Na Luqman
Maloto
NYOTA wa
soka jicho la Watanzania, Mbwana Ally
Samatta, ameendelea kuiweka hai furaha ya Watanzania.
Kuanzia tuzo
ya Mwanasoka Bora Afrika kwa wachezaji wa ndani, kusajiliwa barani Ulaya kwenye
timu ya Koninklijke Racing Club Genk (KRC Genk) ya Ubelgiji na baadaye kuanza
vizuri kwa kutikisa nyavu ni mambo yaliyawapa burudani Watanzania.
Februari 28,
mwaka huu, Samatta alifunga goli muhimu, lililoiwezesha KRC Genk kupata ushindi
wa mabao 3-2 nyumbani dhidi ya vinara Ligi Kuu ya Ubelgiji, Club Brugge KV.
Mambo mswano
kabisa! Kila jema ambalo Samatta analifanya ndivyo anavyowatoa kimasomaso
Watanzania.
Watanzania
waliomba na kutarajia na hakika imekuwa kweli. Hongera sana Mbwana kwa kutwaa
tuzo ya Mwanasoka Bora Afrika kwa wachezaji wa ndani ya Bara la Afrika kisha
kupata matunda mema Ulaya.
Tuzo ya Samatta
na mafanikio yake kwa jumla, yana maana kubwa kwa mtu yeyote anayehitaji
mafanikio. Neno moja tu lina uzito wa kutosha kutoa tafsiri pana ya hatua
anazopita mchezaji huyo aliyetokezea Mbagala, Dar es Salaam.
Na neno
lenyewe ni nyakati. Naam! Samatta alizitafuta na sasa amefikia wakati wake,
ilikuwa lazima ashinde tuzo kisha kupata mafanikio Ulaya ambayo ameanza nayo
kwa sababu huu ni wakati wake.
Samatta
ilikuwa vigumu mno kwake kushinda tuzo mwaka jana, na kutikisa Ulaya hapo kabla
kwa sababu haukuwa wakati wake.
Mwaka jana
na mingine michache iliyopita ilikuwa awamu yake ya kutikisa kwenye Klabu ya TP
Mazembe ya DRC.
Mwakani anaweza
kushinda tuzo nyingine kubwa zaidi, yaani ile ya Mchezaji Bora wa Afrika (tuzo
ya jumla) kama itakuwa ni wakati wake. Na anaweza kushinda tena na tena!
Mafanikio ya
Samatta yanamaanisha nini? Jawabu moja, attitude! Hicho ni Kiingereza,
Kiswahili tunaita hulka.
Wapo
wachezaji wengi wamepita nchini, walikuwa na vipaji pamoja na viwango vikubwa
kuliko Mbwana lakini hawakuweza kufika popote kwa sababu ya hulka (attitude).
Hulka bora
ndiyo nidhamu. Wapo wachezaji wa soka walimaanishwa kutikisa nchini na duniani
kwa jumla wakitokea Tanzania, lakini hulka zao ziliwaponza. Madini yao ya ndani
ya uwanja, yameishia mchangani! Maskini yao!
Lazima
kuheshimu hulka ili kutumia wakati wako vizuri. Na hii ni kwa kila fani, siyo
katika soka peke yake.
Mwanamuziki
Diamond Platnumz au Nasibu Abdul Juma, anatikisa Afrika kwa sasa akitokea
Tanzania, ni kwa sababu hulka yake ilimfanya aufanye wakati wa sasa kuwa
mwafaka kwake.
Yeyote
anayejituma, na akiwa na hulka njema, anaweza kufanya maajabu yenye kugeuza chupa
kuwa almasi.
Na mafanikio
ya Samatta na Diamond, yawe fundisho kwa kila mmoja kutambua wakati wake na
kuutumia vizuri kufika mbali na kupata mafanikio stahiki.
Wapo wengi
hawakutumia vizuri nyakati zao. Alikuwepo fundi Haruna Moshi ‘Boban’,
akasajiliwa Gefle IF ya Sweden mwaka 2010. Akatarajiwa kufika mbali. Haikuwa
hivyo, alirejea nchini kwa kususa na alipofika Bongo, hakuwa Boban yule tena!
Ameishia
wapi Athuman Idd ‘Chuji’? Alikuwa kiungo aliyekamilika kiukweliukweli.
Alihitaji nidhamu tu, yaani kuwa na hulka kama za Samatta, hakika dunia nzima
ingemwelewa.
Jaribu
kuwaza kipaji cha Boban, halafu angeongezewa na nidhamu ya Samatta. Jibu
unaweza ukawa unalo ni wapi ambapo leo hii angekuwa.
Mlete Chuji
kwenye mawazo yako, kifikirie kile kiwango chake, hapohapo itoshe kukupa jawabu
kuwa wacheza soka wa Tanzania walitakiwa kuwa wenyeji wa Ulaya miaka mingi
nyuma ila wamekuwa wakiponzwa na hulka zao.
Shika
muongozo kuwa juhudi na nidhamu huvuta bahati, kisha bahati ndiyo itakufanya
ufike kwenye kipindi chako cha mafanikio. Kwa hiyo hulka inapaswa kuanza kabla
ya vyote.
Muongozo ni
wewe kujituma na utakapofika kwenye wakati wako, hakikisha unautumia vizuri ili
utakapopita, watu waseme “alikuwepo fulani bwana!”
Pambana
kwenye eneo lako ili utengeneze wakati wako mzuri. Utakuwa mwenye kupendwa na
kuheshimika sana kama utafikia wakati wako na kufanya kile kinachohitajika.
Kila
mwanasoka, hususan wale chipukizi, wanalo la kujifunza kupitia kwa Samatta,
vilevile wajiongeze kutoka walipokwama akina Boban, Chuji na wengine ambao
walikwama njiani kutokana na hulka zao.
0 comments :
Post a Comment