ads 728x90 B

ANNE SEMAMBA MAKINDA Spika bora asiyepewa heshima yake







Luqman Maloto
ULITOKEA mgawanyiko mkubwa wa kimawazo pale Anne Semamba Makinda, alipobarikiwa na Kamati Kuu ya CCM, kuwa mmoja wa wanawake watatu waliopigiwa kura na wabunge wa CCM baada ya Uchaguzi Mkuu 2010.
Yalizungumzwa maneno mengine zaidi baada ya Makinda kuchaguliwa na wabunge wa CCM kama mwanamke chaguo la kwanza kati ya wanawake watatu waliopitishwa kuwania Kiti cha Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa hoja tu kuwa “ni zamu ya mwanamke”.
Kwamba ulikuwa muda wa mwanamke kwa sababu tangu uhuru, haikuwa imewahi kutokea kwa mhimili wowote wa dola, Serikali (Executive), Bunge (Parliament) na Mahakama (Judiciary) kuongozwa na mwanamke.
Kamati Kuu ya CCM (CC), ilifanya uamuzi kwamba ni zamu ya mwanamke, hivyo wanaume watatu waliokuwemo kwenye mchakato waliondolewa.
Walioondolewa ni Spika wa Bunge la Tisa, Samuel John Sitta, aliyekuwa anatetea kiti chake, wa pili ni mwanasiasa mtata, aliyetajwa kwenye kashfa nyingi za ufisadi Tanzania, Andrew John Chenge na Mbunge wa Kongwa, Job Yustino Ndugai ambaye yeye alipozwa kwa kuteuliwa kuwa Naibu Spika wa Bunge na sasa ndiye Spika wa Bunge.
Bungeni, Makinda alishinda kwa kura nying, aligombea na mwanasiasa mkongwe nchini, Mabere Nyaucho Marando (Chadema). Huo ndiyo ukawa mwanzo wa kushika majukumu makubwa zaidi nchini, lakini zaidi akiwa mwanamke wa kwanza kuweka rekodi kubwa ya kuongoza mhimili namba mbili kati ya mihimili mitatu ya dola.
Pamoja na mafanikio yote hayo, Makinda alikumbana na ukosoaji kila kona, kutoka kwa wanasiasa na vyombo vya habari. Walimponda kuwa hatakuwa na uwezo wa kulimudu Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambalo lilishuhudiwa likikua kwa kasi kati ya mwaka 2005 na 2010.
Na kwa sababu Bunge la 10, ndilo lililoingiza wabunge wengi wa upinzani kuliko yaliyotangulia kabla yake, iliaminika kuwa hoja zingekuwa nzito na kupelekeshana kati ya serikali na wabunge wa CCM kwa upande mmoja dhidi ya wale wa upinzani. Kila Makinda alipoangaliwa, alionekana asingeweza kumudu changamoto za bunge kubwa, lenye wabunge wengi wa upinzani.
Waliponda kuwa Uspika wa Bunge la 10 ulikuwa wa Sitta lakini Kamati Kuu ya CCM iliamua kuliondoa jina lake kwa kile kilichoelezwa alikuwa mwiba wa mafisadi wakati wa uongozi wake kwenye Bunge la Tisa. Kwamba msimamo huo, ulikuwa unakigharimu chama kwa kupakwa matope kwamba Serikali ya CCM imejaa ufisadi.
Makinda aliitwa Spika wa ufisadi, kwa maana watuhumiwa wa ufisadi ndiyo waliofanya mpango ulioingia mpaka Kamati Kuu ya CCM, kuhakikisha jina la Sitta halirudi bungeni. Kwamba hata kitendo cha Chenge kujitokeza kugombea Uspika wa Bunge, haikuwa kwa dhati, ilikuwa ni njama ya kutaka matokeo ya “tukose wote”, kuwa isionekane Sitta pekee ndiye jina lake limekatwa, kwani hata Chenge naye alikuwemo katika waliopigwa palanja.
Wapondaji hawakuishia hapo, waliongeza kuwa kuwa Spika Makinda ni spika wa viti maalum, kwamba yeye mwenyewe kwa wasifu wake na uwezo wake wa kujieleza, asingeweza kushawishi kupewa uspika wa bunge, mpaka pale aliposaidiwa na Kamati Kuu ya CCM katika kukamilisha shabaha ya kumzuia Sitta kupenya.
Hata hivyo, hayo yalikuwa ni maneno ya wapondaji, ni maneno tu ambayo wana wa Kiswahili hurahisha njia ya mkato kwa kuyabeza yasipoteze muda kuwa “hata kwenye kanga yapo”. Ni sawasawa tu na msemo kuwa kelele za chura hazimzuii ng’ombe kunywa maji. Pamoja na yote yaliyosemwa, ukweli ni kwamba Makinda alifanikiwa katika miaka yake mitano ya kuliongoza bunge.
Kwa kufanyia kazi maneno, unaweza kumnyima sifa njema Makinda ambazo anastahili kwa uongozi wake makini ndani ya bunge. Alikuwa ni spika makini, aliyefanya kazi kwa uangalifu mkubwa, huku akilinda heshima ya chombo hicho cha kutunga sheria. Zipo nyakati aliingia kwenye changamoto na kutakiwa kuamua mijadala ya bunge kwa weledi mkubwa na kweli hilo lilifanyika.
Sifa ya kwanza ianzie jinsi ambavyo bunge lilingia kwenye mtego wa kugongana na mahakama kuhusiana na sakata la uchotwaji wa fedha kwenye akaunti ya Tegeta Escrow. Ilitakiwa spika afanye uamuzi wa kiweledi bila kuchanganywa na maneno ya kila upande. Wapo waliopiga kelele kuwa suala hilo lipo mahakamani, lisiingiliwe, kuna waliosema bunge lipo huru na kwamba mahakama ndiyo iliingilia bunge.
Hati ya zuio la mahakama, kulitaka bunge lisitishe mjadala wa Tegeta Escrow iliwasilishwa bungeni. Wingu zito likatanda, huku swali kama ripoti ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusiana na kashfa ya miamala katika Akaunti ya Tegeta Escrow, ingesomwa bungeni au la, likisumbua vichwa vya wengi. Kwa hakika ulihitajika umahiri wa Makinda.
Suala la ripoti ya Tegeta Escrow kusomwa bungeni, lilikuwa ni changamoto nzito kwa Makinda kuwahi kutokea katika historia ya maisha yake akiwa Spika wa Bunge . Na pengine lilikuwa zito kulikabili na kulitolea uamuzi katika maisha yake yote ya kisiasa. Hata hivyo, kwa umakini na umahiri mkubwa, alilifanyia uamuzi mzuri kabisa.
Kabla ya kusomwa kwa ripoti, ilibidi amsimamishe Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Mtengeti Migiro, asome kanuni za bunge, asome pia muongozo wa Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge pamoja na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika maeneo yanayoonesha kuwa mahakama haina ubavu wa kulizuia bunge kuendelea na mijadala yake ambayo ilishaianza. Aliishinda mahakama kwa hoja za kisheria na kikanuni.
Huwezi kusifu mafanikio ya mjadala wa Tegeta Escrow Novemba 2014, pasipo kutoa heko zote kwa Makinda ambaye ndiye alikuwa na rungu la kuamua mjadala uendelee au usitishwe. Angekuwa ni mla rushwa au mwoga, Tegeta Escrow ingesitishwa, lakini aliangalia wapi yalipo maslahi ya Watanzania kwa upana wake, naye akapita hukohuko.
Makinda ni muwazi sana, maana ni yeye ndiye alikuwa wa kwanza kutoa tamko kuwa kwa jinsi alivyoiona ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG), kwamba kama kusingekuwa na Bunge Maalum la Katiba mwaka jana, kuna mawaziri wangepoteza kazi mapema.
