ads 728x90 B

Baba ampa mimba hausigeli, mama ajazwa na muuza duka



http://i0.wp.com/millardayo.com/wp-content/uploads/2014/10/Dad.jpg?resize=494%2C329
Baba na Mama Rosemina, walikuwa na mawazo sana. Wakiwa njiani walitamani kufika nyumbani haraka ili wamvae hausiboi wao anayeitwa Chaka. Alifanya kitu ambacho wao walikitafsiri kuwa ameingiza kirusi kwenye nyumba yao.
Walikuwa wanatokea hospitali ambako walimpeleka binti yao Rosemina kupimwa, huko aligundulika ana ujauzito wa miezi minne. Walipomhoji kwa kituo, akafichua ukweli kwamba mhusika wa mimba ni Chaka.
“Naombeni sana msimdhuru Chaka, nampenda sana,” Rosemina alijaribu kumtetea Chaka.
“Kelele wewe, tena funga kabisa bakuli lako. Tunakusomesha kwa pesa nyingi, leo unapewa mimba na hausiboi, aibu gani hii?” Baba Rosemina aliwaka kwa hasira. Chupuchupu amchape kibao Rosemina.
Mama Rosemina alikuwa amefura kwa hasira, machozi yakimtoka. Aliona mwanaye ameharibiwa maisha. Naye alitamani afike nyumbani haraka kisha amkamate Chaka, amlambe japo vibao vitano vya kikekike.
Jinsi Baba Rosemina alivyopaki gari, ilikuwa ishara tosha kuwa siku haikuwa ya kawaida. Alishuka na kumshusha Rosemina himahima, akamvuta kuingia ndani. Mama Rosemina naye akawafuata kwa nyuma akiwa na sura ya kisharishari.
Ungebahatika kuwaona, basi moja kwa moja ungeamini siku hiyo pangechimbika, mtu angekong’otwa na kuzikwa akiwa hai. Baba Rosemina alipofika ndani kwenye korido, hakutaka kupoteza muda, alipaza sauti kuita jina la Chaka.
“Naam,” Chaka aliitika.
“Leo utanieleza kwa nini umempa mimba Rosemina,” Baba Rosemina alizungumza kwa hasira. Upande wa pili Chaka alibaki kimya, hakujibu chochote.
“Wewe Chaka,” Baba Rosemina aliita kwa mara nyingine.
“Naam baba,” Chaka aliitika kwa unyenyekevu.
“Usiniite baba, mimi siyo baba yako. Nataka unieleze ni kwa nini umempa mimba Rosemina?” Baba Rosemina alimuuliza Chaka ambaye alikaa kimya.
“Unaniletea dharau siyo, sasa leo utaniambia,” Baba Rosemina alimwambia Chaka, wakati huo Chaka alikuwa ameshajitokeza.
Akajibu: “Sina dharau baba, tatizo kule chumbani nilipokuwa nilikuwa nasikia jina tu, maneno mengine sikuwa nasikia.”
“Acha utoto wewe, haya niambie hapahapa, ni kwa nini umempa mimba Rosemina,” Baba Rosemina alihoji.
“Sawa baba, mimi nitakujibu, ila naomba kwanza uende kule chumbani, ujionee mwenyewe, utakuwa unasikia jina tu, hilo hakuhakikishia,” Chaka alimwomba Baba Rosemina ambaye alikataa: “Usilete utoto wako, hebu nijibu haraka.”
“Nimekwambia nitakujibu, nenda kwanza kule chumbani wewe utaona. Utakuwa unasikia jina tu, Mimi sina dharau baba,” Chaka aliendelea kumsisitiza Baba Rosemina.
Baba Rosemina akaona isiwe tabu. Alikwenda kule chumbani ili kumaliza ubishi, akijua kwamba atakaporudi, Chaka hatakuwa na kisingizio kingine zaidi ya kujibu swali alilomuuliza kuhusiana na kumpa mimba Rosemina.
“Baba,” Chaka aliita. Wakati huo Baba Rosemina alikuwa ameshaingia kule chumbani ambako mwanzoni alikuwepo Chaka.
“Nakusikia,” Baba Rosemina alijibu.
“Kwa nini umewapa mimba mahausigeli wawili hapa nyumbani, alianza Monica, akaja Zuleha, wote sasa hivi ni nyumba ndogo zako, ukiwapa mimba unawahamisha, kwa nini unafanya hivyo baba?” Chaka aliuliza.
Baba Rosemina akawa kimya, Chaka akaita: “Baba.”
“Nimesema nakusikia,” Baba Rosemina alijibu.
“Kwa nini uliwapa mimba Monica na Zuleha halafu ukawalazimisha waache kazi hapa nyumbani kisha ukaenda kuwapangishia nyumba huko nje?” Chaka aliuliza tena.
Kwa swali hilo, Baba Rosemina aliendelea kuwa kimya. Baada ya muda, alitokeza pale kwenye korido, akasema: “Dah, kweli nimeamini, ukiwa kule chumbani unasikia jina tu.”
Mama Rosemina akawa mkali: “Hakuna lolote, leo nyie wote mtanieleza, hakuna chochote kwamba ukiwa kule chumbani hamsikii maneno mengine, mnasikia sana ila mnataka kuleta masihara.”
 “Mama usiwe mbishi, hebu na wewe nenda kule utaona, utakuwa unasikia jina tu,” Chaka alimwomba Mama Rosemina ambaye awali alikataa lakini baadaye alikubali. Akaenda kule chumbani ili naye ajionee.
“Nakwenda, ila nikirudi mtanikoma nyie wote. Iwe mlikuwa mnasikia jina tu au uongo, mtanitambua nikirudi,” Mama Rosemina alisema akiwa anaelekea kule chumbani.
“Mama eeh,” Chaka aliita.
“Haya ongea, nakusikia,” Mama Rosemina alijibu.
 “Kwa nini kila baba akisafiri hapa nyumbani anakuja kulala yule mangi muuza duka la mtaa wa pili? Huyu mdogo wetu wa mwisho, Jorum, umezaa na yuleyule mangi na wanafanana kweli lakini unamdanganya baba ni mwanaye, kwa nini unafaya hivyo?” Chaka aliuliza.
Mama Rosemina hakujibu kitu, alikaa kimya tena kwa utulivu wa hali ya juu kama maji mtungini. Chaka akaita: “Mama unanisikia?”
“Nakusikia Chaka,” Mama Rosemina alijibu.
“Naomba ujibu ni kwa nini unatembea na yule mangi muuza duka, unamkosea heshima baba kiasi kwamba kila akisafiri, unamwita anakuja kulala hapa nyumbani tena chumbani kwake, mnalala kitandani kwake. Haitoshi, umezaa naye lakini unamdanganya baba kwamba Jorum ni mwanaye wakati unaujua ukweli kuwa yule ni mtoto wa mangi,” Chaka alizidi kusasambua.
“Jamani, ni kweli kabisa, ukiwa kule chumbani huwezi kusikia neno ligine lolote zaidi ya jina tu,” Mama Rosemina alisema akiwa amerejea kwenye korido. Alikuwa akitazama chini kwa aibu.
“Wote hamna lolote, kila kitu kinasikika, uchafu wenu wote leo upo hadharani, sasa nimuone mtu wa kunisema na hii mimba yangu. Wewe mama ni mchafu, baba umeshindikana, sasa mniache na Chaka wangu tupendane,” Rosemina aliongea.
Baba na Mama Rosemina aibu iliwashuka, hakuna aliyethubutu kumjibu Rosemina, maana kama ni fedheha ilikuwa ya mwaka. Waliumbuka kuliko mfano wa kawaida.

Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment