Na Luqman
Maloto
Umewahi
kusalitiwa? Ulipogundua ilikuuma bila shaka. Maumivu ni makali mno pale
unaposalitiwa na mtu unayempenda na zaidi unayemwamini. Hangaiko la moyo wako
halitafanana kwa kila usaliti utakaofanyiwa.
Umewahi
kusaliti? Ulipogundulika ilikuingiza kwenye fedheha ya kiwango cha juu. Unapoitwa
msaliti maana yake unakuwa umewekwa kwenye kundi la hovyo. Mtu mwenye tamaa na
usiyefaa kuaminika hata kidogo.
Hakuna
aliyeanza kusaliti akawa hajui madhara ya anachokifanya. Zaidi, usaliti siyo
tendo la bahati mbaya, ni kuchagua. Yaani unajifikiria kisha unaamua kufanya
tendo lenye matokeo ya kumuumiza mwenzio, kujiaibisha na kusababisha usiaminike
tena, zaidi kujidhalilisha.
Baada ya
muda mwenzio anakuja kugundua kuwa wewe siyo mwenye kutosheka, una hila,
unatamani vingi kwa wakati mmoja. Unamuumiza kwa sababu umemfanya ajione siyo
mwenye kukutosha. Unampa mataabiko ya moyo ambayo tiba yake siyo rahisi.
Katika
maisha yangu ya kila siku na tafiti ambazo nimekuwa nikizifanya, jibu la moja
kwa moja ni kuwa hata vijana ambao hawajaanza kubeba majukumu wapo kwenye
kiwango kizuri cha kuhisi maumivu ya usaliti pale yatakapowatokea.
“Mke anauma
sana, yaani mke wangu atoke nje ya ndoa kweli!” kijana mmoja aliwahi kujibu
baada ya kumuuliza kama anajua maumivu ya usaliti pale atakapokuwa ameoa au
atakapokuwa na mwenzi wake, ama mpenzi au mchumba.
“Mwanamke
atakayetembea na mume wangu sijui nitamfanya nini, ila sitamuacha salama!” Maneno
haya alinitamkia binti mwenye umri mdogo kabisa. Anajua matokeo ya baadaye.
Maumivu ya usaliti yapo kiasili zaidi. Binadamu hayajui baada ya kufundishwa.
Yanakuja yenyewe!
USALITI NI UZEZETA
WA AKILI
Inabidi
kutumia neno upumbavu lakini pia halitoshi, usaliti ni uzezeta wa akili!
Usaliti siyo ujinga kwa sababu mjinga ni yule ambaye anakuwa hajui kitu,
akielimishwa anaelimika kisha anafuata njia inayofaa.
Msaliti ni
zezeta wa akili kwa sababu anafanya kitu ambacho anakijua lakini anafanya tu! Matokeo
yakishajiri anabaki kujilaumu kwa aibu. Ni upumbavu kusubiri kujilaumu wakati
ulikuwa na nafasi ya kuepukana na janga.
Usaliti
hutokea kwa sababu ya kutawaliwa na fikra mfu. Kukosa mawazo sahihi.
Kudanganywa na leo kisha kusahau kwamba ipo kesho. Kushindwa kumkataa Shetani
wa usaliti na kumtii hatua kwa hatua mpaka kitendo.
Msaliti huwa
hafikirii athari baada ya usaliti wake kugundulika, hujikita kwenye tamaa za
machoni tu. Kama mtu anaweza kuwa na macho yenye kukosa udhibiti wa akili, basi
huyo ni kipofu kuliko mlemavu wa macho.
Mume wa mtu
damu inamchemka, hisia zipo wima, anawaza kutenda dhambi na mwanamke mwingine.
Tena anaweza kuwa mke wa mtu. Anachoshindwa kufikiri vizuri ni kuwa mkewe au
mume mwenye mali akibaini mgogoro utakuwa mkubwa.
Mke wa mtu
amepumbazwa na macho, akili inashindwa kufanya kazi tena. Anafikiria tu kutoka
nje ya ndoa. Haifikirii mara mbili kuhusu aibu atakayoipata baada ya matokeo ya
usaliti kugundulika. Hawazi kuhusu maumivu anayoweza kumsababishia mume wake.
Kichekesho
cha akili; Mtu una mwenzi wako, upo huru naye kabisa. Mnaweza kujadiliana kila
siku nini cha kufanya, mpeane nini kwa uhuru na utashi wenu. Hakuna wa
kumhofia. Ni ninyi wenyewe kwa raha zenu.
Nani
anapenda kuitwa mwizi? Kumiliki mali yako na kuitumia bila kuhofia macho ya
wengine ni jambo lenye afya na heshima kubwa. Popote kule unakuwa huru kwenda na
mali yako. Ukikutana na watu, kwa kiburi cha umiliki, unasema “huyu ndiye.”
Naye atatamka “mwenyewe ndiye huyu.”
Fumba macho
kwa sekunde kadhaa kisha uwaze raha za kuwa mmiliki. Ile hali ya kujiamini
ambayo unakuwa nayo popote pale. Unaweza kumshika mkono barabarani, kuketi na
kukutana naye kokote. Hakuna asiyependa uhuru huu!
Kituko
kinakuja, mtu huyohuyo mwenye uhuru wake anajiingiza kwenye uhusiano wa siri,
yaani mapenzi ya wizi. Mapenzi yenye presha za kujitakia. Kukutana mpaka
mazingira ya kutafuta. Unapokwenda sehemu unahofia watu wanaokujua wasiwepo.
Unatembea ukiwa umejaa wasiwasi.
Kabla ya
kwenda lazima umsikilizie mwenzi wako, ratiba zake zipoje? Unaamua kudanganya
safari ili kufanikisha malengo yako. Unakosa uhuru kwenye simu yako. Hutaki
mwenzio ajue maneno au namba za siri za akaunti zako za kijamii. Simu yako huna
uhuru nayo. Unaweza kwenda nayo mpaka chooni.
Ikiita mbele
ya mwenzio unagopa kupokea. Ikiita ukiwa mbali kidogo unaweza kukaribia kuvunja
mguu ili uwahi mwenzio asipokee au kusoma sms. Ukijitutumua na kupokea huongei
kwa uhuru, unajibu kwa kutojiamini na unataka mazungumzo yaishe haraka na
unajitahidi kumzuga mwenzio pembeni yako asielewe.
Akikuuliza
nani huyo unajibu: “Nanii… naniii… rafiki yangu, nanii dada.” Unatengeneza jina
litakalomridhisha. Kosa lako ni kujidanganya kuwa mwenzio hana akili.
Atakushtukia.
Jaribu
kuwaza; Wakati kwa mwezi wako una uhuru wa kwenda naye popote. Kutoka naye out
bila kubughudhiwa na mtu. Unajiingiza kwenye uhusiano wenye mapenzi ya pande
mbili tu.
Upande wa
kwanza ni mawasiliano ya mtandao, iwe kuchati kwenye simu, sms za kawaida,
facebook, wahatsapp, viber, skype, instachat, BBM na kadhalika. Upande wa pili
chumbani. Mapenzi sawa na biashara ya ngono mitandaoni.
Wanaofanya
biashara za ngono mitandaoni ndiyo hukutana kwa staili hiyo. Unaangalia
mtandaoni, unaridhishwa na mwanamke au mwanaume anayejiuza, unafuata maelekezo,
unalipa kisha unatoa anuani ya mahali ulipo, uliyemnunua akifika hakuna kingine
zaidi ya kukamilisha biashara.
Mke au mume
wa mtu naye anajiingiza kwenye mapenzi ya mtindo huu. Mepenzi mengi kwenye
simu, facebook, whatsapp na kadhalika. Siku ya kukutana ni chumbani tu! Mtu
mwenye kufikiri vizuri atajisikia vibaya na kuacha mapenzi haya yenye kukosa
uhuru na heshima.
AINA ZA
USALITI
Usaliti kwa
maana pana ni ukosefu wa uaminifu, ustaarabu na uungwana. Ni kumtenda mwenzio
kinyume na inavyostahili. Juu zaidi ni tendo la kikatili. Unaweza kusema huwezi
kuua mtu lakini watu walishamwaga damu kwa usaliti.
Unaweza
kusalitiwa na mzazi wako au wewe mtoto kumsaliti mzazi wako. Wafanyabiashara
kudhulumiana. Mfanyakazi mwenzio anaweza kukusaliti. Marafiki kugeukana. Kwa
kifupi ni kuwa usaliti una pande nyingi. Siyo katika uhusiano tu wa kimapenzi.
Angalizo
kwako ni kuishi kwa kuwatendea wema wenzako. Kile ambacho ni maumivu na mateso
ukitendewa basi usimfanyie mwenzako, kwani naye ana moyo, nyama na damu kama
ulivyo wewe.
Zaidi,
unaposaliti, jihesabu tu kuwa umekosa ustaarabu, uungwana na siyo mwaminifu. Kama
sifa hizo siyo zako kwa nini utende yale ambayo yatakufanya ubebeshwe wasifu
mbaya? Juu ya yote usaliti ni kutokujiheshimu! Je, wewe hujiheshimu? Kama
hujiheshimu, maana yake hufai kuheshimiwa.
ATHARI ZA
USALITI
Ni rahisi
sana kuvunja uaminifu lakini kuaminiwa kwa mara nyingine ni vigumu mno. Wapo
mke na mume walizeeka pamoja lakini manung’uniko hayakuisha. Kumbukumbu za
usaliti waliofanyiana nyakati za ujana wao ziliwatesa mpaka walipotengana kila
mmoja akiingia kwenye kaburi lake.
Athari namba
moja unapokwenda kusaliti, kaa ukijua kuwa unatengeneza kitu ambacho mwenzio
akikibaini, atapoteza kabisa imani juu yako. Hata akikusamehe, utamfanya
asiamini tena kama unaweza kujitunza ukiwa mbali na macho yake.
Elewa kuwa
usaliti wako unakwenda kupiga mstari wenye kufuta neno ‘mwamunifu’ kwenye
mzunguko wa maisha yako yote na kuandikwa ‘msaliti’. Siku zinaweza kupita
ukadhani yaliyotokea yamepita na watu wamesahau. Hutasahaulika.
Maisara
alifunga ndoa na Baraka. Maisha yao ya kimapenzi yalikuwa mazuri mno. Ungewaona
nyakati za mwanzo wa uhusiano wao, usingepata tabu kujua kweli kwamba
wanapendana na kwa hakika walichaguana.
Walijenga
familia bora, wakawa na watoto watatu, walijenga nyumba Kigamboni, Dar es
Salaam. Baraka alikuwa mhangaikaji sana. Alijituma mno kufanya kazi zake za
kila siku ili kuongeza pato la familia. Maisara kazi zake zilikuwa za kawaida,
kutoka asubuhi kurejea nyumbani majira ya alasiri.
Baraka
hakuwahi kumtilia shaka mkewe, alimwamini sana. Si kwamba hakuwahi kusikia
chochote kuhusu mkewe, la hasha! Imani yake kwa mkewe ilikuwa ya kiwango cha
juu mno. Yote aliyapuuza.
Kumbe
Maisara alikuwa anasaliti ndoa kadiri alivyojisikia. Baraka akiamini mkewe ni
mwaminifu, majirani na hata ndugu walidhani hajielewi ndiyo maana anamwacha
mkewe anasaliti. Maisara akadhani Baraka ni mjinga. Aliichezea imani kubwa
aliyopewa na mumewe.
Huwezi
kudanganya siku zote! Nyakati zilifika, Baraka akabaini kuwa mkewe siyo
mwaminifu, ugomvi ulitokea mkubwa sana. Mpaka watoto wao watatu wakabaini
mgogoro uliokuwepo kwa wazazi wao.
Ghafla
Baraka akawa hawezi kufanya kazi zake inavyotakiwa. Alibaki anagombana nyumbani
na mkewe ambaye naye alishindwa kwenda kazini kwake. Mara kupigana, mara vikao,
ikawa mateso juu ya mateso.
Maisara
alipoteza uzito na alikonda sana. Baraka kiasili ni mweupe, alikonda na kuwa
mweusi tii! Watoto shuleni wakawa hawasomi, mawazo yote yakawa kwenye migogoro
ya wazazi wao.
Ni nyakati
ambazo watoto walishuhudia baba yao waliyemuona mpole siku zote na aliye na
upendo kwao na kwa mama yao, akitamka maneno makali mno kwa mama yao. Maneno
yenye kudhalilisha. Maneno ambayo hakuna mtoto ambaye angependa kusikiliza mama
yake akiambiwa.
Shuleni
watoto walifeli mpaka walimu walishangaa. Waliwaita wazazi wajadiliane lakini
hakuna hata mmoja aliyekuwa tayari kwenda kusikiliza mashauri ya watoto
shuleni. Kila mmoja alivurugwa. Maisara hakutaka tena mapenzi ya nje na ndani
yaligeuka kaa la moto.
Baraka
alijitahidi kumsamehe Maisara alishindwa. Miezi ilikatika misuguano iliendelea,
mwisho aliamua kumtimua Maisara. Ndani ya muda mfupi katika ndoa yao walipiga
hatua kubwa kimaendeleo. Walijenga nyumba, wakawa na mashamba, Maisara akawa na
biashara zake, waliweza kuwa na magari matatu. Sasa hivi wanarudi nyuma.
Kumbuka
kuhusu vifo vya watu, wengine kusababishiana ulemavu. Kwa pamoja hayo yote ni
matokeo ya usaliti. Uadui mkubwa kati yako na mwenye mali uliyoiba (mume au
mke).
Namkumbuka
Mama Jayden, alipobaini mume wake ni msaliti na ameweza kutembea mpaka na
rafiki yake, aliona hawezi tena kuishi. Alimpenda sana mume wake Baba Jayden.
Maskini Mama Jayden, akamnywesha kwanza mwanaye Jayden sumu, alipokufa. Akanywa
na yeye! Hakutaka kumwacha mwanaye kwenye ulimwengu huu uliojaa matatizo.
Haukuwa
uamuzi wa busara ambao Mama Jayden aliuchukua lakini huwezi kuingia ndani yake
na kujua ni kiasi gani aliumia. Ukiona mtu anaumia sana baada ya kusalitiwa,
maana yake alimwamini sana aliyemsaliti. Kusalitiwa na usiyemwamini haiumi
sana. Si unajua haaminiki? Hana mwanama!
Maureen ni
kati ya wateja wangu wa siku nyingi. Nimewahi kufanya naye mashauriano katika
masuala kadhaa yaliyomtatiza. Aliwahi kunisimulia kisa cha yeye mimba yake
kutoka baada ya kuona sms ya kimapenzi kwenye simu ya mchumba wake.
“Afadhali
ningekuta inbox, ningewaza watu wanatuma tu! Sms niliikuta outbox kuonesha
mchumba wangu ndiye ametuma. Sikumgombeza mchumba wangu wala mwanamke aliyetumiwa
sms lakini mshtuko nilioupata ulisababisha mimba yangu itoke,” alisema Maureen.
Mfano
mwingine ni James ‘Jimmy’ ambaye sasa hivi yupo jela, alikohukumiwa kifungo cha
miaka 15 baada ya kukutwa na hatia ya kumchoma kisu Modest. Alimchoma kisu
tumboni na kwenye jicho. Modest yupo hai lakini ana chongo hivi sasa. Jimmy
alichukua uamuzi huo baada ya kugundua Modest anatembea na mkewe.
Helen sasa
hivi sasa ni mlemavu wa ngozi. Watu wakimuona hudhani ni albino au Mzungu.
Mwenyewe alikuwa na rangi ya chocolate. Weusi wa kung’ara (black beauty).
Alipoteza ngozi yake ya asili baada ya kumwagiwa maji ya moto yaliyochanganywa
na mafuta ya moto.
Sababu ni
wivu wa mapenzi. Helen ni mfanyakazi mwenzake Sufian ambaye ni mume wa Rehema.
Walikuwa wafanyakazi wanaoelewana sana. Rehema kukuta sms ya Helen kwenye simu
ya Sufian halikuwa jambo la kushangaza.
Sufian
alimtambusha Helen kwa Rehema kama mfanyakazi mwenzake. Sufian alimwita Helen
dada, naye akamwita Rehema wifi. Siku ya siku Rehema akagundua Helen anatoka
kimapenzi na Sufian. Aliumia sana, “kumbe wananifanya mjinga!” aliwaza.
Rehema
alijiridhisha kila kitu baada ya kufuatilia nyendo zao. Akajipa uvumilivu,
akajifanya hajabaini chochote. Akaendelea kumchangamkia Helen. Siku moja
alimwalika nyumbani kwake, Helen akaenda. Hakujua ndiyo anaifuata adhabu yake.
Helen akiwa
amekaa sofani, alimwagiwa maji ya moto yaliyochanganywa na mafuta ya moto kisha
Rehema akakimbia. Mpaka leo Rehema hajulikani alipo. Helen kawa mlemavu, Sufian
hajui mkewe (Rehema) alipo. Ndugu wa Helen walimlazimisha Sufian amuoe kwa
sababu kawa mlemavu kwa sababu yake.
Mifano hiyo
ikupe picha kuwa katika usaliti lolote linaweza kutokea. Inategemea na hasira
za mtendwa. Matukio ya mifano ni mingi. Usimsahau aliyepigwa risasi tumboni na
mama yake akauawa na mchumba wake ambaye naye alijiua.
Zakia ni
mteja wangu wa ushauri, aliniambia: “Mume wangu alikuwa mtu mwema sana, alikuwa
ananiita majina mazuri kila siku. Alipenda kuzungumza yale ninayopenda, na
alinipamba mbele ya ndugu zangu, zake, marafiki zangu na wake.
“Siku
alipogundua nimemsaliti alibadilika kabisa. Nilizowea kumsikia akiniita mke
wangu, sweetheart, darling, honey na mengine ya kupendeza, ghafla akawa ananiita
malaya, changudoa, kicheche na mengine mabaya. Hili huwa linaniumiza sana.
Natamani nikutane na kila mwanamke nimwambie athari ya usaliti. Ni mbaya sana.”
KIWANGO CHA
USALITI
Kuna usaliti
katika mapenzi ni rahisi kusameheka na yakaisha, mwingine athari yake hudumu na
kudumu. Upo ambao unaweza kubabisha kesi ndogo, mwingine ni vita kubwa na uadui
usioisha.
Fikiria
mwanaume unatoka kimapenzi na dada, mdogo au ndugu wa mkeo. Vivyo hivyo, mke
kutembea na kaka, dada au ndugu yeyote wa mume. Hapo unakwenda kutengeneza doa
lisilokwisha. Una akili timamu, unajua athari hii.
Mwanamke
unatembea na mfanyakazi mwenzie mume wako au bosi wa mumeo. Mume kutembea na
mfanyakazi mwenzie mkeo au bosi wa mkeo . Mke kutoka na rafiki wa mume,
kadhalika mume kutoka na rafiki wa mkewe.
Athari
zinatofautiana, yote ni maumivu na kukosa uaminifu. Mke kutembea na houseboy na
mume kutoka na housegirl. Kila eneo lina athari yake. Muhimu ni kuepuka usaliti
na kutunza uaminifu. Muhimu zaidi ni kukwepa kufarakanisha ndugu. Usiwafanye
ndugu wa damu wawe maadui kwa sababu ya tamaa zako.
Hafidh na
Amiru ni ndugu tumbo moja, ila viapo vyao ni kuwa hawatazikana. Hafidh ni kaka
wa Amiru na ndiye alimsomesha. Uadui ulikuja baada ya Amiru kutembea na mke wa
Hafidh. Stella hataki tena kumsikia mdogo wake Roseheart, kisa ni Stella
kubaini Roseheart anamzunguka kwa mumewe.
UMESALITIWA?
HUJADHALILISHWA
Ni kweli
inauma kwa kiwango cha juu mno. Lakini katika mambo ambayo hutakiwi kuumiza
kichwa juu yake ni hisia kuwa mumeo au mkeo anapokusaliti anakuwa
amekudhalilisha. Hapana! Anakuwa amejidhalilisha yeye mwenyewe.
Hupotezi
heshima kwa kusalitiwa, ila anapoteza thamani na utu wake anapobainika siyo
mwaminifu. Mzee Nelson Mandela, alifariki dunia kisha akazikwa kwa heshima
kubwa. Hakuwahi kupoteza thamani yake kwa usaliti aliotendewa na aliyekuwa
mkewe, Winnie Mandela.
Tambua pia
kuwa thamani na utu wa Winnie, vilipungua mara tu alipobainika kuwa amesaliti
ndoa. Mtu anayejiheshimu ni yule ambaye analinda heshima ya ndoa yake.
Usipoilinda utaonekana mtu wa hovyo mbele ya jamii!
Fununu tu
zilisababisha Mfalme Kaisari aache mke. Baraza la Wazee lilifanya uchunguzi na
kurejesha ripoti kwa Kaisari kuwa mkewe hajasaliti ndoa na kijana aliyesemwa,
ni uvumi tu, Kaisari akasema: “Mpaka asingiziwe maana yake anaishi vibaya.”
Kaisari akampa talaka mkewe. Aibu kwa mke kuwa na nyendo mbaya.
Unaposalitiwa
usisage meno kuwa mkeo au mumeo humridhishi ndiyo maana anakusaliti. Zingatia,
kuna tamaa na kuridhika. Wapo wengi baada ya kufumaniwa ndipo walijuta kwamba
walichokuwa wanakifukuzia nje hakikuwa bora kuliko kile wanachokipata ndani.
Mwasiti
alirudi kwa mchumba wake na kupiga magoti: “Nisamehe mpenzi wangu, wewe ni
mwanaume bora sana, sijui hata kilichokuwa kinanipeleka nje. Ni tamaa, ni
Shetani.” Kama Mwasiti, ndivyo na wanaume wengine hujuta, wake zao ni bora,
wazuri, warembo lakini wakishasaliti na kugundulika, husaga magoti kuomba
msamaha.
Wengi
wakishafumaniwa huomba msamaha, hata wakitia kiburi baadaye hurudi na machozi
mengi. Ni kipimo kuwa mwizi wako siyo bora kuliko wewe, ila tamaa tu! Kuna
aliyetoka na hougirl au houseboy! Yupo anayetembea ni muuza genge au bucha!
Unadhani hao ni bora zaidi? Ni tamaa za msaliti na kukosa kujiheshimu.
0 comments :
Post a Comment