ads 728x90 B

MASIMANGO YA LEO NI UNYENYEKEVU WA KESHO




WANAKUCHEKA kisa huna chochote? Hutakiwi kuchachamaa na kulazimisha usichekwe. Pokea vicheko vyao kwako, piga moyo konde!
Vicheko vya dharau dhidi yako dawa yake siyo kukasirika au kupambana na wachekaji. Elewa tu unachekwa lakini ni vicheko vya muda mfupi. Kamwe haviwezi kudumu!
Ukikaa peke yako usijikunyate, maneno ya dharau yasikufanye ujione mnyonge. Katu usivunjike moyo. Badala yake tabasamu kwa dharau zao pamoja na vicheko vyao.
Wala usiende mbele yao kwa tambo na majigambo kisha upayuke: “Ipo siku yenu mtaniheshimu.” Acha mwisho uje udhihirishe mantiki (let the end to justify the means).
Upo kwenye jamii ambayo unabanwa, mchango wako wa mawazo hausikilizwi. Hata hupewi nafasi ya kuzungumza. Unabaguliwa na kuonekana mtu duni wa daraja la mwisho. Najua inauma sana!
Kifua kinakujaa kwa hasira, unatamani kulia kwa sauti kubwa. Nakuomba uamke, usiruhusu machozi yako yaonekane kwa watu wengine. Tafadhali sana simama imara, hebu kuwa kama askari mateka mwenye busara!
Unajua askari mateka wa kivita mwenye busara huwa anakuwaje? Akishakamatwa na maadui hujifanya mjinga. Huvumilia kila mateso na manyanyaso ya maadui, wakati huohuo akipiga hesabu kali za namna ya kuwakabili maadui pamoja na kutoroka.
Ule uzoba kama siyo uzezeta wa askari mateka, pamoja na utiifu wake, huwapumbaza askari maadui, hivyo kupunguza umakini dhidi yake. Na hapo ndipo hufanya kosa. Na pindi askari mateka anapopata mwanya, wale maadui hubaki kusimulia kwa majuto! Hebu tafuta mwanya, ili wanaokudharau wajute!
Haya sasa, hebu tuanze; Wanakusema vibaya, wewe tabasamu. Wanakufanyia dharau waziwazi, jifanye huoni hayo, wewe cheka. Wanakubagua, igiza kwamba hilo siyo tatizo, cheka nao. Chanua tabasamu lako mbele yao.
Acha waseme kuwa wewe ni kabwela kwa maisha yako yote. Siyo kosa lao, ni kwa vile hawajui maisha. Nikupe siri; Yeyote mwenye hulka ya kumcheka asiye nacho, mlemavu wa viungo na kadhalika, mhurumie kwa kuwa hajui maisha na nidhamu yake!
Chukua hii; Wengi waliofanikiwa katika maisha, ni wale waliovumilia manyanyaso ya walimwengu, wakajionesha wajinga. Ni kweli walipata hasira ila walizificha hasira zao. Ukionesha hasira unakuwa mtu wa chuki.
Mungu hapendi mtu wa chuki, maana huwa yupo karibu sana na kisasi. Binadamu wazuri huwaogopa wenzao wenye chuki, hushindwa kushirikiana nao. Chuki zako zitakufanya uogopwe na hata usioneshwe njia za kufanikiwa. Jifunze kutabasamu hata unapoumia.
Ngoja nikwambie; Nelson Mandela ‘Madiba’ alifungwa na Makaburu miaka 27 jela. Walimnyanyasa na kumchukulia uhuru wake. Waliifanya afya yake kuwa dhaifu.
Mandela alikuwa na msimamo lakini alitabasamu mbele yao. Hata walipomtoa jela, aliendelea kukaa nao meza moja, mwisho ikawa sababu ya kufanyika uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia nchini Afrika Kusini na Mandela alishinda na akawa rais wa kwanza mzalendo kuongoza taifa hilo.
Baada ya Mandela kushinda, dunia nzima ikasema: “Tuone sasa, si walimfunga, ngoja awalipizie kisasi!” Mandela wala hakujishughulisha na ulipaji kisasi, alijielekeza kwenye kujenga demokrasia na uchumi shirikishi kwa kila raia wa Afrika Kusini.
Wakati Mandela anafariki duniani, aliweka rekodi ya kuwa mtu anayeheshimika zaidi ulimwenguni, maana kifo chake kiligusa mataifa yote. Mandela angejielekeza kwenye ulipaji kisasi, wala asingevuna heshima aliyoondoka nayo, iliyoifanya dunia nzima ijielekeze Afrika Kusini wakati wa mazishi yake.
Nikupe stori nyingine; Mahathir bin Mohamad akiwa mzalendo hasa kwa nchi yake ya Malaysia, vilevile mwanachama hai wa chama tawala cha United Malays National Organization (UMNO), alionekana kiherehere kwa misimamo yake ya kutetea maslahi ya nchi.
Chini ya utawala wa Waziri Mkuu, Abdul Rahman, Mahathir alifukuzwa kwenye chama cha UMNO, alitimuliwa ubunge kwa kudhalilishwa na kusemwa vibaya sana. Hiyo ilikuwa mwaka 1964.
Mahathir alivumilia miaka sita tu, kwani mwaka 1970, Abdul Rahman alilazimishwa kujiuzulu uwaziri mkuu, vilevile urais wa UMNO. Ni hapo ndipo Mahathir aliporejeshwa kwenye chama, akarejeshewa ubunge wake kisha akateuliwa uwaziri.
Mwaka 1976 Mahathir akawa naibu waziri mkuu na mwaka 1981, alichaguliwa na chama chake kuwa Waziri Mkuu wa Malaysia, ikiwa ni miaka 17 tangu alipodhalilishwa kwa kuitwa msaliti, mchochezi na mwenye kiherehere.
Uwaziri Mkuu kwa Malaysia ndiyo ukuu wa serikali kama ilivyo Urais kwa Tanzania. Wakati Mahathir anakuwa waziri mkuu, Abdul Rahman alishuhudia. Yalikuwa mateso makubwa kwake.
Nakwambia usiwaze kulipa kisasi, jielekeze kwenye ukweli na mihangaiko halali ya kimaisha. Wanaokucheka leo, kesho wanaweza kutamani kuketi meza moja na wewe na wala muda huo usipatikane.
Amka usilie, dunia ina visa vingi hii; Ni kweli inauma kusimangwa lakini mbona wengi waliosimangwa siku hizi ndiyo wanayenyekewa?
Mwanamitindo raia wa Urusi, Natalia Vodianova, mbona alinyanyaswa sana akiwa anauza ndizi barabarani? Alichekwa na beseni lake lenye matunda kichwani, lakini leo hii anaingiza shilingi bilioni 20 kwa mwaka.
Ukisimangwa leo ni njia ya kunyenyekewa kesho; Muone Roman Abramovich. Mtoto wa kimaskini, mama yake alipata mimba nyingine wakati Abramovich akiwa mtoto mchanga.
Kutokana hali duni, na ugumu wa kumlea Abramovich, aliona mzigo utakuwa mzito, akafanya jaribio la kuitoa mimba hiyo. Maskini ya Mungu, hiyo ikawa sababu ya mama yake Abramovich kufariki dunia.
Abramovich alilelewa na bibi yake. Alinyanyaswa kwa umaskini wao, akasemwa kwa kifo cha mama yake wakati wa kutoa mimba, akasimangwa na wenye vyao.
Baadaye alikuwa mmachinga, akijihusisha na uuzaji wa midoli ya kuchezea watoto. Ila sasa ni bilionea wa kuogopwa ulimwenguni. Ndiye mmiliki wa Klabu ya Chelsea, akiajiri makocha, anawalipa fedha nyingi na kuwafukuza. Anasajili wachezaji nyota kwa malipo makubwa. Ameigeuza Chelsea kutoka klabu hohehahe mpaka kuwa tishio Ulaya na duniani kote.
Kisasi ni roho mchafu na ni kifo; Yupo rafiki yetu alibahatika kupata mabilioni ya shilingi kwa ujanjaujanja katika machimbo ya Tanzanite, Mirerani. Alipata awamu ya kwanza akatumia zikaisha, akapata awamu ya pili, nazo siyo tu kwamba hazipo tena, bali na yeye mwenyewe yupo kaburini.
Ndugu yetu huyo alisema analipa kisasi kwa sababu alinyanyasika mno wakati wake wa umaskini. Eti, wanawake walikuwa hawamtaki kwa ubaya wa sura yake pamoja na umaskini aliokuwa nao.
Kwa hiyo alitembea na wake za watu, alivunja ndoa nyingi, aliharibu uchumba wa wengi, maana aliishi na wapambe kwa ajili ya kumtafutia wanawake. Kila mwanamke alimtaka yeye. Wanawake wote waliowahi kumkataa wakati wake wa umaskini, alihakikisha anawapata kwa jeuri ya fedha.
Ndugu yetu aliishi hotelini. Hakukumbuka hata kubadili hali ya maisha ya nyumbani kwao. Na kwa hakika alifanya vurugu. Fedha zilipoisha na afya yake ilidhoofu. Alijaribu kwenda Ulaya ili afiche aibu lakini alirudishwa akiwa taabani. Mauti yalimkuta akiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Unakata tamaa kwa maneno ya walimwengu? Unaona maisha magumu kama vile dunia umeibeba begani? Nikupe siri; Almasi ni madini yenye thamani mno, lakini hukandamizwa na uzito mkubwa zinapokuwa chini ya milima.
Almasi ikishatolewa chini ya mlima, hutamaniwa na kila mmoja. Wewe pia ni almasi. Dunia ni nzito lakini jitahidi, ukishaitua, dunia itakubeba kisha utatamaniwa na kila mtu mithili ya almasi yenyewe.
Mandela, Mahathir, Natalia na Abramovich ni almasi, wao pia walikuwa chini wakikandamizwa na milima lakini baadaye walichomoka kisha dunia ikawabeba. Wakawa tamanio kila mmoja kwa daraja lake, kiutawala, kifedha na kiurembo. Nakusihi tena acha kulia.
Mwanariadha bingwa, Usain Bolt alipata kuandika kwenye akaunti yake ya Twitter: “One day, the people that didn’t believe in you, will tell everyone how they met you.”
Kiswahili; Siku moja wale ambao hawakukuamini, watamwambia kila mtu jinsi ulivyokutana nao.
Tafsiri pana ni kuwa waache wenye kukudharau na hata kukuwekea kauzibe kwenye maisha yako ya kazi. Wala usishindane nao, maana utafika wakati wao ndiyo watakuwa mstari wa mbele kusimulia wanavyokujua na mahali ulipotoka.
Chukua hii; Matumizi mabaya ya muda ni kuusotesha ubongo wako kufikiria magumu ya maisha na kejeli za walimwengu, badala ya kupiga hesabu makini za namna bora ya kubadili kibao cha maisha, kutoka dhiki za kila siku mpaka faraja na neema.
Tambua kuwa maisha ya binadamu yana mengi katikati yake. Zipo kumbukumbu nyingi za kuumiza, zipo pia za kufurahisha. Ni kosa kubwa kwa kesho yako, endapo utaruhusu kumbukumbu za maumivu ziteke hatma yako.
Umetendewa jambo baya, umeumia, sema “asante Mungu”, unachotakiwa kufanya ni kuelewa kuwa kwa vile bado upo hai basi unalo jukumu la kufanya. Maumivu yote weka pembeni.
Ni ukweli kuwa huwa vigumu kusahau unapotendwa mambo mabaya lakini hiyo isikutawale. Amini kuwa ni mapito kisha mwenyewe jisemee moyoni: “Nyakati zijazo zina neema kubwa!”
Asante.
Ndimi Luqman Maloto    
Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment