ads 728x90 B

MUUZA UNGA SAWA NA MCHAWI ANAYEMILIKI MSUKULE



http://api.ning.com/files/MOGlnOwPxer8a6ttpu*0FuBvfrFGiRD6reT1RPWOWH5UkpQqte*4QatFaGAuOVn-KSo8h2jYa1x93ciAueFE5T9OGLOaoYa9/chid.jpg
Na Luqman Maloto
Wauza unga wanafanana na wachawi wanaomiliki misukule. Kitabia na matendo, hawana tofauti. Nitaeleza mbele ya safari na utanielewa, ila kwa sasa hebu ngoja kwanza niseme hisia zangu.
Kwa mtu yeyote mwenye ubinadamu aliyepata kumfahamu vizuri Rashid Abdallah Makwilo ‘Chidi Beenz’, leo hii hawezi kushangilia mabadiliko ya msanii huyo.
Chidi Beenz, mwite King Kong! Nyakati hizo alikuwa sahihi kujiita King Kong. Mwili mzuri, wa mazoezi, shupavu kwelikweli. Na kama umeshaona muvi za King Kong, hapo tupo sawa.
Sauti nzito, jukwaani kifua wazi, mic mbili mkononi, anachezea sauti yake anavyotaka. Jukwaani saa nne (dakika 240) alizimaliza. Leo hii alivyo, inauma sana!
Chidi Beenz ndiye aliyejiita Busta Rhymes wa Bongo. Alistahili pia kujiita hivyo. Msikie Chidi anavyochezea sauti yake, msikilize pia Busta, yule rapa wa Marekani, mapafu manene, aliyewahi kutamba kuwa na uwezo wa kukabiliana na kifaru!
Ilikuwa ukisema Chidi siye Busta, nani mwingine rapa wa Tanzania? Lazima kufika mahali ukiri vipawa vya watu.
Chidi, rapa mwenye pumzi hasa jukwaani. Siku moja aliwahi kuniambia: “Nikiwa jukwaani huwa siyo binadamu wa kawaida.”
Siku nyingine pia katika mazungumzo yetu, aliniambia: “Kuna madude huwa natumia, nikipanda nakuwa mnyama jukwaani.” Vilevile alipata kunitambia: “Mimi ni animal.” Kwamba yeye ni mnyama mkali!
Chidi, aliitenda vema kazi yake. Alikuwa kiungo muhimu mithili ya chumvi kwenye mboga. Kuna nyakati wanamuziki wengi waliona ili nyimbo zao ziwe na ladha sahihi, basi vema kumshirikisha Chidi. Na kila aliposhirikishwa hakuharibu!
Kumbuka Tundaman na Neilah yake, Mwasiti na Hao, Marlaw na Umenuna, Nonini wa Kenya (wimbo Nifanye Muziki) na nyingine nyingi. Hapo sijataja za wana-Hip Hop ambazo ni kibao.
Isisahaulike kuwa kati ya mwaka 2007 mpaka 2010, Chidi Beenz aligeuza tuzo ya Hip Hop katika Tuzo za Muziki Tanzania (Tuzo Kili), kama mali yake. Alizibeba mfululizo.
Mara ya mwisho Chidi kubeba tuzo ya Kili, ilikuwa mwaka 2010, Tuzo ya Msanii Bora wa Hip Hop, Ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam. Baada ya hapo ndiyo ikawa mwisho wa ufalme wa Chidi kwenye Hip Hop Tanzania.
Mwaka 2012, Chidi alipanda jukwaani kukabidhi moja ya tuzo kwa Diamond Platnumz, Mlimani City, Dar es Salaam. Siku hiyo, Diamond alishinda tuzo saba kwa mkupuo. Ona heshima ya Chidi, tafakari huku alipofika. Kama ulimfahamu Chidi na huumii, baki na ukosefu wako wa utu!
TULIE NA WAUZA UNGA!

