chama Tawala, MPLA
na Unita.
Rais Jose
Eduardo dos Santos alikuwa anatetea kiti chake akiwa na MPLA dhidi ya hayati
Jonas Savimbi wa Unita.
Dos Santos
ni Rais wa Angola mpaka sasa, alianza kuongoza taifa hilo mwaka 1979 baada ya
kifo cha shujaa wa wakati wote wa nchi hiyo, marehemu Agostinho Neto,
aliyetawala kati ya mwaka 1975 – 1979 alipofikwa na mauti.
Katika
uchaguzi huo, pamoja na uwepo wa vyama 11 shiriki kwenye uchaguzi, mfumo mzima
ulivibeba vyama viwili (two-party system), yaani MPLA na Unita.
Uchaguzi
ulipofanyika Santos aliongoza kwa asilimia 49 na Savimbi alipata asilimia 40.
Uchaguzi ukatakiwa kurudiwa. Maana katiba ilitaka mshindi atangazwe baada ya
kuzidi asilimia 50.
Uchaguzi wa
mara ya pili (runoff), uliitishwa kati ya Savimbi na Santos ili mmoja aweze
kutangazwa mshindi kwa kupata kura zaidi ya asilimi 50.
Mvutano
ukatokea, Savimbi alitaka mabadiliko kwenye tume kwa sababu alizodai kuwa
Santos aliiba kura. Santos akasisitiza uchaguzi urudiwe hivyohivyo.
Ikawa vuta
nikuvute, mwisho Santos akaamua kujitangaza kuwa rais halali na akatawala bila
ya kuwepo kwa uhalali wa kidemokrasia (democratic legitimacy).
Uamuzi wa
Santos ulikuwa wa kibabe na usiojali damu zisizo na hatia. Pamoja na ukorofi wa
Savimbi, ilikuwa ni jambo jema kusikiliza madai yake na kuyafanyia kazi, kwamba
tume irekebishwe ili uchaguzi uwe huru na haki.
Ikumbukwe
kuwa nchi hiyo ilikuwa imefanya uchaguzi baada ya kusaini mkataba wa kusitisha
vita vya wenyewe kwa wenyewe (Bicesse Accords), ambao Santos na Savimbi
walisaini Mei 31, 1991, chini msuluhishi ambaye ni Serikali ya Ureno.
Mkataba huo
ulisainiwa baada ya vifo vya maelfu ya raia na wengine wengi kujeruhiwa. Zipo
ripoti zinaitaja Angola kuwa taifa lenye watu wengi wenye ulemavu wa viungo kutokana
na athari za vita.
Bila kujali
maelfu ya watu kuendelea kupoteza maisha, wala kuhurumia maelfu wanaoendelea
kupoteza viungo vyao kutokana na kujeruhiwa na mabomu, Santos aliziba masikio,
akaendeleza utawala wake.
Angola
ikarejea tena kwenye vita ya wenyewe kwa wenyewe. Waangola wengi wakazidi kupoteza
maisha na kupata ulemavu. Vita iliendelea mpaka mwaka 2002 Savimbi alipouawa.
Unaweza
kujiuliza; Ni kwa nini Santos na Savimbi hawakufikia mwafaka mwaka 1992 na
kusababisha miaka mingine 10 ya vita? Ubishi wao ulileta matokeo ya vita vya
kiraia Angola kufikisha umri wa miaka 27.
Savimbi
aliuawa, sawa lakini kifo chake hakitoshi kufuta machozi ya damu iliyomwagika
Angola. Wakati huohuo Santos yupo madarakani mpaka leo, kazi yake kuchezea
katiba, anaula tu! Kamfanya mwanaye Isabel Dos Santos kuwa mwanamke tajiri
zaidi Afrika.
Juzijuzi
hapa, Santos na Isabel walitumia zaidi ya shilingi bilioni 4 kumwalika rapa wa
Marekani, Nicki Minaj ili atumbuize kwenye sherehe binafsi ya kiongozi huyo.
Fedha za Waangola zinaendelea kutumiwa vibaya. Santos hajawahi kulipia gharama
za maisha ya Waangola na ulemavu wao, kuanzia mwaka 1992 alipong’ang’ania
uongozi bila ridhaa ya kidemokrasia.
KAMA SEIF
KAMA SHEIN
Ukiona
wanasiasa hawataki kukubaliana maana yake hawajali athari ambazo zinaweza
kutokea kwa kutokukubaliana kwao.
Na tafsiri
ya kutokukubaliana huko ni kuingia kwenye chumba cha majadiliano kila mmoja
akiwa na lake kuwa lazima litimie.
Katika
muongozo wa kitaaluma, majadiliano (negotiations au bargaining) ndiyo huzaa
maridhiano (reconciliation).
Zipo dhana
mbili za majadiliano; Ipo ya mmoja apate mwingine akose (distributive
negotiation), kwamba mnaingia kwenye chumba cha majaliano kuona kwa kutambua
kuwa ni lazima mmoja akose mwingine apate. Katika dhana hii ni vigumu kupata
maridhiano.
Dhana ya
pili ni ile ya kuridhishana ili kila mmoja apate (integrative negotiation).
Kwamba kunakuwa na mvutano wa maslahi kwa kila upande (win-win situation),
hivyo maridhiano yanajengwa kwa mgawanyo sawa au unaokaribiana.
Suala la
Zanzibar ilikuwa ngumu kujengwa na msingi wa majadiliano ya kimlinganyo
(win-win negotiation) kwa sababu Dk. Ali Mohamed Shein anataka uchaguzi
urudiwe, wakati Seif Sharif Hamad anashinikiza atangazwe kuwa Rais wa Serikali
ya Mapinduzi Zanzibar.
Sasa hapo
nani anapate na yupi akose ndiyo kwenye tatizo. Niliwahi kuandika katika makala
yenye kichwa “Shein na Seif atakayekubali kukosa ndiye shujaa” kuwa afadhali
ingekuwa kila mmoja nang’ang’ania alishinda, hapo suluhu kuu ilikuwa ni kurudia
uchaguzi kuondoa ubishi.
Tatizo Seif
akikubali uchaguzi urudiwe atajiona ameshindwa au Shein akikubali Seif
atangazwe atakuwa amekubali kukosa. Ndiyo maana nilisema kuna utata na shujaa
wa maisha na amani ya Wazanzibar ni yule atakayeelekea kwenye hitaji la
mwenzake. Kuvutana hakuna jawabu.
MAMBO YA
KUMULIKA
Suala la
Zanzibar halitaki matamanio ya “lazima niwe rais”, vilevile kuweka misimamo ya
vyama si jambo jema. Ni muda mwafaka kutambua kuwa hali ya sasa inaifedhehesha
Tanzania yetu.
CCM na Cuf
wasijitie upofu wala kujisahaulisha. Machafuko ya Januari 26 na 27, 2001
yalikuwa mabaya mno. Kama nchi hatupaswi kurejea makosa. Watu wafe, wengine
wawe walemavu kwa sababu za ubishi wa wanasiasa.
Kuna idadi
kubwa ya Wazanzibar waligeuka wakimbizi kwa sababu ya machafuko ya Januari
2001. Asiye na aibu wala huruma, anaweza kuona sawa kuendeleza chokochoko
zinazoweza kuleta machafuko kwa mara nyingine.
Hakuna
matakwa na tamaa za wanasiasa, zenye kulingana na thamani ya damu hata ya mtu
mmoja. Seif na Shein waelewe kuwa Zanzibar ni muhimu kuliko wao.
Watambue
kuwa Cuf na CCM siyo vyama vya siasa kama amani na mfumo wa kisiasa haupo.
Palipo na machafuko hakuna siasa, kuna vikundi vya mapigano na uasi. Vyama
vinafuata baada ya amani, usalama na utulivu.
Hali ya
Zanzibar ilipofikia, muhimu kwa sasa siyo nani ni rais, bali maridhiano yenye
tija, yatakayoviacha visiwa hivyo vikiwa na amani na upendo.
Muhimu
kuonya hili; Kama inavyofahamika kuwa Zanzibar hakuna siasa bali kuna chuki.
Uamuzi ambao hautakuwa na maridhiano, utaongeza uhasama na uadui.
Pemba kwa
sehemu kubwa hawaitaki CCM. Na kwa miaka 20 sasa tangu Uchaguzi Mkuu 1995, hali
imekuwa hivyo.
Madai ya Zec kama yalivyosemwa na Mwenyekiti
wake, Jecha Salim Jecha, dosari nyingi zilitokea Pemba. Ipo shaka kubwa hapo!
Kama bila
shaka yoyote kuwa Wazanzibar kwa kura nyingi wamemchagua Seif, CCM wakubali tu
hata kama wanaona chaguo ni baya. Waachwe Wazanzibar wenyewe watajutia uchaguzi
wao kama wamekosea. Ni kosa kuwalazimisha. Ni uamuazi wao!
Uchaguzi
unapofanyika mshindi hupatikana kwa njia ya hesabu ya kura. Uamuzi umeshafanywa
na wananchi kwenye masanduku ya kupigia kura.
Kwa
kuzingatia ukweli huo kuwa uamuzi ni ule ambao ulifanyika kwenye masanduku ya
kura, ndiyo tunakuwa na majibu kuwa vikao vinavyoendelea kwa sasa vinafanyika
baada ya makosa.
Kwamba Zec
kama wakosaji wakuu, Cuf na CCM wanafuata kwa upande wa pili katika kila kosa.
Kama kweli
uchaguzi ulikuwa na dosari, maana yake Cuf wanahusika kwa kushirikiana na
maofisa wa Zec.
Ikiwa
hakukuwa na dosari, maana yake CCM watakuwa walikataa kushindwa, hivyo kumpa
shinikizo Jecha afute matokeo na kuitisha marudio ya uchaguzi.
Jinsi hali
ilivyo sasa na misimamo ya vyama, inataka mtu mkweli na mwenye hofu hasa ya
Mungu, kusimama na kukiri makosa ya upande wake ili amani ichukue mkondo wake.
Mwandishi na
Mwanahistoria mashuhuri nchini Marekani, Timothy B. Tyson, alisema: “If there
is to be reconciliation, first there must be truth.”
Kiswahili:
Kama yatafanyika maridhiano, ukweli lazima utangulie.
Mkazo hapo
ni kuwa kama pande mbili zinazosigana kuhusu mgogoro wa Zanzibar
hazitatanguliza ukweli, hayo maridhiano hayatakuwa na maana yoyote.
Hapohapo
vema kuwakumbusha kwamba hali imefika kwa kiwango cha sasa kwa sababu ya
kukosekana kwa ukweli. Wanasiasa wanajiwekea ulazima kinyume na matakwa ya
wananchi.
Isingekuwa
“lazima mimi” au “lazima sisi”, Zanzibar isingefika ilipo leo. Makubaliano ya
kweli yatapatikana kama wataweka utaifa mbele, siyo vyama.
Waziri Mkuu
wa zamani wa Australia, John Malcolm Fraser, aliwahi kusema kuwa maridhiano
hayapatikani pasipo kuwepo kwa mabadiliko ya kimsingi ndani ya pande zenye
kusuguana.
Fraser
aliyefariki dunia Machi 20, mwaka huu, alisema: “Reconciliation requires
changes of heart and spirit, as well as social and economic change. It requires
symbolic as well as practical action.”
Kiswahili:
Maridhiano yanahitaji mabadiliko ya moyo na roho , vilevile mabadiliko ya
kijamii na kiuchumi. Yanahitaji ishara vilevile utekelezaji wa kivitendo.”
Mazungumzo
kuhusu maridhiano yanapasa kuhusisha pande mbili ambazo wahusika wake wanakuwa
na nyoyo rahisi kwa mabadiliko (flexibility).
Maridhiano
ya Zanzibar ni ndoto kama wahusika wa mazungumzo wanakuwa na nyoyo ngumu zisizo
na hali ya utayari kwa ajili ya mabadiliko (stiffness).
Mazungumzo
yatakuwa mepesi na maridhiano itakuwa rahisi kupatikana kama Seif na Shein
pamoja na pande zao (vyama vyao), wataweka maslahi ya Zanzibar na Tanzania
mbele. Wao kama walivyo binadamu wengine katika zama hizi, wataondoka, Zanzibar
itaendelea kuwepo.
Maridhiano
hayatachukua njia ndefu kufikiwa kama Shein na Seif pamoja na vyama vyao,
wataanza kwa kujiuliza nini Wazanzibar wanataka.
Matakwa ya
Wazanzibar yatazamwe kuanzia katika kuchagua, uamuzi wao ulikuwaje? Na je,
wanataka uchaguzi urudiwe au matokeo ya mchakato wa Oktoba 25 yatangazwe? Ni
busara na uungwana wa hali ya juu kuheshimu hisia na mahitaji ya Wazanzibar.
Mkondo wa
maridhiano utakuwa wenye thawabu nyingi kutoka kwa Mungu kama mazungumzo ya
mwafaka yataweka mbele hatma ya Wazanzibar kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Kinyume chake ni dhambi kubwa.
Kama Seif
alishinda, asifanywe kuwa mfalme wa huzuni (king of sorrow) katika kila
uchaguzi, mnyonge anyongwe lakini haki yake apewe. Na Shein kama ameshindwa, ni
uungwana kukubali matokeo, asijigeuze mfalme wa uonevu (king of intimidation).
Seif pia awe
mkweli, kama uchaguzi ulitawaliwa na dosari nyingi, hakuna sababu ya
kung’ang’ania ushindi wenye kasoro. Labda kama anapenda urais hata bila uhalali
(legitimacy).
Ni kuhusu
ukweli na haki, Shein na Seif kila mmoja anayo nafasi nzuri ya kujenga heshima
yake kwa vizazi vya sasa na vijavyo. Atajwe kuwa shujaa hasa wa siasa za
Zanzibar na Tanzania kwa jumla.
Uungwana na
uvumilivu wa Seif nautambua. Ni mwanasiasa wa mfano. Shein amekuwa na rekodi ya
upole na ustaarabu bila makuu. Kila mmoja atambue sifa yake njema inayombeba.
Asikubali kuipoteza sasa, kwani ni sawa saumu kuifungulia alasiri inayoishia.
KOSA KUBWA
AMBALO LINATAKA KUFANYIKA
Majadiliano
ni wazi yamekufa, na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi
alianza kwa kumweleza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Zanzibar
kuna amani na wananchi wanasubiri tarehe ya uchaguzi.
Kisha
Mwenyekiti wa Zec, Jecha Salim Jecha alitangaza kuwa Uchaguzi Mkuu wa Marudio
Zanzibar ni Machi 20, mwaka huu.
Kauli hizo
ni kosa kubwa la kiufundi. Kinachotaka kufanywa ni ubabe ambao hautakuwa na
matokeo mazuri siku za usoni.
Unaweza
kulazimisha kama ambavyo Balozi Iddi na Jecha walisema katika mazingira ya
mfumo wa ukiritimba wa chama kimoja (one-party dominant system), Zanzibar kwa
sasa ni mlinganyo wa vyama viwili (two-party system) kati ya CCM na Cuf.
Hata kama
machafuko yatadhibitiwa kwa nguvu kubwa ya dola, lakini uchaguzi utasusiwa kwa
asilimia kubwa kama tu Seif na Cuf watashikilia msimamo wao wa kutoshiriki
uchaguzi.
Bila shaka
yoyote uchaguzi utafanyika (CCM wakiamua), na kwa vile Seif atasusa, ni uhakika
kuwa Shein atashinda kiurahisi. Itaitwa ushindi wa kishindo lakini haitakuwa
awamu nzuri ya uongozi kwa maana Wazanzibar wengi watasusa.
Mwenyekiti
wa Nec, Jaji Damian Lubuva alisema juzi kuwa tume haipaswi kuingiliwa, kwamba
hatma ya Zanzibar iachwe kwa Zec.
Lubuva
anapaswa kutambua kuwa suala la Zanzibar linahitaji maridhiano kuliko uamuzi.
KOSA LA SEIF
Msingi wa
majadiliano, kitaaluma na kimkakati, huundwa na pande tatu kisha kushika mambo
mawili.
Mosi; Usuluhishi
(mediation), hapo huwa ni mazungumzo ya kawaida na kupeana maneno matamu na
kuridhishana ili kila upande utoke umeridhika.
Pili; Uamuzi
(arbitration), huambatanisha vielelezo, ushahidi, haki na sheria kisha uamuzi
hufanyika kutokana na ushahidi, vilevile tafsiri za kisheria.
Mazungumzo
ya mgogoro Zanzibar yaliyokwama, sababu yake ni kukosekana kwa upande wa tatu,
vilevile usawa haukuwepo.
Seif alikuwa
mjumbe pekee katikati ya msitu wa wajumbe wa CCM. Usawa upo wapi?
Seif
anachuana na Shein lakini Shein ndiye akawa mwenyekiti wa majadiliano.
Nilitegemea kukwama kwa mazungumzo mapema mno.
Kama dhamira
ya kweli ilikuwepo, ilitakiwa Seif awe na timu yake, vilevile Shein na wenzake
kisha uwepo upande wa tatu ambao ungekuwa unasikiliza na kushauri. Hilo
halikufanyika. Seif alikubali kushiriki mazungumzo ya aina hiyo.
NINI
KIFANYIKE?
Kama kweli
Seif na Shein wanaipenda Zanzibar, basi warudi upya kwenye majadiliano ambayo
yatajengwa kwa usawa na yashirikishe pande tatu. Yaani kuwepo na upande mmoja
ambao siyo sehemu ya mgogoro na hauna maslahi yoyote kwenye mgogoro.
Vilevile
Zec, kama wahusika wa kuharibu uchaguzi nao wahusike. Mazungumzo yafanyike kwa
mjadala huru bila kuweka mbele hisia ili kupata suluhu.
Wafahamu
kuwa majadiliano siyo mchezo kuambulia sifuri (zero-sum game), lazima maslahi
ya kila upande yavutwe katikati kisha maridhiano yatokee.
Kikubwa
zaidi wote wawe wa ukweli. Na lazima tuombe ukweli ushinde matakwa. Katika
sintofahamu ya Zanzibar, ukweli hasa ni upi? Je, Seif alishinda au uchaguzi
ulivurugwa? Kisha ukweli ushinde matakwa na kuleta maridhiano.
Mungu
Inusuru Zanzibar.
Mungu
Ibariki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
0 comments :
Post a Comment