UMEWAHI
kujiuliza ni kwa nini Mbwana Samatta siyo mtoto wa Said Salim Bakhressa?
Vipi kuhusu
Diamond Platnumz, ni kwa vipi siyo mwana wa Rostam Aziz?
Je, Hasheem
Thabeet, si angekuwa mtoto wa Ally Mufuruki?
Mbona Lionel
Messi hajawa mtoto wa Bill Gates? Cristiano Ronaldo kuwa mwana wa Warren
Buffet, Floyd Mayweather Jr kuwa mtoto pendwa wa Carlos Slim Helu. Ni kwa nini
haikuwa?
Ili maji yafuate mkondo Ronaldo de Lima si
angekuwa mtoto wa Mfalme Pele? Galacha wa kikapu, Bill Russell ni kwa nini siyo
baba wa Michael Jordan? Au Magic Johnson si ingependeza akawa baba yake LeBron
James?
Ukiwa na
jawabu ni kwa nini bondia mkali kuwahi kutokea duniani, Joe Louis siyo baba wa
Mike Tyson, haitakusumbua leo kuona kuwa Muhammad Ali siyo kizazi cha mbavu
nene ulingoni, Jack Johnson.
Mayweather
Sr, hakuwa bondia tishio kwa wakati wake lakini ndiye baba wa Mayweather Jr. Vipi
Sugar Ray Robinson mbona hakuna aliyemfuata katika masumbwi? Sanasana mwanaye, Ronnie
Robinson alijikita zake kwenye mchezo wa roller derby.
Chukua siri
hii; Mungu hufanya uteuzi katika mazingira ambayo wengi hawayatarajii. Hata
manabii wake, nazungumzia wale wa ukweli, wengi walitoka katika mazingira duni
kabisa.
Bikira Maria
(Mariam) alikuwa nani mpaka abebe mimba ya Yesu (Isa bin Mariam)? Au Aminah
bint Wahb mbona alikuwa wa kawaida tu lakini ndiye mama wa Mtume Muhammad
(S.A.W). Mungu huteua anavyotaka!
Mungu
amekuwa na utaratibu usiokoma, wa kupandikiza uzao wa matajiri na wafalme
katikati ya familia zinazoishi kwenye lindi la umaskini.
Ni kawaida
kabisa Mungu kuingiza kipaji kikubwa kwenye familia ya watu wasio na vipaji. Mwanamke
anaweza kunasa mimba ya mwanaume mlevi au jambazi lakini mtoto akatoka
mchamungu wa mfano. Mungu hupanga!
Angalia
familia ya Manara, watu waliokuwa na vipaji pamoja na uwezo mkubwa wa soka,
Kassim, Kitwana na Sunday ‘Computer’, mbona hatuoni nyayo za watoto wao?
Justin
Bieber ni mwanamuziki tajiri duniani, ila mama yake, Pattie Mallete alikuwa
mtumia unga, akawa pia kibaka, baba yake, Jeremy Bieber, alikuwa mlevi
kupindukia. Ila walipokutana, ilipatikana mimba, akazaliwa Justin ambaye leo
hii ameishika dunia kwa muziki wa Pop.
Kama Pattie
Mallette angebeba mimba ya Michael Jackson kwa vile ni Mfalme wa Pop, hakika
asingepatikana Justin Bieber. Nina uhakika hili huwezi kubisha hata kidogo,
maana Justin ni muunganiko wa kibaiolojia kati ya Jeremy na Pattie.
Watu wengi
hutamani kuzaa na watu wenye hadhi ya juu kwa kudhani ndiyo watapata watoto
wazuri. Huko ni kujidanganya! Mambumbumbu, makuli, wapigadebe, wasukuma maguta,
wamachinga, mama ntiliye na wengine wengi ndiyo huzaa watu wakubwa. Matokeo
yameonesha hivyo!
Ni nadra
sana kumpata George Bush, Rais wa Marekani kisha na mwanaye (George Bush Jr)
kuwa rais wa nchi hiyo baadaye, au Uhuru Kenyatta kuongoza taifa la Kenya ambalo
lilikombolewa na baba yake Jomo Kenyatta kutoka kwa Muingereza.
Tawala za
kifalme inawezekana kwa sababu ni kurithishana, ila katika nchi zenye uchaguzi
wa kidemokrasia ni vigumu.
Na hapo
ndipo unajionea mwenyewe kuwa Barack Obama, maskini wa Kijaluo mwenye asili ya Kenya,
leo hii ni Rais wa Marekani, tena kwa vipindi viwili. Dk. John Pombe Magufuli,
mtu duni kutoka Chato, Geita, kwa sasa ndiye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
Usijindangaje
kuwa ukizaa na Edibily Lunyamila atapatikana Lunyamila Jr. Au mtoto wa Ali Kiba
naye aje aitwe King Kiba Jr. Mr. Nice kumleta mfalme mwingine wa Takeu kutoka
kwenye maungo yake, vivyo hivyo kwa akina Muumini Mwinjuma, Ally Choki, Banza
Stone, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’, Joseph Haule ‘Prof. Jay’. Ni mpaka Mungu apange!
Haikuhitajika
muunganiko wa damu ya Mwalimu Julius Nyerere kumpata Zitto Kabwe au Oscar
Kambona ili azaliwe Edward Lowassa, Kwamba Halima Mdee atokee kwenye kizazi cha
Bibi Titi Mohamed au Mashavu bint Kabonge ndiye amzae Anne Kilango Malecela,
vivyo hivyo Ester Bulaya awe mjukuu wa Tatu Mzee. Vipi Ummy Mwalimu kuwa damu
ya Binti Kipara? Mungu hateui hivyo!
Hii ndiyo
sababu Sir Isaac Newton, yatima ambaye hata hakumuona baba, akakosa malezi ya
mama ambaye alichukuliwa na mwanaume, yeye akiwa bado mchanga, akabaki kulelewa
na bibi, lakini ndiye mwanahisabati na sayansi ambaye atakumbukwa nyakati zote
kutokana na uvumbuzi wake.
Mtazame
Aristotle, mtu aliyekuwa na kichwa cha ajabu mno ambaye atakumbukwa na vizazi
vyote! Lakini ni mtoto wa mtumishi wa mfalme. Bila shaka mfalme angetamani
kupata mtoto kama Aristotle lakini Mungu hakumpa.
Hakuna
aliyewahi kujichagulia wazazi, unajikuta tu ndani ya familia ya kimaskini kama
ambavyo mtoto wa Bill Gates alishtukia yupo ndani ya familia yenye baba na mama
wote matajiri. Ndivyo ilivyo kwa watoto wa marais, viongozi wakubwa, maskini wa
kutupwa na kadhalika.
Kuzaliwa
maskini siyo laana wala kituko. Mjinga pekee ndiye anaweza kumcheka mtoto
aliyezaliwa kwenye familia ya kimaskini. Tangu enzi, Mungu amekuwa na utaratibu
wa kupandikiza watu wakubwa, matajiri, viongozi wenye heshima na hata wafalme
ndani ya nyumba za maskini.
Abraham
Lincoln alizaliwa maskini, aliishi kimaskini akizingirwa na hali duni mno,
mwisho akawa Rais wa Marekani baada ya kutokata tamaa. Mtoto wa Lincoln akaitwa
mwana wa rais, lakini hakuweza kuyakamata masafa ambayo baba yake alisafiri.
Musa
alizaliwa kwenye familia hohehahe lakini ndiye aliyemaliza jeuri ya Firauni.
Watu wengi mashuhuri ulimwenguni, walitoka kwenye familia duni lakini
wakapambana na kupenya katikati ya ‘wakubwa’, wakaketi meza moja kabla ya
kuanza kuongoza msafara. Ni mara nyingi tu watwana wamegeuka mabwana!
Tafakari
kidogo kuhusu namna Nelson Mandela alivyoilazimisha dunia kumnyenyekea na kumtukuza
wakati mwanzoni walimwita gaidi. Ni Mandela mmoja tu duniani, hakuna mwanaye
wala mjukuu wake kama yeye.
Ndivyo
ilivyo kwa Oprah Winfrey! Nani wa kumcheka leo? Ana kila kitu ambacho kila
mwanamke anapenda awe nacho. Amefikia mafanikio ambayo binadamu wote wangependa
kuyafikia. Waliomcheka siku za nyuma, wanatamani siku zirudi nyuma waanze
kumheshimu na kumnyenyekea tangu akiwa amevaa magunia yake.
‘Akili-kushindwa’
wanaishia tu kusema: “Usimuone vile Oprah, alikuwa anavaa magunia ya kubebea
viazi, tulikuwa tunamcheka!” Shombo ya jana ni historia kama aliyekuwa ananuka,
alipata sabuni na kuoga. Ni kituko kama siyo kichekesho kusema fulani alikuwa
ananuka, wakati ni nadhifu na ananukia leo.
Iwe kuongea
kwa kujifariji, kuponda au kumpongeza, ukweli unabaki palepale kuwa Oprah
wazazi wake hawakuwa na uwezo wa kumnunulia nguo, wakawa wanaungaunga magunia
ya kubebea viazi, wakayatengeneza kama nguo za kumvisha binti yao.
Leo hii
anabadili nguo anavyotaka. Yale maduka wanayoingia viongozi wakubwa wa Marekani
na dunia pamoja na matajiri wanaoheshimika ulimwenguni, ndiyo na yeye anaingia
kufanya manunuzi humohumo.
Ishi kwa
tabasamu kila siku. Hata uwe ndani ya nyakati ngumu kiasi gani, elewa tu kuwa
utavuka. Mungu aliyekuumba anakuona, analo fungu lako bora kabisa.
Jambo la
kutambua na kuheshimu ni kuwa Mungu anajua namna ya kukupa mafanikio. Anaweza
kukufanikishia ukiwa kijana, wakati wa makamo au hata uzeeni.
Mafanikio
yanaweza kuja kwako moja kwa moja (direct) au kupitia mlango wa nyuma
(indirect). Ila yote ni mafanikio yako.
Mafanikio
mlango wa nyuma; Yale ya kuja moja kwa moja hayahitaji ufafanuzi, kwa upande wa
yenye kuja kupitia mlango wa nyuma ni kama vile mzazi kuvuna kupitia kwa
mwanaye aliyemzaa na kumlea kwa tabu au hata mtoto aliyemuasili na kumlea.
Hii ikupe
muongozo wa kutambua kuwa mtoto ni zawadi. Omba Mungu akuongoze na usibague,
maana hujui kuwa pengine huyo unayembagua ndiye mama au baba wa daktari bingwa
atakayegundua dawa za Ukimwi, Homa ya Ini (Hepatitis B na C), Kisukari na
kadhalika. Mheshimu kila mtu!
Mtoto wako
mtunze, mpe malezi bora kadiri Mungu anavyokujalia. Huwezi kujua kuwa pengine
huyo ndiye mkombozi wako.
Wewe mtoto,
ukizaliwa kwenye familia ya kimaskini, ikuongoze kuchangamsha ubongo. Wewe
ndiye shujaa wa familia yako, jitume ubadili hali ya maisha ya wazazi wako na
ndugu zako.
Kuzaliwa
kwenye familia maskini ni ishara kuwa wewe ni mfalme. Ukipambana na kufanikiwa,
unaitwa mfalme. Watoto wa Bakhressa wana fedha lakini siyo wafalme. Wamekuta
mteremko wa maisha!
Unabisha?
Daud alikuwa na uwezo gani wa kuwa Mfalme wa Israel mbele ya Saul? Daud alikuwa
mtu duni kabisa lakini ndiye alimpiga Goliath. Usicheze na Mungu na uteuzi
wake!
Zingatio kwa
mama; Usitoe mimba, usinyonge kichanga wala usitelekeze mtoto. Huyo anaweza
kuwa ndiye ameletwa na Mwenyezi Mungu kuwa mafanikio yako ila wewe unayakataa.
Baba;
Usikatae mimba, usiwe chanzo cha mimba kutolewa, usikimbie damu yako, hakikisha
unakuwa mlezi bora wa mwanao kwa hali na mali. Huwezi kujua ni zawadi gani
ambayo mtoto huyo ametumwa na Mungu akuletee.
Wazazi;
Hakikisha mnatoa malezi bora kwa watoto. Kile ambacho mnakifanya, kiwe ndiyo
uwezo wa juu kulingana na nafasi. Wapeni watoto mapenzi makubwa na muwafanye
wawe na furaha. Hao ni hazina yenu ya baadaye.
Mtoto; Wewe
siyo chochote bila wazazi wako. Wangeamua, ungetolewa ukiwa mimba changa.
Unapopata mafanikio, elewa kuwa wazazi wako wana thumni yao kwenye kila jasho
lako. Wafanye wazazi wako wafurahie kipato chako, usiwaache wakipata shida na
wewe upo ilhali uwezo wa kuwasaidia unao.
Mafanikio
yako yatapaa zaidi, vilevile utakuwa ni mwenye kubarikiwa mno kama wazazi wako
utawalinda kadiri kipato chako kinavyoruhusu.
Nakutakia
Ijumaa Kareem.
Ndimi Luqman
Maloto


0 comments :
Post a Comment