Na Luqman
Maloto
Serikali ya Rais
John Magufuli dhidi ya upinzani, kwa hali ilivyo hivi sasa, hasa Tanzania Bara,
ni sawa na msanii maarufu (supastaa) dhidi ya yule ambaye bado anahangaika
kupata mafanikio (underground artist).
Hali hiyo ni
upinzani na vyama vyao kwa jumla, yaani ACT-Wazalendo, muungano wa vyama
vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na vingine vyote.
Kipindi cha
utawala wa Rais wa Nne, Dk. Jakaya Kikwete, serikali na upinzani, hususan Ukawa,
walikuwa na mvutano mkubwa na walipimwa kwa nani zaidi kama vile klabu za soka
za Simba na Yanga.
Kipimo cha
upinzani na serikali katika kipindi cha kati ya mwaka 2005 na 2015, zaidi 2010
kuelekea 2015, ilikuwa sawa na mchuano wa wanamuziki wa Bongo Fleva, Nasibu
Abdul ‘Diamond Platnumz’ na hasimu wake Ali Kiba. Wafuatiliaji wa muziki wa
kizazi kipya wanaelewa minyukano ya wasanii hao.
Kwa kawaida Serikali
lazima iwe juu lakini pia upinzani ulikuwa juu mno kipindi cha awamu iliyopita.
Na wakati mwingine upinzani ulitengeneza vichwa vya habari katika zile habari
kiongozi (lead stories) kwenye magazeti kuliko serikali na Chama Tawala (Chama
Cha Mapinduzi ‘CCM’).
Zipo nyakati
wahariri wa magazeti waliambizana: “Habari za upinzani zinauza kuliko za CCM na
serikali.” Na kwa sababu ya shabaha ya kulenga soko, ikabidi wapinzani
wamulikwe na wapewe nafasi.
Ilikuwa
wapinzani wakifanya tukio, na Serikali wakifanya tukio lao, wahariri
wanachekecha na kufanya mchezo wa kuchagua kwa kubahatisha, ‘ana anado’, ipi
habari kubwa.
Haikuwa na
tofauti yoyote na ambavyo Diamond na Ali Kiba wakitoa nyimbo kwa kufuatana,
jinsi ambavyo ma-DJ wa redio na televisheni pamoja na watangazaji
wanavyochekecha na kuzipima upi bora kuliko mwingine.
Kwa kawaida
wimbo wa Diamond, Ali Kiba na nyota yoyote yule anayetambulika, ni rahisi
kuchezwa redioni na kwenye televisheni hata kama siyo mzuri kutokana na jina
ambalo amekuwa amejitengenezea.
Redio
zinaachaje kuucheza wimbo mpya wa mwanamuziki Vanessa Mdee au Barnaba wa THT hata
kama siyo mzuri? Wataucheza tu! Baadaye utakaposhindwa kutamba, hayo ni matokeo
ya baadaye lakini unakuwa umeshachezwa kutokana na nguvu ya jina la msanii.
Msanii
asiyefahamika (underground artist), akitoa wimbo ili uchezwe inabidi afanye
kazi hasa. Na wimbo wenyewe uwe na ubora usiotia shaka ili kuwashawishi
watangazaji na ma-DJ ambao hawamfahamu kabisa.
Watangazaji
na ma-DJ wenyewe wanaangalia wimbo umeimbwa na nani. Hivyo, ili wimbo wa
underground uchezwe ni lazima uwe na viwango vya kumshawishi DJ na mtangazaji
kuucheza.
Kama siyo
kumshawishi DJ au mtangazaji, basi wimbo uwe umepenya kwenye nyoyo za watu
ambao wataomba uchezwe. Na kwa sababu redio ni kwa ajili ya msikilizaji,
runinga kwa mtazamaji, basi wimbo ukiombwa utachezwa.
Waandishi wa
magazeti nao wanajua msanii gani akiandikwa ndipo gazeti linakuwa na heshima.
Ili msanii chipukizi apate nafasi ya kuandikwa hapo ni lazima awe anafanya kazi
yenye nguvu ya kumshawishi mwandishi husika.
Hali hiyo ya
masupastaa wa muziki, imekuwa sawa na siasa za Tanzania kwa wakati huu, hususan
Tanzania Bara. Hapa sigusii Zanzibar kabisa!
Ghafla
Serikali ya Rais Magufuli imekuwa supastaa (msanii maarufu). Upinzani kwa sasa
umekuwa underground (msanii asiyefahamika).
Kila kazi au
tukio linalofanywa na serikali yake, linakuwa kivutio cha vyombo vya habari
hata kama ni la kawaida tu. Ni sawa na msanii supastaa kutoa wimbo wa kawaida,
utapewa kipaumble cha kuchezwa.
Upinzani kwa
sasa ili upate nafasi ya kusikika vizuri na kupata kipaumbele kwenye vyombo vya
habari, inatakiwa wawe na matukio yenye nguvu kubwa. Ni sawa na msanii
underground kutoa wimbo wenye mvuto usiotia shaka.
Kitendo cha
upinzani kufanya matukio yenye nguvu ndogo, ni kusababisha Magufuli na serikali
yake kuendelea kung’ara katika vyombo vya habari kwa matukio ya kawaida tu.
Hiyo ni sawa
na wimbo wa msanii mdogo kutochezwa redioni au runingani kwa sababu ubora wake
ni wa kawaida lakini wa supastaa ambao ni wa kawaida unachezwa vizuri kabisa.
Umaarufu unalipa!
Alama za
nyakati zinafaa kuwasha taa kuwa Serikali ya Magufuli imeweza kupata umaarufu
mkubwa tangu kuanza kwake kazi, hivyo ni jicho la kwanza la vyombo vya habari
kabla ya upinzani.
Nyakati za
sasa zinataka wapinzani wawe wabunifu. Kutazama ni matukio yapi ambayo
wakiyafanya yatachukua nafasi pana kwenye vyombo vya habari ili kushindana na
matukio ya kawaida ya Serikali ya Dk Magufuli.
Kama uteuzi
wa Katibu Mkuu wa Chadema Dk. Vincent Mashinji ulizidiwa na uteuzi wa wakuu wa
mikoa, hapo lazima kutambua ipo kazi inatakiwa kufanyika kwa upinzani, kukabili
mvuto wa Serikali ya Magufuli.
Vilevile
itakumbukwa kuwa tukio la muundo wa safu mpya ya sekretarieti ya ACT,
halikupata nguvu kubwa. Ni vizuri kutambua mapema mahali ambako vitu haviendi
kwa unyoofu wake ili marekebisho yafanyike.
Hapa niweke
wazi kuwa sina maana kuwa wapinzani hawana jipya ila huu siyo muda wake.
Magufuli amekuwa na mtindo mpya ambao umewafanya Watanzania wakumbatie ‘kipya
kinyemi’.
Hiki ni
kipindi ambacho neno la Dk Magufuli lina nguvu kuliko matukio ya Ukawa na ACT.
Ni wakati ambao ukitaka usemwe vibaya au hata kuzomewa umkosoe Magufuli na
matendo yake ya kutumbua majibu.
Kwa nini umaarufu wa upinzani
umeshuka?
Jibu ni
kwamba hawajaonesha jipya katika utendaji wao wa kila siku. Mtindo wa miaka 10
ya kipindi cha Dk Kikwete, unatakiwa ufanyiwe mabadiliko makubwa ili kuendana
na kasi.
Upinzani wa
kipindi cha JK, hauwezi kushabihiana na wa Magufuli. Ni marais wawili kutoka
Chama Cha Mapinduzi lakini mtindo wao wa uongozi ni tofauti kabisa. Ikulu ya JK
na ile ya Magufuli, ni tofauti mithili ya jua la asubuhi na mchana.
Hivyo, ni
vizuri kuangalia namna mpya ya kufanya siasa za upinzani kulingana na kasi ya
Magufuli. Ni dhambi kubwa kwa upinzani kubaki kimya na kuiacha serikali iliyo
madarakani ikichanja mbuga yenyewe kwa kujidai.
Upinzani
kunywea dhidi ya serikali ni ukosefu wa ubunifu. Kinachotakiwa sasa hivi ni
kuwa kadiri inavyopaswa kuwa ni lazima wapinzani wazame ndani na kuibua kasoro
za kimsingi ambazo zinatendeka serikalini.
Hali
ilipofikia kwa sasa ni kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, kauli
zake zimekuwa na nguvu kuliko matamshi ya viongozi wakubwa wa upinzani kitaifa?
Umuhimu wa wapinzani kujinoa upya unaonekana waziwazi.
Ikumbukwe
kuwa Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe ambaye pia mwenyekiti
wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), mwezi uliopita alifanya mkutano
na waandishi wa habari kukosoa mtindo wa Magufuli wa kutumbua majipu.
Maneno yake
yalipata nguvu kiasi gani? Mapokeo hayakuwa yale ambayo ilitokea miezi kadhaa
kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu 2015. Wala hiyo isiitwe hali ya hatari, ni
tahadhari au fundisho kuwa hizi ni zama tofauti kabisa.
Bunge la
Januari mwaka huu, tulishuhudia jinsi hoja chache za wapinzani zilivyoweza
kutia ladha ya mijadala bungeni. Wabunge, Zitto Kabwe wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo)
na Tundu Lissu wa Singida Mashariki (Chadema), waling’ara vilivyo.
Taswira ya
bunge la Januari, ilitosha kuonesha kuwa bado wapinzani wanayo nafasi kubwa ya
kutamba kwenye siasa za nchi. Kinachotakiwa ni wakati gani na hoja zipi za
kusimamia.
Hapa ndipo
hoja ya msingi ya wapinzani kuhitaji santuri bora zaidi inapoibuka. Mwanamuziki
anapoona mzunguko wa nyimbo umebanwa na nyimbo nzuri au za wasanii maarufu
zaidi, anachotakiwa kufanya ni kufyatua tungo bora yenye uzani kuliko nyingine
zilizopo kwenye mzunguko.
Kipindi hiki
ambacho mzunguko wa habari ni msisimko wa Rais Magufuli mpaka katika mitandao
ya kijamii, kinachotakiwa ni wapinzani kuibuka na matukio au hoja zenye afya
kuzimisha mvuto wa Dk Magufuli.
Hapo
inahitaji kufikiri kwa makini, vilevile ubunifu unahitajika. Siasa za mazoea
hazitawasaidia wapinzani kwa wakati huu.
Huu siyo
wakati wa JK. Hata nyimbo za msibani na harusini haziwezi kuwa sawa. DJ mzuri
wa nyimbo za mapambio kilioni, hata mara moja hawezi kuwa hodari klabu.
Nasubiri kuona mwamko wenye nguvu wa upinzani lakini gia lazima ibadilike.
0 comments :
Post a Comment