Luqman
Maloto
MABADILIKO
chanya katika maisha yana raha sana. Kutoka ufukara kwenda utajiri, daraja la
chini kikazi na kupanda cheo, raia wa kawaida hadi kuwa kiongozi, upweke na
kupata mwenzi au mtoto. Hayo na mengine mengi ni mambo yanayosimulika kwa
urahisi sana!
Mabadiliko
hasi ni maumivu na simulizi zake kwa kawaida siyo zenye kutoka kwa wepesi.
Fikiria tajiri mjivuni aliyegeuka fukara, bosi mpenda sifa kushushwa cheo,
kiongozi mwenye makeke kunyimwa kura na mengineyo.
Naomba
tuzungumze biashara rahisi lakini yenye mtaji mkubwa, inayoweza kukufanya
ufurahie maisha yako yote. Biashara isiyo na majuto. Hata siku moja
haitakufanya ujilaumu kuifanya. Biashara yenyewe ni uwekezaji kwa mtoto. Wekeza
kwa mwanao kisha utaona jinsi maisha yanavyoweza kubadilika kwa kasi.
Ni suala la
kuvumilia mwanzoni tu, jikaze na umlee kwa imani. Ukipata nafasi ya kuzungumza na Gloria Marie
James, atakwambia raha za kuwekeza kwa mtoto. Yeye ameweza kuyafanya maisha
yake kubadilika kutoka sifuri hadi kuchezea mamilioni ya fedha kwa siku.
Anatumia, mwanaye anazo!
Gloria ni
mama wa staa wa kikapu katika Ligi ya NBA, LeBron James. Maisha ya kumkuza
mkali huyo wa kuteleza kwenye marumaru za uwanja wa kikapu (basketball court)
hayakuwa rahisi hata kidogo. Msisitizo; hayakuwa rahisi kabisa.
Hata hivyo,
Gloria aliamini mwanaye ndiye mkombozi wake, akapambana kumtengenezea barabara
ya kupita. Hakika amefanikiwa, kutoka dhiki za kuwaza japo mlo wa siku, leo
anakoga mapato kutokana na ingizo kubwa la mamilioni ya mwanaye katika kikapu.
Akaunti
benki inafoka dola za Federal Reserve System (FRS), yaani Benki Kuu ya
Marekani. Umri unasogea lakini ndiyo kwanza vijana wanamuona mrembo mbichi. Analipa
kutokana na matunzo. Hana dhiki, mahitaji yote yapo ndani ya uwezo.
ALIKUWA
MTOTO AKAZAA MTOTO
Anayefikisha
umri wa miaka 18 ndiye anatambulika ametoka hatua ya utoto na kuhamia utu
uzima. Gloria alinasa ujauzito akiwa na umri wa miaka 16 tu. Pamoja na hali
hiyo, alijisimamia ipasavyo kumlea mwanaye.
Hakuwa na
mpenzi wa kueleweka, ila sanaa tu za ujana na mapenzi ya kujifurahisha ndiyo
yaliyomfanya anase. Alimjua mwanaume aliyempa ujauzito lakini hakuweza
kushirikiana naye kwenye malezi.
Pamoja na umri
mdogo aliokuwa nao, Gloria hakutaka kumuwazia mwanaume aliyempa ujauzito. Alijiaminisha
tu kuwa mwanaume huyo ni baba wa bahati mbaya, kwa hiyo aliamua kujihesabu yeye
kama baba na mama wa LeBron.
Hata LeBron
mwenyewe amekuwa akikiri mara nyingi kwa kuandika kwenye mitandao ya kijamii
hasa Instagram: “Mama yangu ndiye kila kitu kwangu. Yeye ndiye baba na ndiye
mama yangu.”
Gloria
anamtaja baba wa LeBron kuwa ni Anthony McClelland na katika mara chache ambazo
amemzungumzia, alisema tu kwa kifupi: “Alipogundua tu nina ujauzito alikimbia,
hakutaka kuniona tena.”
SHURUBA ZA
MALEZI
Kwanza
Gloria anastahili pongezi kwa sababu sheria ya nchi yake (Marekani), ilikuwa
inampa ruhusa ya kutoa mimba kutokana na umri mdogo.
Kwa wakati
huo, watoto waliopata ujauzito, walihesabiwa ndani ya kapu moja na wale wenye
matatizo ya kujifungua, hivyo kupewa ruhusa ya kutoa mimba. Hata hivyo, Gloria
aliamua kuitunza na kuzaa. Na Mungu alimsimamia hatua kwa hatua.
Mama wa
Gloria, yaani bibi yake LeBron, Freda James alikuwa karibu kusaidia mjukuu wake
anapata kilicho bora. Na kwa vile umri wa Gloria ulikuwa mdogo, mara nyingi
alikaa pembeni akitazama mwanaye akihudumiwa na Freda.
Gloria akiwa
na umri wa miaka 19, wakati huo LeBron akifikisha miaka mitatu ya kuzaliwa,
Freda alifariki dunia ghafl kwa shambulio la moyo. Ni hapo ndipo hali ilikuwa
mbaya kupita kiasi.
Miezi
michache baada ya kifo cha Freda, Gloria alinyang’anywa nyumba aliyoachiwa na
mama yake, hivyo kuanza kutangatanga kutafuta hifadhi yake na mtoto wake.
Kupata
chakula chake na cha mtoto wake ilikuwa shida, malazi ikawa kituo cha
manyanyaso. Mavazi kwa kuombaomba.
Pamoja na
shida zote hizo, kuishi bila uhakika wa kupata chakula, sehemu ya kulala wala
kuvaa, hakuwahi kumuona LeBron ni mzigo. Na kwa msimamo huo, Mungu amemuangazia
nuru ya aina yake.
AMUOMBEA
HIFADHI LEBRON
Kwa kupigana
huku na huko, mama yake LeBron alijitahidi akapata chumba kimoja cha kupanga.
Miaka ikawa haisogei kutokana na ujazo mkubwa wa dhiki uliokuwa unawaandama.
Pamoja na
hivyo, ilifika kipindi LeBron alifikisha umri ambao haikuwa heshima kuendelea
kuchangia chumba na mama yake. Ni hapo Gloria aliamua kumuombea hifadhi
mwanaye.
Gloria
alikuwa na ndoto za kumfanya LeBron kuwa mwanamichezo mkubwa. Na katika umri wa
miaka tisa, alikuwa anafundishwa soka na kocha malum. Gloria alimuomba kocha
huyo msaada wa kuishi na LeBron katika kipindi akihangaika kutafuta fedha za
kumuwezesha kupanga nyumba yenye vyumba viwili.
Mbali na
suala la kupata nyumba yenye vyumba viwili, sababu kubwa ambayo Gloria aliitoa
ni kuwa LeBron kwa hatua aliyofikia, alihitaji kujengwa zaidi kimchezo na
kihuduma, mambo ambayo yalikuwa nje ya uwezo wake.
Alisema, kwa
kuwa mbali na LeBron kipindi anaishi na kocha wake, alilenga kujipanga ili
apate uwezo wa kumhudumia mtoto wake yeye mwenyewe.
Katika
kufafanua sababu ya kumpeleka LeBron kwa kocha, Gloria alimwambia mwanaye:
“Ulikuwa uamuzi mgumu. Tambua ilikuwa ngumu lakini najua haikuwa kwa ajili
yangu. Ilikuwa kwa ajili yako. Nililazimika kukuweka wa kwanza.”
Kocha wa
LeBron, Frank Walker ‘Big Frankie’ hakumuangusha Gloria, alimlea LeBron vizuri
na kupata kila sapoti ambayo aliona anastahili katika kumkuza ipasavyo
kimichezo.
LeBron
anazungumzia hali hiyo ya kuhamishiwa kwa kocha Big Frankie kama sadaka kubwa
iliyofanywa na mama yake. Anasema: “Alihitaji nipate utulivu, na kweli kwa
mwaka mmoja ndani ya nyumba ya Big Frankie kwa mwaka mzima niliishi nyumba
moja, nililala kwenye kitanda kilekile, nikasoma shule ileile, tofauti na
mwanzo nilipokuwa nahamahama kwa kukosa msimamo wa kimaisha.
“Mama
alitaka niwe mwanaume bora, kwa hiyo alitaka nipate maisha yenye utulivu, yale
tuliyokuwa tunaishi naye kwa kutangatanga hayakuwa na nafuu. Na kweli Big Frank
alinisaidia sana, kwani ni yeye aliyenikutanisha na timu yangu ya kwanza ya
kikapu. Kipindi hicho, nilimuona mama yangu wikiendi tu.
“Mama
alipopata uwezo wa kupanga nyumba ya vyumba viwili kwa msaada wa serikali, nilirudi
kuishi naye tena. Tuliishi pamoja mpaka nilipomaliza elimu yangu juu ya
sekondari, mengine yaliyosalia yanabaki tu kuwa historia.”
LEBRON
ANAUJUA USHUJAA WA MAMA YAKE
LeBron
anasema: “Mama yangu ndiye shujaa wangu. Tulihama nyumba nyingi kila mara kwa
sababu hatukuwa na uwezo. Tulizunguka huku na huko bila mafanikio na matumaini
hayakuonekana.
“Mama yangu
alijitupa huku na huko kufanya kazi, na hakuchagua kazi ya kufanya ilimradi
tupate cha kutukutanisha kwenye meza ya chakula. Pamoja na dhiki zote, nilikuwa
na uhakika wa jambo moja, ni upendo. Mama yangu alikuwepo karibu yangu
kunifunika blanketi na kunipa ulinzi niliohitaji. Hakuna aliyekuwa na umuhimu
kwake zaidi yangu.”
Anaongeza:
“Watu siku zote wanasema nimekuwa mwaminifu sana kwa mama yangu, hiyo ni kweli
kabisa kwa sababu naye amekuwa mwaminifu kwangu. Mama alinifundisha ladha ya
upendo wa kweli, nami nampa. Kwa mfano wake, nimekuwa nikiwasaidia watoto
wanaolelewa na mama zao bila baba. Ni kwa sababu nina uwezo na ni kwa sababu
mama yangu amenifanya niwe hivi nilivyo.”
MCHEZO
ULIGEUKA KITAMBO
LeBron
anasema kuwa tangu alipoanza masomo ya sekondari ya juu (high level), kodi ya
nyumba ilibaki historia kwa sababu kipaji chake kilimuwezesha kuingiza fedha
ambazo zilisaidia kulipia bili zote za nyumbani.
Mwaka 2003,
alifuzu chaguo la kwanza katika chujio la vyuo kuingia Ligi ya NBA. Alijiunga
na Timu Cleveland Cavaliers, aliyoitumikia mpaka mwaka 2010 kabla ya kujiunga
na Miami Heat alikocheza kati ya mwaka 2010 na 2014 kisha kurejea tena Cavaliers.
LeBron ni
staa mkubwa sana duniani kwa sasa, uwezo wake anapokuwa uwanjani umempa heshima
ya kipekee. Na wengine humwita King James, yaani Mfalme James, kwamba viwango
vyake ni vya kifalme. Zaidi ni mshindi mara nne wa tuzo ya NBA Mchezaji mwenye
Thamani kuliko wote (MVP).
Kwa miaka
miwili mfululizo amekuwa akiingiza kwa mwaka dola milioni 72 (shilingi bilioni 152),
mshahara ukiwa dola milioni 19 (shilingi bilioni 40) na mikataba ya matangazo
ikiinenepesha akaunti yake kwa dola milioni 53 (shilingi bilioni 112).
Utajiri wa
jumla ambao LeBron anatajwa kuumiliki ni dola za Marekani milioni 425 (shilingi
bilioni 896.15). Huwezi kuyazungumzia mafanikio bila mama nyuma yake. Gloria
ameweza kumfikisha mwanaye hapo alipo.
Leo hii,
Gloria anajulikana ulimwenguni kote hususan kwa wapenda kikapu na wengine
wanamwita Mama Kikapu, kwa maana tumbo lake limemleta duniani staa mkubwa wa
kikapu.
Gloria hajui tena shida, anakula matunda ya
mwanaye. Anaendesha gari ghali kabisa aina ya Porsche Panamera toleo la mwaka
2014 lenye thamani ya dola 200,000 (shilingi milioni 422). Anaishi kwenye jumba
la mtoto wake, lililopo Akron, Ohio, lililo na kila aina ya burudani, likiwa na
ukubwa wa futi za mraba 30,000 na thamani ya dola milioni 9.2 (karibu shilingi
bilioni 20).
Wakati
anatangatanga na mwanaye, wanaume walimkwepa kwa kuogopa kubeba mzigo wa
malezi, zaidi walimuona hana mvuto kwa sababu ya uchakavu wa sura na mwili,
vilivyotokana na ukosefu wa matunzo.
Gloria ana
umri wa miaka 47 lakini kutokana na maisha kumuendea sawa, vijana wanajigonga
kwake, kwani ananawiri, na mpenzi wake wa sasa ni mwa Hip Hip Da Real Lambo, 33.
Na wengi tu wanammezea mate.
Utamu huo wa
maisha anaupata baada ya kuamini kuwa mtoto siyo mzigo bali zawadi. Ni vizuri
kuchukua somo kwamba mimba haitolewi wala mtoto hatelekezwi. Ipende mimba kwani
ndiyo inaleta neema yako. Mlee mwanao kwa upendo, si ajabu ndiye nuru yako.
ONDOKA NA HILI
Hii ikupe
muongozo wa kutambua kuwa mtoto ni zawadi. Omba Mungu akuongoze na usibague,
maana hujui kuwa pengine huyo unayembagua ndiye mama au baba wa daktari bingwa
atakayegundua dawa za Ukimwi, Homa ya Ini (Hepatitis B na C), Kisukari na
kadhalika. Mheshimu kila mtu!
Mtoto wako
mtunze, mpe malezi bora kadiri Mungu anavyokujalia. Huwezi kujua kuwa pengine
huyo ndiye mkombozi wako.
Wewe mtoto,
ukizaliwa kwenye familia ya kimaskini, ikuongoze kuchangamsha ubongo. Wewe
ndiye shujaa wa familia yako, jitume ubadili hali ya maisha ya wazazi wako na
ndugu zako.
Kuzaliwa
kwenye familia maskini ni ishara kuwa wewe ni mfalme. Ukipambana na kufanikiwa,
unaitwa mfalme. Watoto wa Bakhressa wana fedha lakini siyo wafalme. Wamekuta
mteremko wa maisha!
Unabisha?
Daud alikuwa na uwezo gani wa kuwa Mfalme wa Israel mbele ya Saul? Daud alikuwa
mtu duni kabisa lakini ndiye alimpiga Goliath. Usicheze na Mungu na uteuzi
wake!
Zingatio kwa
mama; Usitoe mimba, usinyonge kichanga wala usitelekeze mtoto. Huyo anaweza
kuwa ndiye ameletwa na Mwenyezi Mungu kuwa mafanikio yako ila wewe unayakataa.
Baba;
Usikatae mimba, usiwe chanzo cha mimba kutolewa, usikimbie damu yako, hakikisha
unakuwa mlezi bora wa mwanao kwa hali na mali. Huwezi kujua ni zawadi gani
ambayo mtoto huyo ametumwa na Mungu akuletee.
Wazazi;
Hakikisha mnatoa malezi bora kwa watoto. Kile ambacho mnakifanya, kiwe ndiyo
uwezo wa juu kulingana na nafasi. Wapeni watoto mapenzi makubwa na muwafanye
wawe na furaha. Hao ni hazina yenu ya baadaye.
Mtoto; Wewe
siyo chochote bila wazazi wako. Wangeamua, ungetolewa ukiwa mimba changa.
Unapopata mafanikio, elewa kuwa wazazi wako wana thumni yao kwenye kila jasho
lako. Wafanye wazazi wako wafurahie kipato chako, usiwaache wakipata shida na
wewe upo ilhali uwezo wa kuwasaidia unao.
Mafanikio
yako yatapaa zaidi, vilevile utakuwa ni mwenye kubarikiwa mno kama wazazi wako
utawalinda kadiri kipato chako kinavyoruhusu.
0 comments :
Post a Comment