Usimcheke Chidi Beenz kwa mabadiliko yake ya kimaisha, unachotakiwa kuelewa ni kuwa safari ya Chidi kutoka Chidi Beenz Chuma, Animal, mpaka sasa ambaye anahitaji huruma na upendo ili arejee kwenye ule Uchuma wake tunaoupenda, inamaanisha safari ya muuza unga, kutoka hali fulani ya kimaisha mpaka utajiri.
Ndiyo kusema, kuporomoka kwa Chidi kiafya, jinsi alivyokuwa anadhoofu ndivyo muuza unga alivyokuwa anatengeneza fedha za kumfanya awe tajiri. Utajiri wa muuza unga ndiyo kifo cha mtumia unga!
Ukivunjika mbavu kwa madhila ya Ray C, dada yangu mpenzi Rehema Chalamila, hapohapo upate picha kuwa safari ya kutoka Ray C yule Kiuno Bila Mfupa mpaka aliyeharibikiwa na madawa, ndiyo safari ya muuza unga kutoka muuzaji mdogomdogo (pusha) mpaka ulodi wa unga.
Hapo namaanisha yule muuzaji wa unga mkubwa anayegawa kwa wauzaji wadogowadogo, kwa hiyo anakuwa ameshatajirika. Amekuwa tajiri kwa kuua watu, kuharibu nguvu kazi ya taifa. Utajiri wa kuyafanya maisha ya vijana kuwa mateso! Utajiri wa kishenzi!
Kama utayakumbuka maisha ya Ray C alivyokuwa anatengeneza pesa kwa muziki na biashara ya maduka, mpaka kugeuka tegemezi, akiwa hana uwezo wa kuzalisha kipato chake mwenyewe, zaidi akawa mgonjwa, unawezaje kumcheka na kumpigia makofi muuza unga?
Ray C alimiliki nyumba na gari akauza! Fedha zilikwenda wapi? Ziliishia kwenye unga. Ndiyo kusema wakati Ray C anapoteza nyumba na gari kwa sababu ya unga, ndivyo muuza unga alivyoweza kumiliki gari na nyumba kwa sababu ya unga.
Ni sawa tu kusema kuwa gari, nyumba na mali zote za Ray C, zilihamia kwa muuza unga katika mlango wa nyuma. Huwezi kuuita unyama?
IPO STORI HII
Kuna msanii mmoja maarufu kabisa. Ni teja! Simtaji jina leo kwa sababu ya tukio la aibu ambalo lilimpata.
Alikwenda kwenye ziara ya muziki nchi jirani akapata fedha nyingi. Aliporudi Dar es Salaam, alikwenda kuripoti tu nyumbani kwao, akaacha begi la nguo kisha akatoweka.
Kumbe mwanamuziki huyo alijiunga na wenzake, wakakaa hotelini, wanavuta unga. Pesa zote zilikwisha na hoteli walifukuzwa.
Mwanamuziki huyo alikwenda kwa wauza unga kukopa madawa, akapewa. Si wanamfahamu ni mteja wao? Alipopewa alitumia palepale na kuzimika.
Ikawa mchezo, akiamka wanampa tena madawa. Msanii akakonda kabisa. Ulevi wa madawa makali bila kula.
Taarifa zikafika nyumbani kwao, wakamfuata. Wale wauzaji wakakataa kumruhusu mwanamuziki huyo kuondoka na ndugu yao kwa sababu wanamdai fedha za unga na huduma za kila siku. Wakata wapewe shilingi milioni tatu.
Familia kwa hofu kuwa wakienda polisi, watalifanya suala hilo kuwa zito na vyombo vya habari kunasa, hivyo kumwaibisha ndugu yao ambaye ni maarufu, ikabidi wajichange mpaka walipopata kiasi cha fedha kilichohitakiwa, wakaenda kumkomboa.
Unaona unyama wa wauza unga? Fedha zake walimmalizia, wakampa unga kwa deni na kumfungia asiondoke mpaka ndugu walipe fedha walizosema wanamdai. Muuza unga hawezi kuwa ndugu wala rafiki wa binadamu. Muuza unga siyo mtu! Muuza unga ni mnyama!
TUELEWANE
Unga ni janga. Usimcheke Chidi Beenz maana huijui kesho. Wapo wamegeuka mateja kwa kulazimishwa, wapo waliohadaiwa.
Yupo alitekwa akapewa mihadarati, damu yake ikaharibika. Naye akajikuta asipopata madude anakuwa na alosto kama teja mwingine.
Wapo waliodanganywa, wakapewa na kutumia bila kujua. Mwisho wakazoea, waliposhtuka wakawa wameshachelewa. Na ukishaanza, kutoka ni ngumu. Wewe usicheke, omba Mungu yasikukute.
Tunaendelea kuishi, unaweza kumcheka teja wa leo, kesho mwanao akaingia kwenye mkondo huohuo. Kama siyo mwanao, basi ndugu yako yeyote au rafiki unayempenda.
Ifike wakati tuache kuwasimanga na kuwanyanyapaa waathirika wa madawa ya kulevya, bali tuwaweke mbele ili tuwakabili wauza unga.
Twende mkono kwa mkono na mateja wetu mpaka kwa matajiri wa unga. Tuwaambie: “Utajiri mnaommiliki, ndiyo umesababisha ndugu zetu hawa wawe hivi.”
Lazima wauza unga watambue hasira tulizonazo dhidi yao. Vema kuwanyooshea vidole na kuwaambia wao wameharibu vipaji vizuri vya Chidi na Ray C. Tuwaambie kuwa tunajua, kama siyo wao, Chidi angebaki kuwa King Kong, Ray C angeendelea kuitwa Kiuno Bila Mfupa!
Wauza unga ni sawa na wachawi wenye kumiliki misukule. Maana nao wanamfanya mtu mzima anageuka ndondocha asiyejitambua.
Teja barabarani ana tofauti gani na yule aliyetendwa vibaya na mchawi akafanywa ndondocha? Athari wanazosababisha ni sawa kabisa.
Yule msichana mrembo aliyekutwa shimoni Kimara, ikadaiwa aliwekwa msukule na tajiri mmoja kwa sababu za kusaka utajiri, ana tofauti gani na kijana aliyekuwa nadhifu, mchapakazi, mwenye maono ya kufanikiwa kimaisha lakini sasa hajiwezi pale Manyanya, Kinondoni kwa sababu ya matumizi ya unga? Teja na ndondocha kuna tofauti gani?
Wote mambo yakishachachamaa wanakuwa hawajitambui. Hayupo kati yao mwenye uwezo wa kuzalisha. Sanasana mateja wengi hugeuka kero mitaani wakipora watu ili wapate fedha za kwenda kununua unga kisha waongeze utajiri wa wauza unga.
Sikiliza na uache ubishi; Kama kuna siku uliibiwa na teja, hebu punguza hasira zako kwa huyo teja, tazama utajiri wa muuza unga, halafu jiongeze kuwa vile vitu ulivyoibiwa, vilikwenda kuongeza mali za haramia huyo wa madawa ya kulevya.
Teja ni mtumwa wa uteja wake. Hana fedha na alishaharibikiwa. Sasa anafanyaje naye ni mwathirika wa mihadarati? Inabidi akuvizie akuibie kisha aende akamtajirisha muuza unga.
Ndiyo! Teja alipokuibia alikwenda kuuza, fedha ambazo alizipata kwa mauzo ya vitu vyako, alikwenda kuzitumia zote kwenye kununulia unga. Faida kuu kwa haramia muuza unga!
Muuza unga na mchawi anayebadili binadamu kuwa ndodocha hakuna mwenye nafuu! Wote ni wanyama, tena washenzi hasa mbele ya Mungu. Ifike mahali tuwaambie wauza unga wanaosema wanachukia uchawi, kuwa wao ni sawa na wachawi. Ni zao moja, ila utendaji ni tofauti!

Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment