Na Luqman Maloto
Awali kabisa wakati unasoma mada hii, nakuomba uitafakari
glasi. Fanya tafakuri ya ndani ya kabisa. Utaweza kugundua kuwa thamani yake ni
ikiwa nzima, ikishavunjika ndiyo basi tena. Hutaweza kuirejesha katika hali
yake hata ufanye nini.
Vivyo hivyo katika mapenzi. Ni bora ukiwa nayo,
ukishayachezea na kutoweka ni vigumu sana kuyarejesha. Wapo wanaojuta kwa
kuwapoteza watu waliowapenda kwa moyo msafi kabisa lakini Shetani alipochezea
vichwa vyao, kila kitu kikageuka historia.
Pengine hawajuti leo lakini walijuta huko nyuma. Wapo ambao
walizeeka na kumbukumbu mbaya katika maisha yao. Wakijilaumu kwa ujinga au
uzembe waliofanya na kusababisha wapenzi wao kuondoka. Hapo ndipo kwenye swali,
kwa nini ujute baadaye?
Ni ukweli ulio wazi kuwa huna sababu ya kujuta, badala yake
unachotakiwa kufanya ni kutimiza wajibu wako leo. Siku zote ni lazima ukumbuke
kuwa mapenzi uliyonayo au unayopata kutoka kwa mwenzi wako hivi sasa, yanaweza
kuendelea au kukoma kutokana na uhusika wako.
Janga kuu ambalo limeendelea kusumbua ni kuwa mtu akiwa
nacho anaweza kukifuja utadhani hakitaondoka. Ni kosa kubwa kushindwa kumtunza
mwenzi wako kwa kiburi tu kuwa kwako ameshafika na hataondoka. Usicheze na moyo
wa mwenzio. Usifanye majaribio ya kujuta baadaye.
Kufanya jambo lolote la maudhi kwa mwenzi wako kwa makusudi
ni jaribio la wewe kujuta baadaye. Unayemuudhi ni binadamu, ana moyo kama
ulionao wewe. Siku atakapofanya uamuzi ambao anaona unafaa, itakuwa ndiyo
mwanzo wa majuto yako. Majuto ni mjukuu!
UCHAMBUZI KATIKA MAANA PANA
Unapoingia kwenye uhusiano wa kimapenzi, lengo la juu kabisa
la kwako wewe, linatakiwa liwe kumfanya mwenzi wako afurahi kuwa nawe, vilevile
na yeye awe na msukumo unaofanana na huo wa kuhakikisha unafurahia mapenzi yenu
siku zote.
Kama kila mmoja ataweka nia hiyo na kuitekeleza kwa vitendo,
hapo ndipo unapoweza kuona kitu kinachoitwa ‘malavidavi’ au kwa swaga za
mapenzi tunaita mahabati. Ikiwa ni kielelezo kuwa wahusika wa uhusiano wanakuwa
kwenye kiwango kizuri sana cha kufurahia ‘kapo’ yao.
Tatizo kubwa hutokea pale ambapo wahusika kwenye uhusiano
wanakuwa wanapishana mitazamo au uamuzi. Unajua kabisa hilo unalolifanya
litamuudhi mwenzi wako lakini unakosa hofu, unatenda tu. Siku akisema
“nakwenda” ndipo unashtuka na kudondosha machozi.
Ni kama unavyoelewa kuwa hakuna mtu ambaye anaweza kufurahia
mwenzi wake kusaliti. Unavaa ujasiri na kuanzisha uhusiano wa pembeni.
Anapobaini hilo na kuondoka zake, unapiga magoti kumzuia asichukue uamuzi huo.
Akiondoka unabaki kujutia ulichomfanyia.
Swali; Je, ulipokuwa unafanya mambo ambayo uliamini
yatamuudhi, akili zako hazikuwa timamu? Ukishapata jibu, basi likupe muongozo
kuwa mapenzi hayachezewi kwa sababu moyo wa binadamu siyo mwanasesere. Akishaakisi
maumivu ya kutendwa hisia za kupenda hubadilika kuwa chuki.
Kuiweka hoja hii katika maana inayokubalika ni kuwa mtu
anayekupenda leo, anayekuita majina mengi mazuri hivi sasa, anayetamani kukuona
kila dakika, ni huyohuyo ambaye ukishamkera mpaka mwisho ataanza kukuchukia,
asitamani kukuona na kukubatiza majina ya ovyo kabisa.
Kwa nini jana alikuita “sweetheart, mpenzi, asali wa moyo,
darling” na mengineyo, iweje baadaye akuite “malaya, fuska, kahaba, kicheche,
gumegume au gubegube?” Jibu ni kwa faida yako kuwa kizuri leo ni lazima
kitunzwe, kikigeuka taswira yake ni mbaya kupita kiasi.
Yapo mengi ambayo husababisha mapenzi kufa! Unaonywa kuacha
vitu vibaya ambavyo hata wewe mwenyewe unakiri kuwa havifai. Shetani anatuama
kwenye kichwa chako, unashindwa kubadilika na kurejea mstarini. Hii ni wazi
kwamba matokeo ya kuachana uliyatengeneza mwenyewe.
Hapendi ziara za usiku zisizo na faida wala tija. Mnazungumza
leo, kesho unarejea yaleyale. Siku zinapita anakusamehe lakini hujirekebishi.
Hii ni dunia, anapokutana na mtu ambaye anamuonesha kwamba hatakuwa na shughuli
nyingi za usiku, lazima atamkimbilia.
Shika kile kinachomfaa mwenzi wako, nafasi ya kuhakikisha
utamu wa mapenzi ambao mnauogelea sasa ni yako mwenyewe. Yakipaliliwa, kuwekewa
mbolea na kumwagiliwa, lazima yatamea na kustawi. Yakitazamwa bila matunzo
yoyote husinyaa.
Ikitokea unapanda mbegu wakati zinaanza kuchipua wewe lile
shamba unaligeuza uwanja wa kuchezea mpira, unakanyagakanyaga, ile mimea
itakufa, kwa hiyo na ile mbegu nzuri ambayo uliipanda nayo itapotea. Huo ndiyo
mfano halisi wa mapenzi.
Ina maana kuwa pengine unaweza kuanza vizuri sana katika
uhusiano wako, kile ambacho ulikiingiza kwa mwenzi wako ni mbegu nzuri sana.
Ulipofika muda wa kuweka mbolea na kufanya umwagiliaji ili kile kilichopandwa
kichipue na kustawi, mambo yanageuka kabisa.
Vitendo vyako vinakuwa sawa na yule anayekanyagakanyaga
shamba lake aliyelilima na kupanda mbegu iliyo bora. Usifanye hivyo, maana kila
kibaya unachomtendea mwenzi wako leo, tambua kinamuumiza sana. Kuna faida gani
kwako kumfanya mwenzi wako ateseke?
Je, mateso yake wewe yanakupa ahueni ipi? Kwa walio kwenye
mapenzi ya dhati ni kwamba mwenzi wako anapoteseka, na wewe pia unakuwa kwenye
mateso makali. Maana furaha yake ni yako, maumivu yake yanakugusa pia. Vivyo
hivyo kilichopo kwako naye kinamhusu kwa tafsiri pana.
Juu ya hapo ni kuwa hisia za maumivu katika mapenzi zina
kawaida ya kuhama kutoka upande mmoja kwenda mwingine. Unamtesa sana, siku
akichukua uamuzi wa kusema “mwana kwenu kwa heri”, hapo ndipo unashtuka, eti
huamini kinachotokea.
Maombi ya msamaha kutoka kwako kwenda kwake yanakuwa kwa
unyenyekevu wa hali ya juu sana. Kwa nini mfike huko? Akili yako itumikishe
kufanya uamuzi sahihi ambao ni kumtunza mwenzi wako ambaye anakutunza hivi
sasa. Maudhi ya hapa na pale jiepushe nayo.
Mdharau mwiba guu huota tende! Usione anachokilalamikia
mwenzi wako ni kidogo, mfanye afurahie uwepo wako kila siku. Usimruhusu
akulilie, maana ipo siku utalia wewe. Hakikisha hatoi machozi ya maumivu,
isipokuwa yawe ya furaha. Kinyume chake kuna siku yatakugeuka.
SOMA KWA MFANO
Kuna uhusiano wa Hawa na Matali, vilevile Gaudensia na
Reina. Kila mmoja una soma lake. Hawa alimchezea sana Matali ambaye alipoona
yamezidi aliondoka. Reina naye alijiona kidume, akamtenda sana Gaudensia
aliyeona mazito, akatimka. Baadaye kila mtenda alilia kwa kusaga meno.
Kabla sijaenda zaidi kudadavua mifano hiyo, nieleze tu kwa
kifupi kwamba tamaa na fedha ni sababu kuu ya majuto. Mwanamke au mwanaume,
anaweza kudharau heshima na mapenzi anayopewa na mwenzi wake kwa sababu ya
fedha au ‘upofu’ wa kudhani aliye mbele yake ana mvuto zaidi.
Ni shida! Mwenzi wako upo naye siku zote lakini macho
yanakudanganya kwamba uliyekutana naye barabarani au katika mkusanyiko mwingine
wowote ni mzuri kuliko mpenzi wako. Akili yako inaamini hivyo, matokeo yake
unafanya uamuzi ambao baadaye unaujutia.
Mapenzi yana tabia ya kisasi, utakaposoma mifano ya
Gaudensia na Reina, vilevile Hawa na Matali, utaelewa hili katika sura pana. Siku
zote za maisha yako, jitahidi kubaki njia kuu. Uliyenaye ndiye mwenzi wako,
umetoka naye mbali, kwa hiyo mpende na kumheshimu, achana tamaa zisizo na
kichwa wala miguu.
Ni kweli ana mvuto lakini kabla ya hajakutana na wewe,
ameshavutia wangapi? Je, unadhani aliyekuwa naye kwa nini aliinua mikono na
kumwacha aende? Ikiwa yeye ndiye katendwa, ameshaumizwa mara ngapi? Kwa nini
yeye? Unadhani nafasi yako inatosha kumfanya awe na furaha?
Utaingia kwake kwa kuona ana mvuto unaosuuza moyo wako,
kumbe mwenzio ni mkali wa kuwapanga, hajui kukataa mtu! Siku za baadaye unakuja
kugundua mpo kama sita lakini mwenyewe anajua jinsi ya kucheza karata zake, kwa
hiyo hukuwahi kulijua hilo kabla.
Umeona pesa zake ni bora kuliko penzi safi na salama
unalopata kutoka kwa mwenzi wako. Miezi miwili baadaye unajikuta upo kwenye kundi
la wengine wengi ambao wanamtazama mtu mmoja kwa sababu ya fedha zake. Tayari
unajigundua kwamba uliyenaye si wa uhakika, hana mapenzi, isipokuwa jeuri ya
fedha inamuongoza kufanya uamuzi.
Labda ni fedha zako ndizo zinakufanya uwe na kiburi, unaamua
kumtenda anayekupenda kwa dhati kwa hisia kuwa fedha ndiyo kila kitu. Hao
wanaovutika na wewe, hawaji kwa upendo wenye mguso wa moyoni, wanavutiwa na noti
zako. Unaweza usifilisike lakini kama hali ipo hivyo, siku ukiumwa itakuwaje?
Unahitaji mwenzi wako ambaye utamuona ndiye wako wa kufa na
kuzikana. Anayekupenda kwa dhati, hatakukimbia ukiwa huna fedha au ukisumbuliwa
na maradhi. Atahangaika na wewe mpaka mwisho. Nilishaandika uhusiano wa
marehemu Sajuki na Wastara, waliishi vizuri nyakati ngumu za kusaka mafanikio,
wakala matunda pamoja na katika majanga walishirikiana pamoja.
Hivyo ndivyo mapenzi yanataka, siyo kurukaruka kama kunguru.
Na kila eneo ambalo nimeligusia hapo juu, huwa na matokeo ya kuumiza sana kwa
aliyetenda. Karibu kila mmoja hapo hutamani kurejea kwa mwenzi wake
aliyemfanyia ndivyo sivyo. Sasa hapo ndipo kwenye swali, kwa nini ujute
baadaye?
WASOME REINA NA GAUDENSIA
Walianza uhusiano wao wakiwa chuo! Wote walikuwa wanasoma
Chuo cha Uhasibu, Kurasini, Dar es Salaam ngazi ya diploma. Baada ya kuhitimu
kiwango hicho cha elimu, waliamua kufunga ndoa kabla ya mambo mengine yoyote.
Kwa bahati nzuri, wazazi wa Reina walikuwa na uwezo mkubwa kifedha.
Walimhakikishia mtoto wao kuwa watampa sapoti yote na maisha
yao yasingeyumba! Ndoa ikafungwa, wazazi wa Reina waliwazawadia gari la
kutembelea, nyumba na maduka mawili, moja la vifaa vya ujenzi la pili lilikuwa
la kuuza vyakula kwa jumla. Maisha yanataka nini?
Miezi miwili baada ya ndoa yao, Reina akabadilika kwa
kiwango kikubwa sana. Kuna maneno ambayo hapo kabla hakuwahi kumtamkia
Gaudensia lakini kipindi hicho aliyatamka. Mwanzoni Gaudensia aliyaona kama
majaribu ya ndani ya ndoa lakini siku zilivyozidi kwenda hali ikawa mbaya sana.
Siku za mwanzoni, walikubaliana Reina awe anasimamia mauzo
ya duka la ujenzi na Gaudensia duka la vyakula lakini miezi miwili baadaye,
ilibidi maduka yote awe na anasimamia Gaudensia kwa sababu Reina hakuwa na
muda. Alitoka asubuhi pwee kwenda kujumuika na wanawake wa mjini na alirejea
nyumbani alfajiri akiwa amelewa na siku nyingine hakurudi kabisa.
Gaudensia alivumilia, wakati mwingine alijitahidi kuzungumza
na mume wake ili abadilike lakini haikuwezekana. Reina alimpiga marufuku
Gaudensia kutumia gari walilopewa na wazazi wake. Zaidi ya hapo akawa anachukua
fedha bila utaratibu kwenye maduka yote, Gaudensia akihoji anajibiwa: “Tulia
hizi mali ni zangu, nimepewa na wazazi wangu, hukutoka nazo kwenu.”
Baada ya kuona manyanyaso yamezidi, huku mali walizopewa na
wazazi wa Reina zikizidi kupukutika, Gaudensia akaona isiwe tabu, akaamua
kwenda chuo angalau apate shahada ya kwanza. Alikwenda Udom, hali ambayo
ikamfanya awe mbali na mumewe.
Huku nyuma akawa anapata taarifa za mume wake kuingiza
wanawake mpaka kwenye chumba chao cha kulala. Alivumilia kwa kuhisi kwamba
pengine angeweza kubadilika baadaye. Hata hivyo, mambo yalikuwa tofauti kabisa.
Akiwa chuoni akasikia taarifa kuwa maduka yote yamefilika.
Aliumia sana ila hakujua afanye nini. Alipowalalamikia
wazazi wa Reina, hawakuwa na la kufanya zaidi ya kusikiliza na kukaa kimya. Maisha
yalizidi kupiga hatua kwa kasi ya ajabu, kila likizo alirejea nyumbani lakini
mapenzi kwa mumewe hakupata kabisa.
Reina alirejea nyumbani usiku wa manane akiwa amelewa.
Kipindi hicho maduka yamefilisika na hana fedha kabisa, kwa hiyo akawa kazi yake
kwenda kwa wazazi wake kupiga mizinga ndipo maisha yanakwenda. Hali ilikuwa
mbaya sana.
Miezi kisha mwaka ulikatika, ukafuata wa pili baadaye wa
tatu, mwisho akafanikiwa kumaliza shahada yake ya kwanza ya uhasibu. Ni kipindi
ambacho Reina naye alifanikiwa kupata kazi kwenye kampuni ya Tanzanite One,
Arusha kama mhasibu msaidizi, mambo yake yakawa supa upande wake.
Taarifa za Reina kupata kazi, Gaudensia alizipokea kwa
furaha sana, akampigia simu kumpongeza lakini alipata majibu ya kukatisha tamaa
lakini hakujali sana. Maana alipompigia simu kumpongeza, Reina alijibu: “Sasa
pongezi za nini na inakuhusu nini, kazi nimepata kwa ujanja wangu,”
Gaudensia aliendelea na utaratibu wake wa kila siku, kila
asubuhi ilikuwa lazima ampigie simu kumsalimia, mchana kumjulia hali na usiku
kumtakia usiku mwema. Reina alipogoma kupokea, yeye alimtumia SMS na mambo
yalikwenda.
Baada ya kumaliza chuo na kurejea Dar es Salaam, hakumaliza
siku tatu, aliunganisha Arusha kwenda kuungana na mume wake. Kule palikuwa na
hali mbaya sana. Gaudensia alipoingia ndani kitu cha kwanza cha kumuumiza
kilikuwa ni kukuta boksi la kondomu, na alipotazama kapu la uchafu (dustbin)
chumbani, alikuta kondomu zilizotumika.
Akamuuliza mumewe kuhusu uwepo wa kondomu hizo, akajibu:
“Ulitaka nitembee nao bila kinga?”
Gaudensia: “Reina hebu onesha heshima kwangu, mimi ni mkeo
wa ndoa, unanijibu unavyojisikia kweli, hiyo ni tabia gani?”
Reina: “Tatizo wewe mwanamke una gubu sana, badala ya
kunipongeza kwa kuwa mwangalifu, wewe unanisema kukuta kondomu. Hizi nimeziacha
makusudi ili uone jinsi ninavyojilinda.”
Gaudensia: “Kwa hiyo umeacha makusudi ili kunithibitishia
kuwa ulikuwa ukitembea na wanawake ovyoovyo?”
Reina: “Siyo kutembea
ovyoovyo, kwani wewe ulitegemea muda huo wote ningekuwa bila mwanamke? Acha
utani kabisa, hata wewe kule Dodoma mimi nitajuaje kama siku zote hukuwa na
wanaume? Tena nyie wanafunzi wa Udom kwa wabunge ndiyo zenu.”
Huku akitokwa na machozi, Gaudensia alisema: “Basi baba,
naona umeanza kunitukana, lakini angalia Reina mume wangu, hii ni ndoa,
ilifungwa kwa tamko la jina la Mungu. Unavyoichezea, itakudhuru.”
Baada ya kuzungumza hivyo, Gaudensia alianza kufanya usafi
kwa kuchukua kondomu zote, zile zilizotumika na ambazo hazikuwa zimetumika
kisha akaenda kuzichoma moto. Hata hivyo, maisha hayakuwa na amani kabisa,
vitimbi viliendelea kuchukua nafasi.
Kuna wakati Gaudensia alipigiwa simu na wanawake wa Reina
kumtukana lakini hakuwajibu, alinyamaza na hata mume wake aliporejea nyumbani
wala hakumuuliza. Alichojali yeye ni kujenga ndoa ya yake, aliamini upo wakati
mume wake atabadilika na maisha yatakuwa mazuri.
Uvumilivu wake ulifika ukingoni siku moja baada ya kukuta
karatasi kwenye suruali ya mume wake alipokuwa anafua nguo. Ile karatasi
ilikuwa imeandikwa “WANAWAKE AMBAO NIMESHAWADUU”. Gaudensi akashtuka, akahesabu
majina na kukuta yapo 71.
Gaudensia akagundua kuwa miongoni mwa wanawake hao, wapo
marafiki zake wawili ambao alisoma nao nao Chuo cha Uhasibu, Kurasini, Dar es
Salaam. Kwenye orodha hiyo kulikuwa na wahudumu wa baa na machangudoa. Ilimuuma
sana.
Reina aliporudi nyumbani, ilikuwa usiku wa manane, kwa hiyo
akamuacha alale, asubuhi alipoamka akamuonesha ile karatasi na kumuuliza sababu
ya kuandika na kuihifadhi. Bila kutarajia, Reina aligeuka mbogo. Alimkaripia
kwa kumchunguza kisha akaanza kumpiga.
Alimpiga na kumuumiza vibaya, baadaye alizimia. Reina bila
kujali kama mkewe hana fahamu, aliita gari na kuchukua kila kitu, aliamua
kuhama nyumba. Hata hivyo, mmoja wa vijana waliokuwa wanabeba vitu, aliingiwa
na huruma, kwa hiyo baada ya kushusha vitu, alikwenda kituo cha polisi kutoa
taarifa.
Polisi walifika pale chumbani na kumkuta Gaudensia bado hana
fahamu, walimbeba mpaka Hospitali ya Mkoa wa Arusha, Mt. Meru ambako
alihudumiwa na kurejewa na fahamu. Polisi walimtia nguvuni Reina lakini baada
ya Gaudensia kupona, alikana kupigwa na Reina.
Hakutaka mume wake aingie kwenye matatizo. Pamoja na imani
hiyo lakini Reina hakumjali na alimpiga marufuku kufika nyumbani kwake
alipohamia na alikataa kabisa kumuelekeza. Ilimuuma sana Gaudensia, aliomba
japo nauli ya kurudi Dar kwa wazazi wake lakini alinyimwa.
Ilibidi Gaudensia ampigie simu mama yake na alipomsimulia
mateso aliyonayo, haraka sana alimkatia tiketi ya ndege na ile anafika Uwanja
wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere, mama yake alimwambia: “Mwanangu ni sawa
kuvumilia lakini umetukosea sana, uvumilivu wako ni kama vile huna kwenu, kwa
nini mwanaume akunyanyase kwa kiwango hicho na wewe uwe kimya?”
Dunia ina kawaida ya kurejesha majibu haraka, miezi sita
baada ya Gaudensia kutimuliwa na Reina, tayari alikuwa ameshapata kazi nzuri
katika Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), tayari alishajijenga
sawasawa, akanunua kiwanja akiwa na ndoto za kujenga nyumba ndani ya miezi 10
inayofuata.
Reina alishafukuzwa kazi wakati huo, mambo yalishaharibika,
wazazi wake hawakutaka kumuona. Mtaani alionekana kama kibaka kwa jinsi
alivyochakaa. Maisha yalimdanganya, akarudi kwa Gaudensia kuomba msamaha.
Kipindi hicho Gaudensia anaendesha gari lake aina ya Toyota Land Cruiser Prado
milango mitatu.
Swali ni hili; Haya majuto ya Reina ya nini wakati alikuwa
na nafasi ya kufanya uhusiano wake na Gaudensia uwe bora? Usimfanyie vitimbi
mpenzi wako leo, maana hujui kesho yako ipo vipi. Majuto ya baadaye hayafai
kabisa.
Niongeze hapo kwa kunukuu msemo wa Mbunge wa Same Mashariki
(CCM), Anne Kilango Malecela ambaye ni mke wa Waziri Mkuu Mstaafu, aliye pia
Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu, John Samuel Malecela, aliyewahi kusema:
“Ukimuacha mke unamuongezea PHD.”
Alimaanisha kuwa endapo utamfanyia vitimbi mwanamke wako
kisha ukamtelekeza au kumwacha, usije ukadhani ndiyo utakuwa umemharibia
maisha, badala yake ikae akili kwamba ukimfanyia hivyo unakuwa umemuongezea
akili ya ziada. Usije ukashangaa baadaye ukikutana naye akiwa na maisha bora
zaidi.
Hivyo ndivyo ilitokea kwa Gaudensia, akili yake ilifanya
kazi zaidi baada ya kuachwa na Reina. Matokeo yakawa kinyume kabisa. Reina
akawa anachunga muda wa Gaudensia kurudi nyumbani kwake kisha anakwenda
kujibanza getini kuomba msamaha.
Kwa nini ujute baadaye? Tumia vizuri fursa iliyopo sasa.
Ikiwa ipo wazi kuwa mpenzi wako anakuheshimu na anakupenda, linda heshima hiyo
kwa kutomfanyia mambo ya ajabuajabu, kwani gharama yake ni kubwa sana pale
mambo yanapogeuka kama ambavyo ilimgharimu Reina.
WASOME HAWA NA MATALI
Matali alikuwa mwenye upendo mkubwa sana na Hawa. Alijitahidi
kumpa huduma zote muhimu. Hisia zake zilikuwa wazi mno. Hawa hakugundua hilo mapema,
matokeo yake ule upendo wa Matali aliugeuza fimbo. Alimtenda sana kiasi ambacho
kuna wakati Matali alipoteza kabisa furaha ya maisha.
Hawa kwa kiburi tu kwamba Matali anampenda sana, kwa hiyo
hawezi kumwacha, alimfanyia vitimbi vingi. Kwa mfano; Matali alimpigia simu
Hawa ambaye kwa kujisikia tu hakupokea. Alipomtumia SMS nazo hazikupata majibu.
Hawa aliamua tu kumfanyia Matali vibweka.
Hakuishia hapo, Hawa akaanzisha uhusiano wa pembeni na
wanaume wengine. Matali apoona mambo magumu, ikabidi aachie ngazi. Mwanzoni
Hawa hakujutia, aliona sawa kwamba amepewa nafasi ya kutanua na aina ya wanaume
anaowataka.
“Sitaki mwanaume mzembemzembe mimi, nataka mwanaume aliye
‘fiti’ kimazoezi, mwenye ‘six-pack’ ambaye tukiwa hata ufukweni, akikaa kifua
wazi analipa,” yalikuwa ni maneno ya Hawa akisema mwanaume anayemtaka si aina
ya Matali.
Hawa akawa anajiachia na wanaume wenye six-pack. Miaka
miwili baadaye akashtuka kukuta Matali yupo mbali sana kiuchumi. Kampuni yake ilishapata
mafanikio makubwa. Hawa aligundua hayo wakati ambao wanaume aliowataka
walishampa maumuvi makali.
Baada ya kuhangaika na dunia kwa muda mrefu, mapenzi yakiwa
sawa na msumari wa moto moyoni mwake, akili ilikaa sawa, akaona atafute kazi
ambayo itampa kipato cha kusogeza maisha yake mbele. Hakuna mwanaume mwenye
six-pack hata mmoja aliyemsaidia chochote katika maisha yake.
Dunia ilimwendea mrama, siku moja akasikia tangazo la nafasi
za kazi redioni. Alichukua anwani, akaandika barua, alipoitwa kwenye usaili ndipo
akagundua hiyo kampuni aliyokwenda kuomba kazi, mmiliki wake ni Matali,
mwanaume ambaye alimpa mapenzi yote yeye akayapuuza.
“Ujinga wangu wa kudanganywa na dunia umenikosesha mengi,
leo nakuja kuomba kazi niwe mtumishi wa kawaida, wakati kumbe ningemheshimu
Matali na kuyatunza mapenzi yake, leo hii ningekuwa first lady wa hii kampuni
yake,” aliwaza Hawa.
Baada ya kutoka kwenye chumba cha usaili, aliomba kumuona
Matali. Katibu muhtasi alimjibu yupo ‘bize’ sana. Hata hivyo, wakati anageuka
aondoke Matali alitoka ofisini kwake akiwa kwenye mwendo kasi, alipita anamuaga
katibu muhtasi wake, akamwambia anakwenda kwenye mkutano ofisi ya uwekezaji,
atarejea saa 9:30 alasiri.
Hawa pamoja na
kumuona Matali yupo mbiombio, hakutaka kumpa nafasi, akamzuia mlangoni,
akamwambia: “Please Matali, naomba unisikilize japo kwa dakika moja.”
Matali akamjibu: “Ooh Hawa, sikujua kama ni wewe. Ila kwa
muda huu siwezi kabisa, njoo kesho saa 3:00 asubuhi tutatongea au ukiweza, urudi baadaye saa
11:00 jioni.” Baada ya kumjibu hivyo, Matali alimuunganisha Hawa na katibu muhtasi
wake.
Hawa hakutaka kwenda nyumbani, alizungukazunguka, saa 10:30
alasiri alirejea ofisini kwa Matali. Saa 11:00 alikuwa kwenye kiti anatazamana
na Matali. Alipigwa na mshangao kukutana na ofisi nadhifu ambayo ilionesha wazi
kuwa inatunzwa kwa gharama kubwa.
Bila aibu, Hawa alishindwa kuvumilia akaanza kuomba msamaha.
Alikumbuka mengi kutoka kwa Matali, akakiri kuwa ni mwanaume wa kipekee kwake,
aliyekuwa na mapenzi ya kiwango cha juu mno kuwahi kutokea katika maisha yake.
Alitamani yote ya nyuma yajirudie.
Ni kipindi ambacho aligundua kumbe Matali ni mwanaume mzuri,
ana sura nzuri, umbile la kiume, mrefu. Mwanzoni kwa tamaa za dunia hakuyaona
yote. Ni hapo ndipo swali linafuata; Kwa nini Hawa anajuta baadaye wakati
alikuwa na fursa pana akaichezea?
HITIMISHO
Mapenzi ni fursa, jaribu kumheshimu na kumlinda uliyenaye. Wengi
hutambua uzuri wa wapenzi wao muda mrefu
baada ya kuharibu. Zingatia hisia za mwenzi wako, anapokwambia anakupenda,
jaribu kuheshimu. Usithubutu kumtenda maana ukifanya hivyo ni lazima itajirudia
kwako baadaye na kujuta.
Tambua kwamba mpenzi
mbaya ni kwa sababu upo naye, akishaondoka halafu ukakutana na wabaya wenyewe, akili
itakurejesha kwa yule uliyemchezea kisha utaanza kujuta ila majuto ni mjukuu! Bahati
mbaya ni kwamba unaweza kutaka kurudi kwake kipindi ambacho ameshawahiwa na
anayemthamini kwelikweli.
0 comments :
Post a Comment