Hiyo ni kuonesha kuwa Makinda alikuwa anajua madudu yaliyokuwemo kwenye ripoti ya CAG na kwamba ufisadi mkubwa ulitendeka. Kitendo cha kusimama kidete bila kuyumba kuhakikisha ripoti ya CAG kuhusu miamala iliyofanyika Benki Kuu ya Tanzania katika Akaunti ya Tegeta Escrow, inachambuliwa vizuri na PAC kisha inasomwa bungeni kama ilivyoahidiwa na kama ilivyo utaratibu wa kibunge siku zote, kilimpa hadhi kubwa katika usimamizi wake wa shughuli za bunge.
Kwa kuruhusu uwazi zaidi uonekane, wakati Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe, alipokuwa anasoma ripoti ya kamati yake baada ya kuichambua ripoti ya CAG, muda wake ulikuwa dakika 30 tu, hata hivyo, Makinda aliona kuna vitu havitaeleweka, alimuongezea muda Zitto asome uchambuzi wa kamati yake mpaka utakapoisha, siyo kwa kurukaruka vipengele.
Alimwambia: “Soma mpaka utakapomaliza.” Zitto akajibu: “Asante, asante sana mama.” Kila kitu kilikuwa na uashirio mkubwa kuwa Makinda ameweza kuongoza bunge kisasa, akikabili changamoto nzito na kupita kishujaa kabisa. Ni Bunge la 10 chini ya Makinda, lililoweka rekodi ya kuwa bunge lililowajibisha mawaziri wengi kuliko lolote lile katika historia ya Tanzania.
Kabla ya kuangaza matukio mengine ambayo yalitokea bungeni wakati wa uongozi wa Makinda na kuwajibisha mawaziri, vema kumpa heshima nyingine Makinda kwa namna alivyohitimisha mjadala wa Tegeta Escrow. Baada ya hoja iliyojengwa na PAC kupitia ripoti yake iliyosomwa bungeni, kulikuwa na kazi kubwa ya kuyaweka mapendekezo ya PAC ili kuja kuwa maazimio ya bunge.
Katika mapendekezo ya PAC, kulikuwa na lugha kali na hata kuingilia mihimili mingine. Alitaka lazima kuwe na lugha laini ya kuishauri serikali badala ya kuiamrisha. Kwa uzoefu na uelewa wake, alishaona kazi imetendeka na kila mtu ameona, hivyo haikuhitaji lugha ya kuamrisha eti ndipo serikali ingefanya uamuzi.
Baada ya bunge kuvurugika, Makinda hakutaka kufunika kombe mwanaharamu apite. Ikumbukwe kuwa siku bunge lilipovurugika kutokana na hali ya kubishana kutokana na namna ya mpangilio wa mapendekezo ili baadaye kuja kuwa maazimio ya bunge (parliamentary resolutions), ilikuwa siku ya mwisho ya kuahirishwa kwa mkutano wa 17 wa Bunge la 10.
Hata hivyo, kwa kuwa aliona umuhimu wa suala la Tegeta Escrow kufika mwisho, Makinda aliunda kamati ya maridhiano iliyokutanisha wajumbe wa PAC, wabunge wachache wa CCM, upinzani na serikali, kisha kuunda mapendekezo ambayo yalipita na kufanywa kuwa maazimio ya bunge ambayo ndiyo yalimfanya Rais Kikwete kuamua kumfuta kazi aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Mandeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka.
Maazimio hayo ya bunge ndiyo sababu ya aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Fredrick Werema, kujizulu kila mmoja kwa wakati wake, huku Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini akisimamishwa kazi kwa muda usiojulikana kupisha uchunguzi.
Kuutambua ubora wa Makinda ni lazima pia kukumbuka jinsi alivyoisimamia Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, inayoongozwa na Mbunge wa Kahama (CCM), James Lembeli, iliyochunguza madudu yaliyotokea katika Oparesheni Tokomomeza Ujangili ambapo mawaziri wanne walilamizimishwa na bunge kujiuzulu.
Waliokuwa mawaziri, Emmanuel Nchimbi (Mambo ya Ndani), Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa), Mathayo David (Mifugo) na Balozi Hamis Kagasheki (Maliasili na Utalii), waliachia ngazi kutokana na kashfa ya Oparesheni Tokomeza Ujangili kama ilivyosomwa bungeni.
Kuna mawaziri nane walioachishwa kazi na Rais Kikwete Januari 2013, kutokana na ripoti za kamati za bunge, hususan zile za mahesabu, iliyokuwa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na PAC. Mfumo wa Makinda wa kuliongoza bunge kwa misingi ya ukweli na uwazi, imekuwa sababu ya mawaziri wasiowajibika ipasavyo kukiona cha moto.
Waliokuwa mawaziri, Mustafa Mkulo (Fedha), William Ngeleja (Nishati na Madini), Cyril Chami (Viwanda na Biashara) na wengine, walijikuta wakifunguliwa milango yaa kutoka kwenye Baraza la Mawaziri kutokana na kazi ya kibunge chini ya uongozi wa Spika Makinda. Huwezi kumnyima pongezi hizi.
Mara nyingi, ilitokea kiti cha spika kinapokuwa kimekaliwa na naibu wake, Ndugai au wenyeviti, hasa kipindi ambacho Sylvester Mabumba alikuwa mmoja wa wenyeviti wa bunge, hali ilikuwa inachafuka, lakini anapokaa mwenyewe alikuwa akijua namna ya kuwatuliza wabunge na kwenda nao sawa katika kujadili hoja za kibunge.
Kwa hakika, Makinda alieweza kuifanya heshima yake kama Spika wa Bunge ikae kwenye mkondo wake na kwa hili, waliokuwa wanaamini kuwa atavuja, walibaki kushangaa alipomaliza miaka mitano ya uspika, akiwa na mafanikio mengi. Zaidi aliwathibitishia hasi (proved wrong), wale wote waliokuwa wanaamini angeshindwa.
Mwaka 2013, bunge lilikumbwa na kashfa nzito kuelekea kusomwa kwa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini. Uliibuka mjadala mzito kwamba aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi na Bodi ya Tanesco, walikiuka sheria ya manunuzi kwa kuipa zabuni kampuni iliyoshindwa kwenye mchakato wa zabuni ya ununuzi wa mafuta ghafi kwa ajili ya mitambo ya umeme.
Upande wa pili, ikadaiwa kuwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini pamoja na wabunge wengine kadhaa, walikuwa wamehongwa na makampuni ya mafuta ili kumtetea Mkurugenzi wa Tanesco aliyefukuzwa kazi, William Mhando. Kulikuwa na pande mbili zilizokuwa zinashambuliana kwa maneno mazito, kwa hoja nzito.
Uamuzi wa kwanza ambao Makinda aliufanya ni kuruhusu bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini isomwe, kisha akaivunja Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, halafu aliunda kamati ya kuchunguza tuhuma hizo ili kubaini ukweli wa kashfa hiyo. Kamati iliongozwa na Brigedia Jenerali mstaafu, Hassan Ngwilizi ambaye ni mbunge wa Mlalo (CCM).
Ripoti ilipotoka, ilibaini ukweli kwamba Maswi na waziri wake Muhongo, walilidanganya bunge kwa kuwasingizia wabunge kuhongwa na kula rushwa. Alitoa onyo kali kwa Maswi na Muhongo kwamba kama wangelidanganya bunge siku nyingine, angewachukulia hatua hali za kinidhamu.
Hoja inayojitosheleza hapa ni kuwa Makinda pamoja na uimara wake wa kusimamia vikao, amekuwa akitoa fursa ya kila tuhuma kuchunguzwa kama inavyofika bungeni na majibu kuwekwa wazi. Pale alipotoa uamuzi mbaya, alijisahihisha, mfano pale alipoivunja Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, baada ya ripoti ya Ngwilizi aliisafisha kwamba wajumbe wa kamati hiyo walisingiziwa.
