Luqman
Maloto
JIWEKE
karibu na Mungu unapotaka kufunga ndoa. Omba mwenzi sahihi ambaye ataleta
msisimko wa mafanikio katika maisha yako.
Hata siku
moja usije ukapuuza kuwa mwenzi wa maisha yako ni lazima aendane na maono yako.
Hutakiwi kupishana na mwenzi wako katika maisha ya ndoa.
Ndoa bora ni
ile yenye nuru. Ile iletayo mabadiliko ya kimaisha. Ulikuwa peke yako, kwa hiyo
mnakuwa wawili, hivyo kipato kinaongezeka.
Mawazo ya
wawili si sawa na wazo la mmoja. Na hiyo ndiyo imekuwa sababu ya mafanikio
makubwa kwa familia ambazo mume na mke wanaishi kwa maelewano makubwa.
Chukua
pointi hii; Kati ya sababu mbalimbali ambazo zinaweza kumfanya mtu ashindwe
kufanikiwa maishani, kubwa zaidi ni kukosea kuchagua mwenzi wa maisha.
Unahitaji
mwenzi mpenda maendeleo na aliye na nidhamu ya maisha. Mbunifu anayewaza mbali.
Mwelewa na mwenye kukutia moyo ili uzidi kuyasogelea mafanikio.
Muhimu zaidi
ni awe unaeyeendana naye. Maelewano yalete raha ndani ya ndoa na kila mmoja
ajione yupo salama dhidi ya mwenzake.
Yote
yanaweza kufaa lakini utamu wa ndoa hudhihirika pale mume na mke wanapokuwa
marafiki wakubwa. Wanazungumza na kubadilishana mawazo vizuri. Wanafanya
mizunguko yao pamoja. Kila mtu anakuwa huru kuzungumza neno lake kisha mwenzake
anasikiliza na kupokea.
Doris Fisher
ni mwanamke shujaa. Mawazo yake mazuri yameweza kuitetea familia yake na
kuifanya isimame kifua mbele duniani.
Hata hivyo,
asingefanikiwa au kupata heshima aliyonayo sasa hivi kama yeye na mume wake wasingekuwa
na maelewano.
Doris ni
tajiri, ni bilionea kwa dola na Kitanzania ni trilionea wa shilingi. Tumbo lake
lilibeba watoto watatu ambao sasa ni mababa na wote ni matajiri wakubwa.
Jarida
maarufu la Forbes ambalo linaheshimika kwa utafiti na utoaji wa takwimu
mbalimbali ulimwenguni, linamtaja Doris kuwa mmoja wa wanawake 100 wenye nguvu
zaidi duniani.
Doris ndiye
mama wa Kampuni ya The Gap, Inc. ikizoeleka zaidi kama Gap Inc. ambayo ni
maarufu ulimwenguni kwa utengenezaji na uuzaji wa mavazi kwa jumla na rejareja.
Toa heshima
kwa Gap kama kampuni ambayo takwimu za mwaka 2014 ziliitaja kuwa na waajiriwa
135,000. Vilevile mtandao wake wa kutengeneza ajira ulimwenguni kote ni mkubwa
mno.
Ipe heshima
Gap kwa sababu takwimu zinaonesha kuwa mwaka jana, kampuni hiyo ilitengeneza
mapato ya dola bilioni 16.148 ambazo ni sawa na shilingi trilioni 34.377.
Bajeti ya
Tanzania kwa mwaka wa fedha 2015-2016 ni shilingi trilioni 23. Hivyo, mapato ya
Gap kwa mwaka mmoja yanatosha kuendesha serikali ya nchi yetu na chenji ya
kutosha.
Fanya hesabu
ya harakaharaka, unapata shilingi trilioni 11.377 ambayo inabaki na hiyo inatosha
kulifanya Jiji la Dar es Salaam kujaa barabara za juu (overpass) ambazo kwa
lugha ya Kijumuiya ya Madola, zinatambulika zaidi kama flyover.
Kama Doris
ameweza kufanikisha matokeo hayo, ni kwa nini asiitwe shujaa? Ongezea pointi
hii kwamba mwanaume yeyote mwelewa anapompata mwanamke kama Doris lazima
afanikiwe.
Ipo ile
kanuni yangu kuwa Mke Bora + Mume Mwelewa = Familia Tajiri. Doris alikutana na
mumewe mwenye uelewa hasa, hivyo kutengeneza utajiri ambao unaitikisa dunia
hivi sasa.
Doris
alikuwa mke wa Donald Fisher ambaye alifariki dunia Septemba 27, 2009. Walikuwa
wakiishi kawaida tu. Lakini maisha yao yalitawaliwa na upendo wenye kuthibitika
ndani ya mioyo yao na kuonekana machoni kwao.
Kutokana na
upendo huo, walijadiliana aina ya mavazi na vipimo, vilevile walikwenda kwenye
manunuzi pamoja.
Kwa vile
walikuwa karibu mno, ilikuwa rahisi hata kujadiliana changamoto zao kwa
ukaribu.
Walipokuwa
wananunua nguo, waligundua kwamba kupata jeans ya vipimo vyao ni tatizo. Maana
walikuwa wakihangaika sana.
Doris
alifanya utafiti na kugundua kuwa tatizo la vipimo vya jeans halikuwa lao tu,
bali liliwagusa wengine wengi.
Kupitia
changamoto hiyo, Doris alipata wazo la kuanzisha kampuni ya kuuza mavazi yenye wigo
mpana wa vipimo ili kila mtu aweze kuvaa nguo nzuri bila bughudha wala
masharti.
Alikaa na
mumewe (Donald), wakajadiliana kuhusu wazo hilo, wakakubaliana vizuri lakini
mume akawa na wasiwasi, Doris akamwambia inawezekana.
Wazo kuu
ambalo Doris alikuwa nalo ni kuhakikisha kampuni yao inakuwa na vitu mbalimbali
vya mauzo ya nguo, vikiwa katika vipimo tofautitofauti ili kurahisisha kila mtu
kupata vazi la ‘saizi’ yake.
Doris
alikuwa na wazo la baadaye kwamba kampuni yao ikishakuwa watakuwa wanauza
mavazi yenye nembo (chata) zao. Lakini kwa kuanzia, ilibidi waingize sokoni
chata za wengine.
Kutokana na
uwezo wao kuwa mdogo, walianza kudunduliza fedha ili wapate uwezo wa kufungua
vituo vya mauzo ya Gap. Walifanikiwa kukusanya kiasi cha dola 63,000.
Walipopata
fedha hizo, ndiyo ikawa mwanzo wa kuukimbilia utajiri kwa kasi ya juu mno. Kasi
ambayo imesababisha mapinduzi makubwa kwa upande wa mauzo ya nguo ulimwenguni.
Agosti 21,
1969, Doris na Donald walifungua kituo cha kwanza cha mauzo ya mavazi ya Gap,
eneo la Ocean Avenue, San Francisco, Marekani na kupata mafanikio ya
harakaharaka.
Kwa vile
hawakuwa na chata ya kuisimamia, walinza mauzo kwa kufanya makubaliano na
kampuni ya Levi's pamoja na LP records. Katika mwaka wa kwanza tu, walipopiga
mahesabu, waligundua kumbe walichelewa mno kuanzisha biashara hiyo, kwani
inalipa vizuri kabisa.
Mwaka wa
pili wa biashara, waliweza kufanya mauzo yenye thamani ya dola milioni 2,
ambazo ukibadili kwa sarafu ya shilingi kutokana na thamani ya sasa, utapata
zaidi ya bilioni 4.
Ikabidi
waanze kujitanua. Mwaka 1970 baada ya kuuza mavazi kwa dola milioni 2, Gap
iliongeza kituo cha pili mjini San Jose, California.
Mwaka 1971,
Gap ilitambulisha makao makuu yake mjini Burlingame, California, ikiwa na
wafanyakazi (waajiriwa) wanne tu. Hapa ni kuona namna ambavyo watu huanza
mbali.
Mwaka 1973, tayari
kampuni ilikuwa imeshakuwa zaidi, kwani iliweza kumiliki vituo zaidi ya 25.
Kutanuka huko kuliweza kufika mpaka Pwani ya Mashariki (East Coast).
Ndani ya
East Coast, walifungua kituo kikubwa kwenye jengo la biashara la Echelon Mall, Voorhees,
New Jersey.
Ilipofika
mwaka 1974, Gap ilianza kuuza mavazi yenye nembo yake yenyewe.
Kimsingi
ukuaji huo wa Gap ni kutokana na juhudi za Doris. Kwamba hakuishia tu kutoa
wazo, alihakikisha anashirikiana vizuri na mume wake, hivyo kuishinda shere ya
umaskini.
Hapo
unapaswa kuzingatia kuwa Doris ndiye hasa mbunifu wa wazo la kuuza mavazi.
Hakuishia hapo, alishiriki kutafuta mtaji na walikuwa bega kwa bega kuhakikisha
kila kitu kinakuwa sawa.
Pointi hii
inampambanua Doris kama mwanamke kichwa. Na ndiyo maana tumbo lake pia limebeba
watoto matajiri leo hii. Baba na mama matajiri, watoto wanapita njia hiyohiyo,
hakuna aliyetoka kwenye mstari.
Mafanikio ya
wanaye, unaweza kuyachukua na kumjaza Doris kama mama mlezi bora. Familia
nyingi hukosa msimamo kutokana na malezi ya watoto.
Hili
liongezee kuwa Doris ni mama bora, msaka fedha mwenye kiu. Zaidi ya yote ni
mama anayejitambua.
Doris akiwa
mkurugenzi, Donald akiwa mwenyekiti wa Gap, walifanya kazi kubwa mno ambayo
imewafanya wote wawe mashujaa.
Kama
isemavyo Biblia Takatifu katika Mithali 13:22: “Mtu mwema huacha akiba kwa wana wa wanawe.”
Mantiki hapo
ni kuwa mtu mwema huwa anaacha urithi kwa wanawe na wana wa wanawe, yaani baraka
za wema wake zinaweza kufikia hadi kwenye kizazi cha wanawe.
Huo ni
muongozo wa maandiko kuwa kila mtu ni lazima atafute mali na aziache ili
wajukuu wake waje kuziona. Huo ndiyo msingi bora wa maisha kwa kila mmoja.
Na kwa hoja
hiyo, Doris ameweza kuwa mtu bora hata katika maandiko maana amefanikiwa kuacha
utajiri mkubwa ambao wanaye na wajukuu zake wanaufaidi.
Gap ilikuwa
chini ya Donald na Doris tangu kuanzishwa kwake mwaka 1969 mpaka mwaka 2004,
walipokabidhi mamlaka kwa mtoto wao mkubwa, Robert Fisher, akijulikana zaidi
kama Bob Fisher.
Robert akiwa
mwenyekiti wa Gap, Donald na Doris walibaki ndani ya bodi ya wakurugenzi,
wakihusika zaidi katika ushauri, lakini masuala yote ya uongozi kiutendaji
waliyaacha kwa Bob na watoto wao wengine.
USHUJAA WA
DORIS
Kwa kuweka
rekodi sawa, ushujaa wa Doris unaonekana katika mambo matatu, ambayo ni ubunifu
wake, kufikiria kama tatizo walilokuwa nalo la kupata jeans zenye kuwatosha
linaweza kuwa mtaji wa wao kugeuka wawekezaji wakubwa katika soko la mavazi.
Pili ni
kusimama kwake kama mama, kwamba alitambua wajibu wake kama mke ni kumuweka
mume wake karibu, kuwa marafiki na ndiyo maana waliweza kushauriana mambo hayo
ambayo yamegeuka faida kubwa kwao.
Tatu ni
usimamizi wa fedha na uongozi. Doris akisimama kama mkurugenzi mtendaji wa Gap,
alikuwa kiungo muhimu kuhakikisha kila kitu kinakwenda sawa kulingana na
malengo.
Hata Donald
kabla hajafariki dunia, aliwahi kukaririwa akisema: “Mafanikio ya Gap ni Doris,
ni mke bora. Ni mama wa familia na ni mama wa Gap. Tusingepata mafanikio haya
kama tusingekuwa pamoja kama mke na mume.”
Doris katika
moja ya nukuu zake anasema: “Mwanamke mzuri na una akili nzuri unapompata
mwanaume mzuri ni kwa nini usiwe bilionea? Bahati kubwa katika maisha yangu ni
kwamba nimeolewa na mwanaume muungwana.
“Ningekuwa
wa ajabu sana kama nisingefanikiwa wakati nipo na Donald. Hiyo pia ipo kwa
Donald, angekuwa mtu wa hovyo kama asingetajirika wakati yupo na mimi. Hiyo ni
kumaanisha kuwa mafanikio kwa familia yanatokana na aina ya wahusika.”
Kingine
ambacho amewahi kukizungumza ni hiki: “Mume na mke lazima washirikiane,
wazungumze mambo mbalimbali. Kila mmoja ajione yupo huru kusema chochote mbele
ya mwenzake.
“Uhuru ambao
watu hupeana ndiyo hurahisisha mafanikio ya pamoja, maana mtu akiwa na wazo
anajisikia huru kumshirikisha mwenzake kama mtu wa kwanza kabla ya mwingine
yoyote.”
CHUKUA HII
Mke na mume
ambao hawatenganishwi na chochote katikati ni wale ambao nyoyo zao zipo karibu. Mtu anaweza kuwa
Bosnia na mwenzake Somalia lakini wakawa karibu sana moyoni.
Siku zote
jitahidi kumuweka mwenzi wako karibu moyoni, siyo ukaribu wa miili. Kama
hujamuweka moyoni, hata umuweke karibu kiasi gani, mafanikio hayatakuwepo.
Wanandoa na
wapenzi ambao wamekuwa karibu moyoni wamekuwa na mafanikio makubwa kimaisha na
kiuhusiano lakini wale wenye ukaribu wa viwiliwili, hupata usumbufu mkubwa
kwenye maisha yao.
MIZIZI YA
DORIS
Doris ana
umri wa miaka 84 hivi sasa. Watoto wake wote ni watu wazima. Kila mmoja ana
familia yake nzuri. Na hapo ndipo unapoweza kuona matunda ambayo Doris aliyaweka
kwenye maisha yake na kizazi chake chote.
Mtoto wake
wa kwanza, Bob ndiye bosi mkuu wa Gap. Amekuwa na mikoba ya usimamizi wa mali
zote kwa niaba ya familia yao.
Kutokana na
majukumu hayo, Bob amekuwa akipata mshahara mkubwa lakini wakati huohuo akibaki
mwana hisa wa Gap, kama ilivyo kwa ndugu zake wengine.
Bob
alizaliwa Agosti 26, 1954, ana umri wa miaka 61 kwa sasa. Na alianza kukuzwa
kibiashara na uongozi wa kampuni na wazazi wake tangu akiwa kijana mdogo
kabisa.
Mwaka 1990,
Bob akiwa na umri wa 36 aliteuliwa kuwa mkurugenzi wa kampuni, kipindi ambacho
Doris alianza kujipunguzia majukumu ya kiutendaji ili kuyakasimisha kwa watoto
wake.
Wakati
akiandaliwa kuwa mkuu wa kampuni baada ya wazazi wake, Bob aliteuliwa kushika
nafasi mbalimbali. Na alikuwa mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi kati ya mwaka
2004-2007 kabla ya kuwa mwenyekiti wa kampuni nzima kiutendaji (mwenyekiti
mtendaji).
Mtoto wa
pili wa Doris ni William Fisher, alizaliwa mwaka 1958, umri wake ni miaka 57. Ni
mkurugenzi wa Gap tangu mwaka 2009. Kutokana na mafanikio ambayo ameyapata,
aliamua kuanzisha kampuni nyingine inayoitwa Manzanita Capital Limited.
Katika
kampuni hiyo ya Manzanita, William ndiye ofisa mtendaji mkuu. Hii inamfanya
kuwa na majukumu makubwa, kwani Manzanita ni kampuni kubwa ambayo inajihusisha
zaidi na uwekezaji wa masoko katika biashara mpya, utafiti na ushauri kwa
wajasiriamali.
Mtoto wa
mwisho wa Doris ni John Fisher ambaye alizaliwa Juni Mosi, 1961. Huyu naye ni
mfanyabiashara. Ni mmoja wa wajumbe katika bodi ya wakurugenzi ya Gap.
Hata hivyo,
John amekuwa akisaka mafanikio ya peke yake na kutokana na gawio ambalo hupata
kutokana na biashara za Gap, ameweza kuwekeza kwenye michezo na kwa sasa ni
mmoja wa wamiliki wa Klabu ya Oakland Athletics inayoshiriki Ligi Kuu ya Baseball
nchini Marekani.
John pia ni
mmoja wa wamiliki wa Klabu ya San Jose Earthquakes, inayoshiriki Ligi Kuu ya
Soka ya Marekani. John vilevile ni mwanahisa mkubwa katika Klabu ya Soka ya
Celtic inayoshiriki Ligi Kuu ya Scotland.
Ukiangalia
umri wao wote, unaona kuwa watoto wa Doris tayari wana wajukuu. Hivyo, hata
kesho Mungu akimchukua, atakuwa amefanikisha kuacha utajiri ambao umeweza
kuonwa mpaka na wajukuu wa watoto wake.
Kwa maana
hiyo, amezidi ule ubora ambao Mungu ameuweka kwa wanadamu kama ilivyoelezwa
kwenye Mithali 13:22, kuwa mtu bora huwaachia urithi wana wa watoto wake,
lakini yeye amefikisha mpaka wana wa wajukuu zake.
CHUKUA MTAJI
HUU
Kutoka kwa
Doris, unachotakiwa kushika ni kuwa hakikisha unatafuta mwenzi bora wa maisha
yako ambaye mtasikilizana. Mfanye kuwa mshirika wako wa kwanza. Jadiliana naye
mambo ya mafanikio pamoja na mawazo mapya.
Lile wazo
ambalo mtaona linafaa, hakikisha mnalipa kipaumbele na mnashirikiana
kufanikiwa. Mke bora siku zote huonekana ndani ya mafanikio yake binafsi na
hata yale ya mume wake.
Iwe ni
mafanikio binafsi au ya mume, au ya wote, hesabu ni mafanikio ya familia. Hivyo
basi hakikisha mnashirikiana inavyotakiwa ili kujenga maisha yenye kuonesha
ushujaa wako. Doris ni mama shujaa!
0 comments :
Post a Comment