Makinda alikuwa mpingaji wa vitendo vya rushwa bungeni. Wakati anafunga mjadala wa Tegeta Escrow bungeni, aliwaonya wabunge kuacha tamaa, kwa kile alichokiita kuwa tamaa zao za kuchukua fedha ndogondogo itawaponza. Aliwasisitizia kuwa kama hawataacha, kuna watakaoumbuka. Aliyasema hayo kipindi ambacho kulikuwa na tuhuma kuwa wabunge huyumbisha mijadala inayoendelea bungeni kwa sababu ya kuhongwa fedha.
Mwaka 2013, wakati sakata la rushwa lilipoibuka wakati wa Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini, Makinda alisema: “Unakuta mtu anaongea kwa jazba kweli bungeni mpaka mishipa inamtoka, unafikiri anaizungumzia nchi, kumbe mishipa inamtoka kwa sababu anafanyia kazi fedha alizopewa.”
Chukua viwango ambavyo alivionesha akiwa Spika wa Bunge, uzingatie kwamba alikuwa Naibu Spika wa Bunge kabla hajafikia hatua hiyo. Ongeza uzoefu wake wote katika siasa na utumishi wa serikali, utaona kwamba ni ‘mama mkubwa’ katika Taifa la Tanzania.
Ni bahati mbaya kuwa huwa hapewi sifa kwa namna alivyoliendesha Bunge la 10 ambalo lilikuwa na matokeo mengi yenye kusisimua.
Bunge la 10 angalau lilijenga dhana ya woga kwa watendaji serikalini, kwamba wakifanya ubadhirifu wanawajibishwa. Kongole sana Makinda!
Bunge la 10 lilipanua demokrasia ya kibunge. Liliongeza afya ya upinzani. Maana sauti za wabunge wa vyama mbalimbali zilisikika hata kwa uchache wao. Makinda ni mwana-demokrasia.
Pamoja na dosari chache au maeneo machache yenye kuweza kukosolewa, bado Bunge la 10 liliweza kuonesha nguvu zake, kwa sehemu kubwa lilijipambanua kama mhimili huru pasipo kujipendekeza kwa serikali.
Zipo nyakati CCM kupitia wingi wao, waliweza kuzuia mijadala mikali ya wapinzani, hususan ile iliyokuwa na sura ya kuiumbua serikali lakini kwa jumla, Makinda alisimama kama kiongozi mkuu wa bunge na siyo mwakilishi wa chama.
MAKINDA ALIPOTOKA
Mwaka 1975, Makinda akiwa kijana mwenye umri wa miaka 26 tu, alimvutia Rais wa Awamu ya Kwanza ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akamteua kuwa Mbunge wa Kuteuliwa, nafasi hiyo aliendelea nayo kwa miaka 10 mpaka pale Mwalimu Nyerere alipong’atuka mwaka 1985. Mbali na ubunge, Makinda aliteuliwa na Mwalimu Nyerere kushika nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwemo uwaziri.
Ubora wa Makinda, ulimvutia pia Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, aliyemteua tena kuwa mbunge mpaka mwaka 1995 alipogombea Ubunge Jimbo la Njombe Kusini na kushinda, kisha kuendelea kulishikilia jimbo hilo kila uchaguzi na bila kupingwa mpaka mwaka 2015 alipotangaza kutogombea.
Ameshakamata nyadhifa za uwaziri, ukuu wa mkoa pamoja na idara mbalimbali ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bila kusahau ujumbe na ukurugenzi wa bodi mbalimbali za mashirika ya umma.
Baada ya Uchaguzi Mkuu 2015, Makinda aliamua kukaa pembeni, hakugombea tena uspika. Hii inampambanua kama mtu asiye na uroho wa madaraka. Kijiti kimepokelewa na Ndugai, ni zamu yake sasa. Ila naamini kuwa zitakuja nyakati ndani ya bunge watu watamkumbuka Makinda ambaye alikuwa spika bora sana lakini hapewi thamani yake.

Share on Google Plus

About LUQMAN MALOTO

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment